Search

Mahubiri

Somo la 10: Ufunuo (Ufafanuzi juu ya Ufunuo)

[5-2] Mwana-Kondoo Aketiye Katika Kiti cha Enzi (Ufunuo 5:1-14)

(Ufunuo 5:1-14)
 
Tumeshapitia Ufunuo sura ya 5. Hapa, Neno la Mungu linatueleza kuwa Bwana ndiye atakayewaokoa na kuwahukumu wanadamu katika nyakati za mwisho. Je, huyu Bwana tunayemwamini ni nani? Neno linatueleza kuwa Yesu Kristo ni Mwokozi kwa wale wote wanaomwamini Yeye, na kwamba yeye ndiye hakimu wa wanadamu, na Mfalme wa wafalme. 
Mara nyingi tunamfikiria Yesu kuwa ni Bwana mwenye mipaka. Lakini ukweli ni kuwa Bwana wetu ni hakimu wa uumbaji wote.
Bwana alitukomboa toka katika dhambi zetu zote, toka katika hukumu, na toka katika maangamizi kwa kutupatia injili ya maji na Roho. Hivyo, Bwana alifanyika kuwa Mwokozi wetu na Mungu wa kweli. Na wakati huo huo, Bwana wetu ni Mfalme na hakimu wa wanadamu wote. Hebu tuiamshe mioyo yetu yenye shukrani kwa Bwana leo hii, Bwana ambaye tunamwamini na tunayemtegemea.
Kuanzia aya ya 1 na kuendelea, tunaona kuwa yeye aliyekuwa ameketi katika kiti cha enzi alikuwa na kitabu akiwa amekishika mkono wake wa kuume, na kwamba Mwana-Kondoo, ambaye ni Yesu Kristo alikichukua kile kitabu. Pia katika aya ya mwisho tunaona kuwa Bwana aliketi katika hiki kiti cha enzi. Neno hili linatueleza kuwa muda si mrefu Bwana atakuwa hakimu wa wanadamu wote, yaani waamini na wasio amini. Hivyo, tunaweza kufahamu na kuamini kuwa Yesu ni Mungu ambaye amefanyika kuwa hakimu wa wote.
Bwana wetu hajaziwekea ukomo thawabu na adhabu kwetu sisi tuliozaliwa tena upya tu, bali yeye ni Hakimu wa kweli na Mfalme wa wafalme kwa kila mwanadamu na kwa kila kitu kilichopo ulimwenguni. Mara nyingi watu wanasema kuwa sasa tumeingia katika karne ya 21. Na kwamba karne hii inaweza kuwa ni wakati ambapo Bwana atarudi. Basi tunaposema kuwa kurudi kwa Bwana kumekaribia ina maanisha kuwa maangamizi ya ulimwengu yamekaribia pia. 
Tunachoweza kukipata toka katika Neno hapa ni kwamba Bwana ana mamlaka ya kuwa Hakimu wa wote. Bwana wetu alikuja hapa duniani katika mwili wa mwanadamu, na alipokuwa na umri wa miaka 30 alizichukua dhambi zote za mwanadamu katika mwili wake kwa ubatizo wake mara moja na kwa wote. Yesu alihukumiwa kwa ajili ya dhambi zote za mwanadamu kwa kusulubiwa hadi kifo.
Ni Mungu Baba pekee ndiye anayeweza kupokea heshima na kuabudiwa toka katika kila mwanadamu na toka kwa kila kiumbe mbinguni na duniani. Lakini Mwana wa Mungu, Yesu Kristo alipewa haki ya kupokea heshima na kuabudiwa pamoja na Baba kwa sababu ya kuyatii na kuyatimiza mapenzi ya Mungu Baba. Hivyo, Kristo aliweza kurithi mamlaka yote toka kwa Baba.
Yesu Kristo alipewa haki ya kumhukumu kila mwanadamu, na kila mwanadamu anaokolewa na kuhukumiwa na Yesu tu. Hivyo ni jambo lenye faida sana kwetu kumfahamu kiusahihi huyu Bwana aliyetuokoa sisi. Ufahamu huu ni wa muhimu sana kwetu ili tuweze kuilinda imani yetu imara katika nyakati za mwisho. Tunapomwamini Bwana kwa ufahamu sahihi na kuufahamu uweza alionao, basi ufahamu huu unageuka na kuwa ni nguvu kubwa sana kwetu
Bwana aliyetuokoa sisi ndiye yule aliye na mamlaka ya kumhukumu kila mtu kwa mema au mabaya. Ni lazima tutambue na kuamini kuwa huyu Bwana anastahili kuabudiwa kama anavyoabudiwa Mungu Baba. Kifungu hiki cha maandiko kinatueleza kuwa Bwana wetu alikuja hapa duniani na akauawa, na kwamba kwa damu yake aliwakomboa wanadamu kwa ajili ya Mungu toka kila kabila, lugha, watu na taifa, na akawafanya kuwa wafalme na makuhani katika uwepo wa Mungu wetu ili kutawala hapa duniani.
Kisha kifungu hiki cha maandiko kinatueleza kuwa kulikuwa na sauti za malaika Mbinguni, ambao walikuwa na idadi ya makumi elfu kwa makumi elfu, na maelfu kwa maelfu, huku wakimsifu na kumwabudu Bwana kwa sauti kuu: “Astahili Mwana-Kondoo aliyechinjwa, kupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka.” Katika aya ya 13 Yohana anaendelea na ushuhuda wa kile alichokiona na kukisikia akisema: “Na kila kiumbe kilichoko mbinguni na juu ya nchi na chini ya nchi na juu ya bahari, na vitu vyote vilivyomo ndani yake, nalivisikia vikisema, Baraka na heshima na utukufu na uweza una yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na yeye Mwana-Kondoo, hata milele na milele” Je, viumbe hawa wote wanampatia nani utukufu wote? Ukweli ni kuwa baraka, heshima, utukufu na uweza zinatolewa kwa Mwana-Kondoo aketiye katika kiti cha enzi milele na milele.
Utukufu, sifa na ibada toka kwa wanadamu vilikuwa vimetengwa kwa ajili ya Mungu tu, ambaye ni Baba wa Yesu Kristo. Yesu Kristo alipewa utukufu wote pamoja na Baba kwa kuwa ana mamlaka sawa na ile ya Baba ambayo inatokana na yeye kuja hapa duniani na kuwakomboa wanadamu toka katika dhambi, maangamizi, na hukumu, na kwa sababu ya wokovu huu wa upatanisho basi Yesu amefanyika kuwa Mwokozi wetu anayestahili kuabudiwa.
Unapofikiria haya yote kuwa Bwana anayeketi katika kiti cha enzi na ambaye ni Bwana na Hakimu wa wote ni Mwokozi wetu, basi jambo hilo linatupatia utukufu mkuu unaoijaza mioyo yetu. Bwana ni Mfalme wa wafalme, Mungu wa uumbaji ambaye kwa yeye kila kitu katika ulimwengu huu kiliumbwa.
Kwa kuwa Bwana wetu ni Mungu wa uumbaji, ambaye alikuja hapa duniani na akatuokoa kwa maji na damu yake, basi anastahili kuabudiwa na kila mwanadamu na kila kitu katika ulimwengu huu kwa kupiga magoti na kusujudu mbele ya kiti chake cha enzi na kumpatia sifa, utukufu, na heshima yote. Imani yetu imetiwa nguvu sana na mioyo yetu imetiwa nguvu sana kutokana na ule ufahamu kuwa Bwana wetu ndiye anayeketi katika kiti cha enzi cha utukufu kama Hakimu wa wote.
Baadhi ya watu wanamfikiria Yesu kuwa ni kama miongoni mwa wenye hekima wanne, lakini ukweli ni kuwa Bwana si mwanadamu kwa namna yoyote ile. Bwana ni Mungu wetu aliyetuumba na kutuokoa. Hivyo hatuwezi kamwe kumlinganisha Bwana na kule kuumbwa kwetu kama wanadamu. Hata Sokrato, Konfusio, au Buddha wala mwanadamu yeyote hawezi kulinganishwa na Bwana wetu. Yesu aliishi kama mwanadamu kwa miaka 33 tu ili aweze kutuokoa. Lakini hali yake ni Mungu yuleyule. Huu unaweza usiwe mfano mzuri, lakini kama wanadamu wanavyozaa wanadamu wenzao, basi Yesu Kristo ni Mungu kwa kuwa yeye ni Mwana wa Mungu Baba.
Hivyo, Yesu ni Mungu mwenyewe, Mungu wa uumbaji wetu. Lakini Bwana alikuja hapa duniani ili kutuokoa. Kwa kuwa alituokoa, basi anastahili kupokea utukufu wote toka kwetu, na ni lazima tuamini kwa nguvu katika mioyo yetu kuwa Yesu si kiumbe, bali ni Muumbaji. Kwa kweli tunashukuru sana!
 

Bwana Wetu Anayeweza Kuutimiza Mpango wa Mungu
 
Zaidi ya Bwana Yesu hakuna anayeweza kukifungua kitabu kilichofungwa kwa mihuri saba. Kitabu hiki kilichofungwa kwa mihuri saba ni kitabu cha Mungu cha ahadi. Mungu aliumba vitu vyote hapa ulimwenguni tukiwemo sisi katika Yesu Kristo. Hata kabla ya uumbaji, Mungu alikuwa amepanga mpango katika Yesu Kristo wa kutufanya sisi kuwa watoto wake. Bwana wetu alikipokea kitabu hiki kilichofungwa kwa mihuri ili kulitimiza dhumuni la Mungu la uumbaji na mpango wake wa kutuokoa na kuwahukumu wanadamu.
Neno la Mungu linatueleza kuwa, “Wala hapakuwa na mtu mbinguni, wala juu ya nchi, wala chini ya nchi, aliyeweza kukifunga hicho kitabu, wala kukitazama.” Kwa maneno mengine, hapakuwa na yeyote aliyeweza kuukamilisha mpango wa Mungu. Ni Yesu Kristo tu ndiye anayeweza kufanya hivi. Kwa nini? Kwa sababu Mungu amepanga kila kitu kwa kupitia Mwana wake.
Hii ina maanisha pia kuwa Bwana ana mamlaka ya hukumu ya kukifungua kitabu kilichofungwa kwa mihuri saba, ambao ni mpango wa Mungu Baba. Kwa mamlaka hii, Yesu alitimiza kila kigezo cha Mungu Utatu kwa kuzichukua dhambi zetu zote katika mwili wake kwa ubatizo wake na kwa kutuokoa kwa kuadhibiwa kwa ajili ya dhambi hizo kwa ajili yetu Msalabani. Bwana ametufanya sisi kuwa makuhani wake mbele za Mungu kwa kutukomboa toka katika dhambi kwa kupitia sadaka yake na gharama ya uhai wake. .
Pia Yesu Kristo amewafanya wale wote wanaoamini katika wokovu wake kutawala pamoja naye. Kama Neno la Mungu linavyotueleza, “Tutatawala duniani,” wakati Bwana atakaporudi hapa duniani, Bwana atavishinda vitu vyote tena na kisha atauleta Ufalme wa Milenia katika uhalisia wake hapa duniani.