Search

Mahubiri

Somo la 10: Ufunuo (Ufafanuzi juu ya Ufunuo)

[3-1] Barua Kwa Kanisa la Sardi (Ufunuo 3:1-6)

(Ufunuo 3:1-6)
“Na kwa malaika wa kanisa lililoko Sardi andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye na hizo Roho saba za Mungu, na zile nyota saba. Nayajua matendo yako, ya kuwa una jina la kuwa hai, nawe umekufa. Uwe mwenye kukesha, ukayaimarishe mambo yaliyosalia, yanayotaka kufa. Maana sikuona matendo yako kuwa yametimilika mbele za Mungu wangu. Basi kumbuka jinsi ulivyopokea, na jinsi ulivyosikia; yashike hayo na kutubu. Walakini usipokesha, nitakuja kama mwivi, wala hutaijua saa nitakayokuja kwako. Lakini unayo majina machache katika Sardi, watu wasioyatia mavazi yao uchafu. Nao watakwenda pamoja nami hali wamevaa mavazi meupe, kwa kuwa wamestahili. Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele za malaika zake. Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.”
 

Mafafanuzi
 
Aya ya 1: “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Sardi andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye na hizo Roho saba za Mungu, na zile nyota saba. Nayajua matendo yako, ya kuwa una jina la kuwa hai, nawe umekufa.”
Bwana anazo Roho saba za Mungu na nyota saba. Kanisa la Sardi lilikuwa na mapungufu mengi katika maisha yake ya kiimani. Hivyo, Mungu alilionya na kulitia moyo Kanisa hilo kuishi kwa imani. Mungu aliwaambia watumishi wa kanisa la Sardi, “una jina la kuwa hai, nawe umekufa.” Kwa kusema hivi, Mungu alimaanisha kuwa imani ya mtumishi wa Kanisa la Sardi ilikuwa imekufa kimatendo.
 
Aya ya 2: “Uwe mwenye kukesha, ukayaimarishe mambo yaliyosalia, yanayotaka kufa. Maana sikuona matendo yako kuwa yametimilika mbele za Mungu wangu.”
Mungu hakumruhusu tena malaika wa Kanisa la Sardi kuendelea kutokuwa na imani. Mungu alilikemea Kanisa hili kwa kuwa lilikuwa limeishi pasipo kuwa na imani kamilifu katika Neno la Mungu. Kwa kuwa kitendo cha watakatifu kuishi pasipo kuamini kwa mioyo yao yote katika Neno lote la Mungu lililoandikwa ni uthibitisho wa wazi kuwa wataishi hali wakitenda dhambi mbele ya uwepo wa Mungu.
Ikiwa watakatifu wataishi kwa imani zao katika Neno la Mungu, basi watakatifu hao watainuliwa mbele za Mungu na wanadamu hata kama ni wadhaifu. Ili tuweze kufanyika watakatifu wa jinsi hiyo ambao imani yao ni kamilifu tunapaswa kuishi kwa kuamini kwa uaminifu na kulifuata Neno la Mungu ambalo limewafanya wakatifu kuwa wakamilifu.
 
Aya ya 3: “Basi kumbuka jinsi ulivyopokea, na jinsi ulivyosikia; yashike hayo na kutubu. Walakini usipokesha, nitakuja kama mwivi, wala hutaijua saa nitakayokuja kwako.”
Watakatifu na watumishi wa Kanisa la Kwanza walipaswa kutoa sadaka kubwa isiyopimika ili kuisikia na kuitunza injili ya maji na Roho. Hivyo, Bwana aliwaambia kutoipoteza imani yao katika injili hii ya thamani ya maji na Roho, injili ambayo iligharimu sadaka nyingi na hata uhai wao ili kuweza kuipokea. Waamini ni lazima waionyeshe imani yao vizuri na matendo yake kwa Mungu kwa kuing’ang’ania injili hii ya wokovu mkamilifu, yaani injili ya maji na Roho.
Wale waliokuwa wanapaswa kukumbuka wakati wote jinsi walivyoisikia na kuiamini injili ya maji na Roho, hali wakiyaishi maisha yao kwa shukrani kwa neema ya wokovu. Wale waliozaliwa tena upya na watakatifu ni lazima wadumu katika kutafakari jinsi injili waliyoipokea toka kwa Bwana ilivyo kuu na yenye baraka. Wasipofanya hivyo, basi watajikuta wakisimama mahali pa wajinga na wasijue ni lini Bwana atakuja hapa duniani.
 
Aya ya 4: “Lakini unayo majina machache katika Sardi, watu wasioyatia mavazi yao uchafu. Nao watakwenda pamoja nami hali wamevaa mavazi meupe, kwa kuwa wamestahili.”
Hata hivyo, Bwana anatueleza hapa kuwa Kanisa la Sardi lilikuwa na waamini wachache ambao walikuwa hawajayachafua mavazi yao, yaani waliokuwa wakiishikilia imani yao. Pia Bwana anasema kuwa hawa watakatifu waaminifu wataishi kama watumishi wa Mungu, ambao wamejivika haki ya Mungu, na ambao watatembea pamoja na Bwana. Watakatifu hawa watatembea pamoja na Bwana kwa sababu imani yao imewastahilisha kutembea pamoja na Bwana.
Watakatifu ambao imani yao imethibitishwa na Mungu wanamfuata Bwana mahali popote atakapowaongoza wao kwenda. Ule ukweli kuwa hawakuyachafua mavazi yao una maanisha kuwa hawakuyatii mambo ya ulimwengu kwa kuwa walikuwa wakiliaminia Neno la Mungu. Wale waliovikwa mavazi ya haki kwa injili ya maji na Roho iliyotolewa na Bwana wanalishikilia Neno la Mungu kwa nguvu na hawafanyi mapatano na ulimwengu. Kwa maneno mengine, wanauchora na kuuweka mstari wa wazi unaowatenganisha na injili za uongo.
Wale waliovikwa mavazi meupe kwa kuamini katika injili ya Bwana wanafanya kazi kwa ajili ya injili yake na wanayaishi maisha yao katika ulimwengu yanayotembea pamoja na Bwana. Hii ndiyo sababu Bwana yupo pamoja nao wakati wote, kwa kuwa wamemfuata wakati wote kwa kuliamini Neno la Mungu.
 
Aya ya 5: “Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele za malaika zake.”
Wale watakaoushinda ulimwengu kwa kuamini katika Neno la Mungu wataishi milele hali wakiwa wamefunikwa katika haki ya Mungu kama watakatifu wake huku wakizitumikia kazi za Mungu. Pia Bwana ataithibitisha na kuikubali imani yao na atayaandika majina yao katika Kitabu cha Uzima, na majina haya hayatatoweshewa mbali milele.
Neno la Bwana wetu la ahadi linatueleza kuwa wale walio na imani ya kweli watayashinda mapambano yao ya imani dhidi ya maadui wa Mungu. “Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe.” Mavazi meupe yana maanisha ni ushindi katika vita ya imani dhidi ya maadui wa Mungu. Washindi wa imani wanapewa baraka ambazo kwa hizo majina yao hayataweza kutoweshewa mbali kamwe katika Kitabu cha Uzima. Pia majina yao yataandikwa katika Yerusalem Mpya. “Nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele za malaika zake.” Hili neno “nitalikiri” au kukiri, lina maanisha kuwa Bwana ataithibitisha imani yao.
 
Aya ya 6: “Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.”
Wale walio na imani ya kweli wanamsikia Roho Mtakatifu akiongea nao kwa kupitia Kanisa la Mungu. Kwa sababu hiyo, wanaishi pamoja na Mungu, na wanaongozwa na Roho Mtakatifu wakati wote.