Search

Mahubiri

Somo la 11: Maskani

[11-10] Imani Iliyodhihirishwa katika Birika la Kunawia (Kutoka 30:17-21)

Imani Iliyodhihirishwa katika Birika la Kunawia
(Kutoka 30:17-21)
“BWANA akanena na Musa, na kumwambia, Fanya na birika la shaba, na kitako chake cha shaba, ili kuogea; nawe utaliweka kati ya Hema Takatifu la Kukutania na madhabahu, nawe utalitia maji. Na Haruni na wanawe wataosha mikono yao na miguu yao humo; hapo waingiapo ndani ya Hema Takatifu la Kukutania; watajiosha majini, ili wasife; au hapo watakapoikaribia madhabahu ili watumike, kumteketezea BWANA sadaka ya moto; basi wataosha mikono yao na miguu yao ili kwamba wasife; na neno hili litakuwa amri kwao milele, kwake yeye na kwa wazao wake katika vizazi vyao vyote.’”
 
 
Birika la Kunawia Katika Ua wa Hema Takatifu la Kukutania
 
Birika la shaba
Vifaa: Ilitengenezwa kwa shaba, ilikuwa imejazwa maji wakati wote.
Maana ya kiroho: Shaba inamaanisha hukumu ya dhambi zote za wanadamu. Ili kubeba adhabu ya dhambi zote za wanadamu, Yesu alizichukua dhambi za ulimwengu katika mwili wake kwa kubatizwa na Yohana. Kwa hiyo, maana ya birika la kunawia ni kwamba tunaweza kuoshwa dhambi zetu zote kwa kuamini kwamba dhambi hizi zote zilipitishwa kwa Yesu kwa kupitia ubatizo wake.
Makuhani waliohudumu katika Hema Takatifu la Kukutania pia waliiosha mikono yao na miguu yao katika birika la kunawia kabla ya kuingia katika Hema Takatifu la Kukutania na kwa hiyo walikiepuka kifo chao. Shaba inamaanisha hukumu ya dhambi, na maji ya kwenye birika la kunawia yanamaanisha ubatizo ambao Yesu aliupokea toka kwa Yohana na ambao kwa huo alizichukua dhambi za ulimwengu katika mwili wake. Kwa maneno mengine, birika la kunawia linatueleza kuwa Yesu alizipokea dhambi zetu zote zilizopitishwa kwake na akabeba adhabu ya dhambi hizi. Maji katika birika la kunawia yanamaanisha, katika Agano la Kale, nyuzi za bluu za Hema Takatifu la Kukutania, na katika Agano Jipya, ubatizo ambao Yesu aliupokea toka kwa Yohana (Mathayo 3:15, 1 Petro 3:21).
Kwa hiyo, birika la kunawia linamaanisha ubatizo wa Yesu, na ni mahali ambapo tunathibitisha imani yetu katika ukweli kuwa Yesu alibeba dhambi zetu zote, zikiwemo dhambi zetu halisi, na akazioshelea mbali zote mara moja kwa kupitia ubatizo alioupokea toka kwa Yohana Mbatizaji takribani miaka 2,000 iliyopita.
Kuna wenye haki katika ulimwengu huu ambao wamezaliwa upya kwa kuiamini injili ya maji na Roho. Ni wale ambao wamepokea ondoleo la dhambi zao kwa kuamini kwamba dhambi zao zote zilisamehewa kwa kazi za Yesu zilizodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Hata hivyo, kwa sababu hata wenye haki ambao wamepokea ondoleo la dhambi wana mapungufu katika miili yao, na hawawezi kukwepa bali watatenda dhambi kila siku, basi dhambi za jinsi hiyo zinaitwa dhambi halisi. Mahali ambapo wenye haki ambao wamepokea ondoleo lao la dhambi halisi si pengine bali ni katika hili birika la kunawia. Kila inapotokea kuwa mwenye haki ametenda dhambi halisi, basi wanakuja katika birika la kunawia katika ua wa Hema Takatifu la Kukutania na kisha wanaiosha miguu yao na mikono yao, na ndipo wanapoweza kuthibitisha ukweli kuwa Yesu Kristo amekwisha wasamehe dhambi zao halisi zote kwa kuliamini Neno la Mungu lililoandikwa.
Katika Biblia, maji kwa baadhi ya nyakati yametumika kumaanisha pia Neno la Mungu, lakini maana muhimu kabisa ya maji ni ubatizo wa Yesu. Waefeso 5:26 inasema, “ili makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno,” na Yohana 15:3 inasema, “Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya lile neno nililowaambia.” Birika la kunawia linawawezesha watakatifu ambao wamepokea ondoleo la dhambi zao kuumiliki uhakika kwamba Bwana amezisamehe dhambi zao zote kwa maji hata kama miili yao ina mapungufu kiasi gani.
1 Petro 3:21 na 22 inaeleza, “Mfano wa mambo hayo ni ubatizo, unaowaokoa ninyi pia siku hizi; (siyo kuwekea mbali uchafu wa mwili, bali jibu la dhamiri safi mbele za Mungu), kwa kufufuka kwake Yesu Kristo. Naye yupo mkono wa kuume wa Mungu, amekwenda zake mbinguni, na malaika na enzi na nguvu zikiisha kutiishwa chini yake.” Kabla ya aya hizi, Petro anaeleza maana ya kiroho ya maji katika siku za Nuhu. Pamoja na kuwa Nuhu aliwaonya wenye dhambi, kwa maneno mengine nafsi zilizokuwa zimefungwa katika dhambi, juu ya gharika ambayo itasafisha uchafu wote wa ulimwengu wa kwanza, ni wanane tu ndio waliookolewa na gharika ya maji. Maji ya gharika katika wakati ule yakawaua wote ambao hawakuliamini Neno la Mungu. Na sasa, Petro anaelezea toka katika lile tukio la gharika kwamba ubatizo wa Yesu ni mfano wa maji haya. Kwa hiyo, birika la kunawia ni mahali ambapo tunauthibitisha wokovu wetu tena mbele za Mungu kabla na baada ya kuokolewa.
Watakatifu ambao wameokolewa toka katika dhambi zao kwa imani wamevishwa neema ya Mungu kwa kuyaamini maji ya kwenye birika la kunawia (ubatizo wa Yesu), shaba (hukumu ya Mungu kwa dhambi zote), na kwamba Yesu amewakomboa toka katika dhambi zao. Ingawa tuna wingi wa udhaifu na mapungufu kiasi kwamba hatuwezi kujitambua sisi wenyewe kuwa ni wenye haki, kwa hakika tunaweza kuthibitisha kwamba sisi ni wenye haki wakamilifu kwa kuiweka tena na tena imani yetu katika ubatizo wa Yesu (kuzibeba dhambi, maji) na damu yake iliyomwagwa Msalabani (adhabu ya dhambi, shaba). Kwa sababu tunaliamini Neno la Mungu ambalo limekwisha kutuokoa sisi sote toka katika dhambi zetu na adhabu ya dhambi hizi, basi tunaweza kufanyika wenye haki wasio na dhambi.
Neno la Mungu ambalo tunaliamini linatueleza sisi kuwa Yesu alizichukua dhambi zetu katika mwili wake kwa kupitia ubatizo wake alioupokea toka kwa Yohana, akamwaga damu yake Msalabani ili kuibeba adhabu yote ya dhambi badala yetu, na kwa hiyo ametuokoa sisi kikamilifu toka katika dhambi zetu. Mungu aliliweka birika la kunawia katika ua wa Hema Takatifu la Kukutania ili kwamba tuweze kuthibitisha kwa imani yetu kuwa sisi ndio tuliookolewa kikamilifu toka katika dhambi zetu zote bila kujali hali inavyoweza kuwa.
 
 
Je, Umekombolewa Daima Toka Katika Dhambi Zako Halisi?
 
Katika karamu ya mwisho, baada ya kushiriki mkate wa Pasaka na kinywaji akiwa na wanafunzi wake, Yesu, kabla hajafa Msalabani, alitaka kuiosha miguu ya Petro na wanafunzi wengine kwa maji. Kwa sababu Yesu alikuwa amekwisha chukua dhambi zote za wanafunzi wake kwa kupitia ubatizo wake alioupokea toka kwa Yohana, alitaka kuwafundisha juu ya ukweli wa birika la kunawia. Baada ya kubatizwa, Yesu aliwaambia kuwa, yeye, kama Mwanakondoo wa Pasaka, ataulipa mshahara (kifo) cha dhambi kwa kuuawa mtini. Kwa hiyo, wanafunzi kumi na mbili wa Yesu, ingawa walibaki na mapungufu baada ya kumwamini, lakini hawakuweza kamwe kuwa wenye dhambi.
Vivyo hivyo, ukweli kuwa Yesu aliiosha miguu yao kuliwathibitishia wao juu ya kile ambacho Neno la kweli lilishuhudia―kwamba Yesu amekwisha ziosha dhambi zao zote za ulimwengu. Hivyo ndivyo ambavyo wanafunzi wa Yesu walikuwa wakihubiri kwa watu wa ulimwengu kwamba Yesu ni Mwokozi na wakaieneza injili ya maji na Roho ambayo Yesu alikwisha itimiza (Waebrania 10:1-20). Hivyo birika la kunawia linawaruhusu wenye haki waliookolewa toka katika dhambi zao zote kwa kuuamini ukweli na kuukumbuka ubatizo wa Yesu. Pia linatoa uhakika wa wokovu kwamba Mungu mwenyewe amewakomboa.
 
 
Biblia Haitaji Juu ya Kipimo cha Birika la Kunawia
 
Wakati vipimo vya kila kitu katika Hema Takatifu la Kukutania vimetajwa, kipimo cha birika la kunawia hakijatajwa. Hii inatuonyesha ukweli kuwa Yesu Mwana wa Mungu alizichukua dhambi zetu katika mwili wake kwa ubatizo wake, na kwa kweli jambo hili ni kubwa. Pia inatueleza kwamba upendo wa Yesu ambaye ametuokoa toka katika dhambi zetu na adhabu kwa kweli hauna kikomo. Birika la kunawia linadhihirisha upendo mkuu wa Mungu kwamba haupimiki. Wanadamu wamefungwa kuendelea kutenda dhambi kwa kadri wanavyoishi. Lakini kwa kuzichukua dhambi zote za ulimwengu katika mwili wake kwa kupitia ubatizo wake alioupokea toka kwa Yohana, na kwa kusulubiwa na kuimwaga damu yake Msalabani, Yesu amezitowesha dhambi zetu milele.
Birila la kunawia lilitengenezwa kwa kuyeyusha vioo vya shaba vya wanawake waliohudumu katika Hema Takatifu la Kukutania (Kutoka 38:8). Hii inamaanisha kuwa Neno la Mungu linawaangazia mwanga wa wokovu wenye dhambi na linawaondolea giza. Ni lazima tutambue kuwa Mungu amelifanya birika la kunawia ili kwamba yeye mwenyewe aweze kuziosha dhambi zetu. Neno hili la kweli limeziangazia mwanga dhambi za watu zilizofichika katika vina vya mioyo yao, limeziosha dhambi zao daima, na limewapatia ondoleo la dhambi, na hivyo limewageuza na kuwafanya wenye haki. Kwa maneno mengine, birika la kunawia linafanya kazi ya kuishuhudia kweli kwamba Yesu Kristo ametuokoa sisi wenye dhambi kikamilifu kwa Neno la Mungu.
 
 
Birika la Kunawia Lilitengenezwa Pia Kwa Shaba
 
Je, unaufahamu umuhimu wa shaba iliyotumika katika kutengenezea birika la kunawia? Shaba inamaanisha ni adhabu ya dhambi ambayo tulipaswa kuikabili. Ili kuielezea kwa ufasaha zaidi, hii shaba inatueleza kwamba Yesu alizibeba dhambi zetu zote Msalabani kwa ubatizo wake na aliadhibiwa kwa niaba yetu. Ilikuwa ni sisi ndio tuliostahili kuadhibiwa kwa ajili ya dhambi zetu, lakini kwa kupitia maji ya birika la kunawia, basi tunaweza kuthibitisha tena kuwa dhambi zetu zote zimesafishwa na kutakaswa. Wale wanaoamini katika hili wanafanyika kuwa ni wale waliohukumiwa kwa kupitia imani yao, na kwa hiyo hawakutani tena na hukumu zaidi.
Birika lililojazwa na maji linatueleza sisi kuwa, “kwa kupitia nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa, Yesu amekwisha kuzisafisha dhambi zako na amekwisha kukuokoa kikamilifu toka katika dhambi zako. Amekufanya kuwa safi.” Kwa maneno mengine, birika la kunawia, ni uthibitisho chanya kwa wenye haki waliopokea ondoleo la dhambi na kwamba wamesafishwa dhambi zao na wameokolewa.
Miongoni mwa vifaa vya Hema Takatifu la Kukutania, madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa inamaanisha hukumu ya dhambi, wakati birika la kunawia, linahusianishwa na nyuzi za bluu zinazotueleza sisi kuwa Yesu alichukua dhambi zetu katika mwili wake kwa ubatizo wake katika Agano Jipya.
Tunaweza kuingia Mahali Patakatifu pale tu tutakapofungua na kuingia katika lango la ua wa Hema Takatifu la Kukutania, tukiipita madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa, na kisha tukilipita birika la kunawia linalofuata. Wale wanaoweza kuingia katika Hema Takatifu la Kukutania ni wale tu ambao wamekwishaipitia madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na birika la kunawia kwa imani. Ni wale tu waliopokea ondoleo la dhambi kwa kuuamini ukweli wa birika la kunawia katika ua wa nje wa Hema Takatifu la Kukutania ndio wanaoweza kupaingia Mahali Patakatifu.
Wakati mtu anapojaribu kupaingia Mahali Patakatifu kwa kutumia nguvu zake, moto utatoka Mahali Patakatifu na kumwangamiza mtu huyu. Hata watoto wa Haruni hawakuwa na ruhusa ya kuihalifu amri hii, na kwa kweli baadhi yao walikufa kama matokeo ya kutotii maagizo hayo (Mambo ya Walawi 10:1-2). Wale ambao hawaifahamu kazi ya haki ya Mungu ya kuibeba dhambi na hukumu na wana udharau ukweli huu basi watauawa kwa sababu ya dhambi zao. Watu wanaojaribu kuingia katika Ufalme wa Mungu kwa kuamini kwa mujibu wa mawazo yao binafsi badala ya kuamini kwa mujibu wa wokovu wake wa Mungu ulifafanuliwa toka katika dhambi, basi watu hao kwa hakika watakumbana na hukumu ya moto kwa sababu ya dhambi zao. Kwa sababu ya hukumu ya dhambi isiyoepukika, kinachowangojea wao kama matokeo ni kuzimu tu.
Yesu aliutimiza wokovu wetu toka katika dhambi kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa ili kwamba tuweze kuingia katika Mahali Patakatifu. Ni kwa kuamini katika ukweli huu kwamba tumeokolewa kikamilifu toka katika dhambi zetu zote. Mungu aliandaa mpango wake wa kuwaokoa wanadamu toka katika dhambi hata kabla ya uumbaji, na hebu sisi tuyafahamu mapenzi yake kwa kina kwa kupitia ukweli wa nyuzi za bluu (ubatizo wa Yesu), nyuzi nyekudu (kifo cha Yesu Msalabani), na nyuzi za zambarau (Mungu alifanyika mwanadamu) katika Biblia. Na kwa mujibu wa mpango huu, kwa kweli amewaokoa wenye dhambi wote toka katika dhambi na maovu yao kwa kupitia kazi za Yesu zilizodhihirishwa katika nyuzi hizi za bluu, zambarau, na nyekundu.
1 Yohana 5:4 inasema, “na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu,” hii inafuatwa na aya ya 10, inayosema, “Yeye amwaminiye Mwana wa Mungu anao huo ushuhuda ndani yake.” Je, ushuhuda huu wa wokovu ni upi? Injili ya kweli ambayo imetupatia wokovu wetu kwa kupitia maji, damu, na Roho ni ushahuda wa imani yetu katika Mwana wa Mungu (1 Yohana 5:6-8). Kwa maneno mengine, ni injili ya maji na Roho tu ambayo tunaiamini ndio ushuhuda kwamba Mungu ameziosha dhambi zetu na ametufanya kuwa watu wake mwenyewe. Njia pekee ya sisi kuokolewa toka katika dhambi zetu, na kuingia Mahali Patakatifu, na kuula mkate wa uzima uliotolewa na Mungu, na kuishi katika neema yake ni kwa kuiamini injili hii ya maji na Roho. Kwa kuiamini injili ya maji na Roho ambayo inazisafisha dhambi zetu, ni lazima sasa tuokolewe na kuishi maisha yetu ya imani kwa kuungana na Kanisa la Mungu.
Ni kwa ukweli wa injili ya maji na Roho ndipo tunapoweza kujilisha katika Neno la Mungu katika Kanisa lake, tukiungana na Kanisa lake, na kisha tuishi kama wenye haki ambao maombi yao yanasikilizwa na Mungu. Tunapoamini katika ukweli huu, tunaweza kufanyika wenye haki ambao tuna imani ya nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu, na ambao wanaishi wakiwa wamefunikwa na neema ya Mungu mbele ya uwepo wake. Maisha ya imani ambayo yanawezekana kuishi na watu wa Mungu tu yanatokana na kuamini katika maji, damu, na Roho. Tunaweza kuokolewa toka katika dhambi zetu kwa kuamini kwa mioyo yetu yote katika ubatizo wa Yesu, damu yake iliyomwagika na kifo, na kwamba Yesu ndiye Mungu mwenyewe. Imani ambayo imekuwezeshwa wewe kuishi katika Kanisa la Mungu ni imani ya nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa.
Siku hizi, watu wengi wanasema, “Kitu tunachotakiwa kukifanya ni kumwamini tu Yesu; kwa nini kujitaabisha na mambo haya yote yanayochanganya? Hebu tusipoteze muda wetu kwa mazungumzo yasiyo na maana na hebu tuamini kwa njia yoyote ambayo tunafikiri kuwa inafaa.” Kwa watu wa jinsi hiyo, tunaweza tukaonekana kuwa sisi ni wasumbufu katika Ukristo, lakini kitu ambacho ni wazi kabisa ni kuwa ikiwa mtu anamwamini Yesu hali hajapokea ondoleo la dhambi, mtu huyu atakutana na adhabu ya milele. Kutoamini kikamilifu katika injili ya maji, na damu, na Roho ni makosa na ni imani potofu. Kwa kweli ni sawa na kutomwamini Yesu kuwa ni Mwokozi.
Ikiwa mimi, ili kupata upendeleo wa mtu fulani mgeni, nitaendelea kukazia kwa upofu kwa mgeni huyu, “Ninakuamini wewe,” je, mtu huyu atashawishika, “Kweli mtu huyu inawezekana ananiamini mimi,” na kuwa na furaha kuhusu imani hiyo? Kwa upande mwingine, pengine anaweza kusema, “Unanifahamu mimi? Sifikiri kama ninakufahamu wewe.” Ikiwa nitamwambia tena, “Lakini hata hivyo mimi bado ninakuamini,” na halafu nikamwangalia kwa macho ya ukakamavu ili kujaribu kumfanya ajisikie vizuri, je ataifurahia hali hiyo? Kwa kweli inawezekana akaniona mimi kama mtu anayejikomba na asiye msimamo, ambaye anajaribu kuyasoma mawazo yake na kuunyakua upendeleo wake.
Hata Mungu hapendezewi na watu ambao wanamwamini kiupofu. Tunaposema, “Ninamwamini Mungu. Ninamwamini Yesu kuwa ni Mwokozi wa wenye dhambi,” basi ni lazima tuikiri imani yetu kwake baada ya kufahamu na kuamini jinsi ambavyo Yesu ameyashughulikia maovu ya wenye dhambi. Ikiwa tunaamini kimakosa na kwa upofu, kana kwamba hatuna tabia kabisa, basi kwa kweli hatuwezi kuokolewa. Tunaokolewa pale tunapofahamu kwanza kwa wazi jinsi ambavyo Yesu amezifanya dhambi zetu kutoweka. Tunaposema kwamba tunamwamini mtu fulani, tunayaweka matumaini yetu ya kweli katika mtu huyu kwa sababu tunamfahamu vizuri na tunamchukulia mtu huyu kuwa ni wa kuaminika. Kuweka matumaini kwa mtu ambaye hatumfahamu vizuri inaweza kumaanisha kuwa sisi tunadanganya au sisi ni wajinga ambao tunastahili kusalitiwa. Kwa hiyo, tunapokiri kumwamini Yesu, ni lazima tufahamu kikamilifu jinsi ambavyo Yesu amezifanya dhambi zetu kutoweka. Ni hapo tu ndipo hatutaweza kuachwa na Bwana wetu katika siku ya mwisho na kisha kuingia Mbinguni kama wana wa Mungu waliozaliwa upya.
Imani ya kweli inayoweza kutuongoza sisi kwenda mbinguni ni imani ya nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu. Kwa maneno mengine, imani ya kweli ni kuamini katika injili ya maji na Roho ambayo imetuokoa kwa kupitia maji (ubatizo wa Yesu), na damu (kifo cha Yesu), na Roho Mtakatifu (Yesu ni Mungu). Ni lazima tufahamu jinsi ambavyo neema ya Bwana wetu ni kubwa ambayo imetuokoa sisi, na kisha tuiamini, kwa kuwa kuuamini ukweli huu kutatupeleka katika wokovu wetu.
Kwamba imani ya mtu fulani ni kamilifu au si kamilifu inafahamika ikiwa mtu huyu anaufahamu au haufahamu ukweli. Unaweza kumwamini Yesu kuwa ni Mwokozi wako pale tu unapoiamini injili ya maji na Roho kwa moyo wako wote. Na imani hii katika Yesu kuwa ni Mwokozi wetu, ambaye ametupatia sisi ondoleo la dhambi kwa kupitia injili ya maji na roho, ni imani ya kweli iliyotuokoa sisi toka katika dhambi zetu zote.
 
 

Birika la Kunawia ni Uthibitisho wa Wokovu Uliozisamehe Dhambi Zetu

 
Birika la kunawia lilijazwa maji. Liliwekwa upande wa kulia mbele ya Mahali Patakatifu. Birika la kunawia ni mahali ambapo tunajikumbusha sisi wenyewe kuwa tumepokea ondoleo la dhambi, na tunathibitisha kupokea huko kwa imani. Ni uthibitisho wa ukweli kwamba Mungu amezisafisha dhambi zote za waamini. Kama ambavyo makuhani walihudumu katika Mahali Patakatifu wakaosha miguu yao na mikono yao katika birika la kunawia kila walipochafuka, vivyo hivyo, wale waliopokea ondoleo la dhambi, inapotokea kuwa wamefanya dhambi, basi na wao pia wanaziosha dhambi hizo kwa kujikumbusha wao wenyewe na kukiri tena, kwa kupitia Neno la Mungu, kwamba Yesu amekwisha zitowesha dhambi zao zote na pia amewapatanisha kwa kuhukumiwa na kuadhibiwa kwa haki.
Tunachafuliwa na dhambi kwa sababu hatuwezi kukwepa bali tunaendelea kutenda dhambi kadri tunavyoishi katika ulimwengu huu. Je, tutatumia kitu gani kujisafisha na dhambi hizi ambazo zinatuchafua? Tunazioshelea mbali hizo dhambi kwa kuamini kwamba Yesu Kristo, Mfalme wa wafalme, alikuja hapa duniani takribani miaka 2,000 iliyopita katika mwili wa mwanadamu ili kuwaokoa wenye dhambi, akazichukua dhambi zao katika mwili wake kwa kupitia ubatizo wake, akamwaga damu yake Msalabani, na kwa hiyo amezisamehe dhambi zote za wenye dhambi. Tunaweza kupokea ondoleo la dhambi na pia kuzioshelea mbali dhambi zetu halisi pale tu tunapoamini katika ukweli kuwa Yesu alizichukua dhambi zote katika mwili wake kwa kubatizwa. Kwa maneno mengine, pia tunaweza kusafishwa dhambi zetu halisi pale tu tunapouamini ukweli huu kwamba Mungu amekwisha zisafisha dhambi zetu zote kwa kupitia nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu.
 
 
Ni Lazima Tuwe na Imani Inayofahamu na Kuamini Katika Ukweli wa Birika la Kunawia
 
Pasipo kuwa na imani katika birika la kunawia, hatuwezi kuingia Mahali Patakatifu ambapo Mungu anaishi. Matendo yetu hayawezi kuwa sahihi wakati wote. Kwa sababu tuna mapungufu, tunafanya dhambi katika nyakati fulani. Lakini wokovu ambao Mungu ametupatia kwa hakika ni mkamilifu, kwa kuwa Neno la Mungu ni kamilifu. Kwa sababu Mungu ameyaoshelea mbali mapungufu yetu kwa wokovu wake mkamilifu, tunaweza kupaingia kwa ujasiri Mahali Patakatifu kwa imani. Wale ambao hawapitii katika birika la kunawia hawawezi kuingia kamwe katika Mahali Patakatifu. Tunafanywa kuwa wanaofaa kuingia katika Mahali Patakatifu kwa imani yetu katika ukweli kwamba Yesu alikuja hapa duniani miaka 2,000 iliyopita na akazitowesha dhambi zote za ulimwengu kwa injili ya maji na Roho, na damu na Roho Mtakatifu vilivyotabiriwa kwa kupitia nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu. Pasipo kuamini kuwa Bwana amekwisha zitowesha dhambi zetu zote na kutufanya kuwa wasio na dhambi, kwa kweli hatuwezi kupaingia Mahali Patakatifu.
Kama ambavyo hatuwezi kupaingia mahali patakatifu pa Mungu pasipo kuamini katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu, basi ikiwa hatuamini katika injili ya maji na Roho, vivyo hivyo hatuwezi kuifurahia baraka ya kwenda mbele za kiti cha enzi cha neema ya Mungu kwa kuliamini Neno lake katika Kanisa lake, ya kumwomba Mungu na kupokea neema yake, na ya kuishi na watumishi na watakatifu wake. Tunaweza kuishi maisha yetu katika Kanisa la Mungu pamoja na ndugu zetu waamini, hali tukisikia na kuamini katika Neno lake na kumwomba Mungu, pale tu tunapoamini kuwa Mungu amekwisha tuokoa toka katika dhambi zetu kwa kupitia nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu.
Birika la kunawia ni uthibitisho wa mwisho wa wokovu wetu toka katika dhambi. Mungu aliliweka birika la kunawia mbele ya Mahali Patakatifu na akaijaza maji ili kutoa uthibitisho wa imani kwa wale wanaoamini katika injili ya ondoleo la dhambi. Birika hili la kunawia linasafisha dhamiri iliyochafuliwa ya mwenye haki anayeamini.
Hebu tusome 1 Yohana 2:1-2. “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote.” Amin.
Ikiwa tunatenda dhambi, tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki. Yesu anaiosha mioyo iliyochafuliwa ya wenye haki kwa maji na anaifanya kuwa safi. Siku ile kabla ya kusulubiwa, wakati wa chakula cha mwisho Yesu aliwakusanya wanafunzi wake pamoja, akaweka maji katika beseni, na akaanza kuiosha miguu yao. “Wakati nilipobatizwa, nilizibeba dhambi zenu zote, zikiwemo dhambi ambazo utazifanya baadaye, na nitaadhibiwa Msalabani kwa ajili yake. Pia nilizichukua hata dhambi zako zinazokuja baadaye katika mwili wangu, na nikazitoweshea mbali. Mimi nimefanyika kuwa Mwokozi wako.”
Pia ni kusema hivi kuwa Yesu aliiosha miguu ya wanafunzi katika chakula cha mwisho cha Pasaka. Akamwambia Petro ambaye alikataa kuoshwa miguu na Yesu, akasema, “Yesu akajibu, akamwambia , Nifanyalo wewe hujui sasa; lakini utalifahamu baadaye” (Yohana 13:7). Yesu alitaka kufanyika Mwokozi mkamilifu wa wale ambao wanaamini kwa kweli katika injili ya maji na Roho. Kwa wale wanaoamini katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu, Yesu amefanyika Mwokozi wao wa milele.
 
 
Matumizi ya Birika la Kunawia
Matumizi ya Birika la KunawiaBirika la kunawia lilitumika katika kuosha uchafu wote wa makuhani walipofanya kazi katika Hema Takatifu la Kukutania wakitoa sadaka kwa Mungu. Ilihitajika kuyaosha madoa na uchafu ambayo makuhani waliyapata katika kuua mwanasadaka wa kuteketezwa, katika kuikinga damu yake, na katika kuikata vipande ili kumtolea Mungu sadaka ambayo itawapatanisha watu wa Israeli na Mungu toka katika dhambi zao. Wakati makuhani walipochafuliwa walipokuwa wakitoa sadaka, iliwapasa kuoshwa kwa maji, na birika la kunawia lilikuwa ni mahali ambapo uchafu huu wote ulisafishwa.
Tunapofanya dhambi, kiroho au kimwili, na kila inapotokea kuwa tumechafuliwa kwa kuzivunja amri za Mungu, ni lazima tuoshelee mbali uchafu wetu wote katika birika hili la kunawia. Ilipotokea kuwa miili ya makuhani imegusa kitu chochote kichafu, walipaswa kwa lazima kuosha sehemu zilizochafuka katika miili yao kwa maji.
Vivyo hivyo, inapotokea kuwa wale wanaoamini katika Mungu wamegusana na kitu chochote kisicho safi na kichafu, maji ya birika la kunawia yanatumika kuoshelea mbali huo uchafu wote. Kwa kifupi, maji ya birika la kunawia yalitolewa ili yatumike katika kuuosha uchafu wa waliozaliwa upya. Kwa hiyo, birika la kunawia lina rehema za Mungu. Maana ya birika la kunawia si kitu cha kuchagua ambacho tunaweza kuchagua kuamini au kutoamini, bali ni kitu cha muhimu na lazima kwa wale wanaomwamini Yesu.
Mungu aliweka vipimo kwa vifaa vingine vyote katika Hema Takatifu la Kukutania, akatoa vipimo maalum jinsi ambavyo vitakuwa na dhiraa kadhaa kwa kimo, urefu, na upana. Lakini hakutoa kipimo cha birika la kunawia. Hii ni tabia ambayo inapatikana tu katika birika la kunawia. Hii inadhihirisha upendo usiokoma ambao Masihi ametupatia sisi, ambao tunatenda dhambi halisi kila siku. Katika upendo huu wa Masihi kunapatikana ubatizo wake, aina ya kuwekewa mikono ambayo inaziosha dhambi zetu zote. Kama ambavyo maji mengi yalitumika wakati makuhani walipokuwa wamechafuka wakati wakitekeleza majukumu yao, ilikuwa ni lazima birika la kunawia lijazwe maji wakati wote. Kwa hiyo, kipimo cha birika la kunawia kilitegemeana na hitaji hili. Kwa sababu birika la kunawia lilitengenezwa kwa shaba, basi kila ilipotokea makuhani wakinawa, walikuwa wanafikiria juu ya hukumu ya dhambi.
Makuhani waliokuwa wanahudumu katika Hema Takatifu la Kukutania walipaswa kuoshelea mbali uchafu wote wa mikono yao na miguu yao kwa maji ya birika la kunawia. Ikiwa shaba inadhihirisha hukumu ya Mungu, basi maji yanadhihirisha kuoshwa kwa dhambi. Waebrania 10:22 inasema, “tumeoshwa miili kwa maji safi,” na Tito 3:5 inasema, “kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu.” Kama vifungu hivi vinavyoonyesha, Neno la Agano Jipya pia linatueleza sisi kuhusu kuuosha uchafu kwa maji ya ubatizo.
Ikiwa makuhani waliuosha uchafu wao walioupata katika maisha yao kwa maji ya birika la kunawia, sisi wakristo wa leo tuliozaliwa upya, tunaweza kuzioshelea mbali dhambi zetu halisi zote zilizofanywa katika maisha yetu kwa kuuamini ubatizo wa Yesu. Maji ya birika la kunawia la Agano la Kale yanatuonyesha sisi kuwa Masihi alikuja hapa duniani na amezisafishia mbali dhambi zote za ulimwengu kwa ubatizo alioupokea toka kwa Yohana.
Kwa kupitia Biblia, Mungu anatueleza sisi kuwa sio dhambi zilizofanywa na watu wa Israeli tu bali dhambi halisi zilizofanywa na watu wote katika historia nzima ya mwanadamu zote zilipelekwa kwa Yesu kwa kupitia ubatizo alioupokea toka kwa Yohana. Wakati Yesu alipobatizwa na Yohana, alisema katika Mathayo 3:15, “Kubali hivi sasa; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote.” Kwa kuupokea ubatizo wake toka kwa Yohana ambaye ni mwakilishi wa wanadamu, jambo ambalo ni sawa na kuwekewa mikono, Yesu alizipokea dhambi zote za wanadamu katika mwili wake mwenyewe.
Kwa hiyo, kwa kuamini katika ukweli kuwa dhambi zetu zote zilipitishwa kwa Yesu Masihi kwa kupitia ubatizo wake, sisi sote tunaweza kuoshwa uchafu wote wa dhambi katika mioyo yetu. Kwa sababu tulikwisha zipitisha dhambi zetu zote kwa Yesu kwa kuuamini ukweli huu, tunachotakiwa kukifanya ni kuamini kuwa Mwana wa Mungu alizichukua dhambi za ulimwengu Msalabani, alisulubiwa na akamwaga damu yake, akafanyika sadaka kamilifu ya kuteketezwa kwa wanadamu wote, na kwa hiyo ametukomboa sisi toka katika dhambi zetu zote. Je, unaamini hivi katika moyo wako? Wale ambao wanaamini kwa kweli kwamba Masihi alifanyika sadaka yetu ya kuteketezwa wameokolewa milele.
 
 

Tatizo la Dhambi Halisi Linaweza Pia Kutatuliwa Kwa Kuamini Katika Ubatizo wa Yesu

 
Je, Biblia inatueleza jinsi ambavyo tunaweza kuziosha dhambi zetu halisi? Kama ambavyo makuhani waliuosha uchafu wao kwa maji ya birika la kunawia katika Agano la Kale, katika Agano Jipya, tunaweza kupokea ondoleo la dhambi zetu halisi kwa kuamini kwamba Yesu ameitimiza haki ya Mungu kwa kuzichukua dhambi za ulimwengu katika mwili wake kwa kupitia ubatizo wake alioupokea toka kwa Yohana. Mwishoni, dhambi zote zinaoshwa kwa kuuamini ukweli huu.
Wakati watu wa Israeli walipotoa sadaka ya dhambi kwa Mungu, walileta katika Hema la Kukutania mnyama wa kuteketezwa asiye na mawaa kama vile kondoo, au mbuzi, walizitubia dhambi zao na kuzipitisha zote katika sadaka hiyo kwa kuiweka mikono yao katika kichwa cha mnyama wa sadaka, na kisha wakamuua mnyama huyu wa sadaka aliyezipokea dhambi zao. Kisha walikata koo lake na wakakinga damu yake, wakaweka damu katika pembe za madhabahu ya kuteketezwa na kisha wakaimwaga damu iliyosalia ardhini (Mambo ya Walawi 4). Hata dhambi zao za mwaka mzima zote ziliondolewa mara moja kwa imani kwa kupitia sadaka ya dhambi ya siku ya Upatanisho (Mambo ya Walawi 16). Mwishoni, tunapokea ondoleo la dhambi zetu kwa njia ile ile kama sadaka ya dhambi ya Agano la Kale—hii ni kusema kuwa, kwa kuamini katika ubatizo wa Masihi aliyekuja kuzitowesha dhambi zetu na katika damu ya Msalaba.
Kitendo cha kuwekea mikono cha Agano la Kale ni sawa na ubatizo ambao Yesu alioupokea katika Agano Jipya. Masihi wetu alizishughulikia na kuziosha dhambi zetu zote kwa kubatizwa na Yohana na kusulubiwa. Ni kwa kazi ya ubatizo wa Masihi na damu yake Msalabani kwamba Mungu ametuokoa kikamilifu toka katika dhambi zetu zote, je nini kinahitajika kwa sisi kukifanya ili tuweze kusamehewa dhambi zetu? Tunachotakiwa kukumbuka na kuamini ni kwamba hata pale tunapotenda dhambi kila siku katika maisha yetu kwa sababu ya udhaifu wetu, dhambi hizi zote pia zimekwishaoshwa na Yesu Kristo aliyekuja kwa maji na damu. Hata kama tunamwamini Mungu, kwa sababu ya mapungufu yetu, bado tunaangukia katika udhaifu na makosa yetu. Lakini Mungu wetu, ambaye anafahamu haya yote, ametuokoa kwa kumtuma Masihi katika dunia hii, akamfanya kuzichukua dhambi za mwanadamu katika mwili wake kwa kupitia ubatizo, na akamtoa ateketezwe.
Kwa kuweka madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na birika la kunawia katika ua wa Hema Takatifu la Kukutania, Mungu ameturuhusu sisi kuzioshelea mbali dhambi zetu halisi zote zinazofanywa kila siku kabla ya kuingia Mahali Patakatifu, ambayo ni Nyumba ya Mungu. Lakini hii haimaanishi kuwa tunapaswa kuziosha dhambi zetu halisi kwa maombi ya kila siku ya toba. Kinyume chake, ni imani yetu katika ubatizo wa Masihi na damu yake Msalabani inayozisafisha dhambi zetu zote. Mungu ameweka hivyo ili wenye haki wanapofanya makosa na kufanya dhambi baada ya kumwamini Yesu, waweze kuoshwa dhambi hizo zote kwa kuamini katika ubatizo ambao Masihi, Bwana wa birika la kunawia, aliupokea.
Watu wengi wameanguka kwa kukifikiria kitendo cha Yesu cha kubeba dhambi na kule kuhukumiwa kwa ajili ya dhambi zote kana kwamba ni kitu kimoja, wanayafunga mambo haya mawili pamoja kwa upofu katika furushi moja. Lakini kwa sababu tunatenda dhambi halisi kila siku kutokana na udhaifu wetu, kuoshwa kwa dhambi na hukumu ya dhambi ni lazima vitenganishwe katika sehemu mbili. Ubatizo ambao Yesu aliupokea toka kwa Yohana na kifo chake Msalabani vilikuwa na lengo la kuzibeba dhambi zetu katika mwili wake, kuhukumiwa kwa ajili ya dhambi hizi, na kisha kutuokoa sisi kikamilifu toka katika dhambi. Katika imani hii, basi tunaweza kupokea hukumu ya dhambi zetu zote mara moja. Kwa hiyo, tatizo la dhambi zetu halisi zinazotendwa kila siku ni lazima zitatuliwe kwa kuamini katika ubatizo wa Masihi. Ni kwa kuviunganisha vitu hivi viwili, ubatizo na Msalaba, ndipo wokovu kamili mmoja unapokamilika. Huu ndio ukweli wa ondoleo kamilifu la dhambi. Kwa hiyo, kwa mujibu wa suluhisho la tatizo la dhambi zetu, ni lazima tufikiri na kuamini katika ukweli huo kwa kutofautisha kati ya ubatizo wa Yesu na Msalaba.
Wakati makuhani walipoua wanyama wa kuteketezwa katika Hema Takatifu la Kukutania, walichafuliwa na uchafu na madoa ya kurukiwa na damu. Hatuwezi hata kufikiria jinsi ambavyo walichafuka. Makuhani walipaswa kuoshelea mbali uchafu huu wote, lakini kama kusingekuwa na maji katika birika la kunawia la ua wa Hema Takatifu la Kukutania, wasingeweza kufanya hivyo. Haijalishi kama angekuwa ni Kuhani Mkuu au kuhani wa kawaida ambaye amesamehewa dhambi za mwaka mzima, pasipo kuuosha uchafu wake kwa maji ya birika la kunawia, mtu huyu asingeweza kufanya lolote zaidi ya kuendelea kuishi na uchafu huo katika mwili wake.
Hata kama Kuhani Mkuu alikuwa na aina zote za uchafu katika mwili wake, kwa sababu kulikuwa na birika la kunawia katika ua wa Hema Takatifu la Kukutania, aliweza kusafishwa wakati wote. Hata kama kuhani alisamehewa dhambi za mwaka mzima, bado ilikuwa ni kwa kuziosha dhambi za kila siku ndipo huyu mtu aliposafishwa. Mungu aliwaweka makuhani walimtolea sadaka wasafishwe uchafu wao katika birika la kunawia. Basi tunaweza kutambua kuwa ni kwanini Mungu aliweka birika la kunawia katika ua wa Hema Takatifu la Kukutania. Pia tunaweza kufahamu kuwa ni kwa nini birika hili la kunawia liliwekwa kati ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na Mahali Patakatifu.
 
 
Kwa Nini Tunahitaji Birika la Kunawia?
 
Ukweli unaodokezwa katika birika la kunawia unafunuliwa katika Yohana 13. Wakati wa Pasaka, baada ya kula Karamu ya Mwisho na wanafunzi wake, Yesu alianza kuiosha miguu ya wanafunzi wake, ikafikia zamu ya Petro. Wakati Yesu alipojaribu kuiosha miguu yake, alimwambia Petro kuinyosha miguu yake ili aweze kuiosha. Hata hivyo, Petro alikataa, akasema, “Mimi ninapaswa kuiosha miguu yako; inawezekanaje wewe Bwana kuiosha miguu yangu?”
Petro alikataa kwa sababu alifikiria kuwa ilikuwa haimpasi mwalimu kuiosha miguu ya wanafunzi wake. “Ninawezaje kudiriki kumwomba mwalimu wangu kuiosha miguu yangu? Siwezi.”
Petro aliendela kuikataa huduma ya Yesu. Basi kile ambacho Yesu alikiongea kwa Petro hapa ni kitu cha kutafakarisha kwa kina.
“Yesu akajibu, akamwambia , Nifanyalo wewe hujui sasa; lakini utalifahamu baadaye” (Yohana 13:7). Hivi ndivyo Yesu alivyomaanisha: “Huwezi kufahamu sasa kuwa ni kwa nini ninapaswa kuiosha miguu yako. Lakini jambo hili litakuwa ni ufunguo wa kutatua tatizo lako la dhambi zako halisi. Utatenda dhambi nyingi halisi kuanzia sasa na kuendelea, lakini nimekwisha zichukua hata dhambi zako halisi za baadaye katika mwili wangu, na kwa sababu ya dhambi hizi, ni lazima sasa niimwage damu yangu Msalabani. Hivyo ni lazima ufahamu na kuamini kuwa mimi ni Masihi ambaye nimezishughulikia hata dhambi zako halisi za baadaye.”
Katika mawazo ya Petro, ilionekana kuwa ni kitu kisicho cha kimaadili kwa Masihi kumuosha miguu yake, na hii ndio sababu alikataa kuoshwa. Lakini Yesu akamwambia Petro, “Utafahamu baadaye,” na akaiosha miguu yake.
“Ni pale tu nitakapokuosha miguu yako ndipo unapoweza kuwa na uhusiano na mimi. Kwa sasa hufahamu kwa nini ninakuosha miguu yako. Lakini baada ya kusulubiwa kwangu na kupaa katika Ufalme wa Mbinguni, ndipo utakapofahamu kuwa ni kwa nini niliiosha miguu yako. Kwa sababu mimi ni Masihi wako, nilikwishazibeba hata dhambi zako za baadaye kwa ubatizo wangu, na kwa kufanyika sadaka ya kuteketezwa kwa ajili ya dhambi zako, nimefanyika kuwa Mwokozi wako.”
Kama Bwana wetu alivyosema, Petro hakufahamu kitu chochote kuhusu mambo haya kwa wakati ule, lakini baada ya ufufuko wa Bwana, alikuja kulitambua jambo lile. Kwa kweli , hili lilikuwa ni tendo ambalo lilizitoweshea mbali hata dhambi zake halisi.
“Kwa sababu siwezi kukwepa zaidi ya kuendelea kutenda dhambi halisi katika ulimwengu huu, Bwana aliiosha miguu yangu ili kwamba niweze kuamini kuwa Yesu Masihi alizichukua hata hizi dhambi halisi katika mwili wake kwa ubatizo wake toka kwa Yohana Mbatizaji! Ubatizo wa Masihi ulizishughulikia hata hizi dhambi halisi za baadaye! Yesu alizichukua dhambi hizi zote katika mwili wake kwa ubatizo wake, akazibeba dhambi za ulimwengu Msalabani, akabeba adhabu ya dhambi hizi zote kwa kusulubiwa! Kwa kweli ametuokoa sisi kikamilifu toka katika dhambi zetu zote kwa kufufuka tena toka kwa wafu!”
Ni mpaka baadaye, hata baada ya kumkana Bwana mara tatu, ndipo Petro alipokuja kufahamu na kulitambua jambo hili. Hii ndiyo sababu Petro alisema hivi katika 1 Petro 3:21, “Mfano wa mambo hayo ni ubatizo, unaowaokoa ninyi pia siku hizi; (siyo kuwekea mbali uchafu wa mwili, bali jibu la dhamiri safi mbele za Mungu), kwa kufufuka kwake Yesu Kristo.” Hapa, neno ‘mfano’ maana yake “yule ambaye anaonyeshwa kama kivuli au anayetambulika kwa alama ya awali au mfano, kama vile mtu mashuhuri katika Agano Jipya ambaye ana kitu cha kufafanishwa katika Agano la Kale.” Kwa hiyo, muktadha unaotangulia kwa kweli unaonyesha kwa wazi kuwa ubatizo wa Yesu ni mfano halisi wa ‘maji’ katika Agano la Kale.
Katika Agano la Kale, wakati sadaka ya dhambi ya Siku ya Upatanisho ilipotolewa kwa Mungu ili kupokea ondoleo la dhambi la mwaka mzima, Kuhani Mkuu, akiwawakilisha watu wa Israeli, alipaswa kuiweka mikono yake katika sadaka ya kuteketezwa na kisha kukiri na kutubu dhambi ambazo waisraeli wamezifanya ili kuzipitisha dhambi zao kwa mwanasadaka huyo. Njia hii ya kuweka mikono ilikuwa na muundo mmoja na ubatizo wa Yesu. Katika Agano la Kale, sadaka ya kuteketezwa ilipaswa kutoa damu hadi kifo kwa sababu ilikuwa imezipokea dhambi za waisraeli wote. Koo lake lilikatwa, na kisha ikamwaga damu yote mara moja. Kisha makuhani waliichuna, wakaikata katika vipande, na wakatoa nyama yake kwa Mungu kwa kuichoma kwa moto.
Masihi ambaye ni kiini halisi cha sadaka ya kuteketezwa ya Agano la Kale, alikuja hapa duniani, akazipokea dhambi zetu kwa kuwekewa mikono, na kuimwaga damu yake Msalabani, na akafa badala yetu. Kwa hiyo, leo hii, mimi na wewe tumepokea kikamilifu ondoleo la dhambi zetu kwa kupitia ubatizo wa Yesu Kristo na kifo chake Msalabani. Na ni lazima tuoshelee mbali dhambi zetu halisi tunazozitenda katika maisha ya kila siku kwa kuamini kuwa dhambi hizi zimekwisha safishwa kwa ubatizo ambao Bwana wetu aliupokea na damu ambayo aliimwaga Msalabani. Ni lazima tuufahamu ukweli huu na kisha tuuamini. Tunaweza kukombolewa toka katika dhambi zetu zote halisi kwa kuamini kuwa Yesu alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake na akazioshelea mbali kwa kupitia ubatizo wake. Kwa maneno mengine, kila tunapotenda dhambi halisi, ni lazima tuithibitishe imani yetu katika injili ya maji na Roho. Na kwa kuutafakari ukweli kuwa hata hizi dhambi halisi zilikwisha toweshwa mbali na Yesu kwa ubatizo wake na Msalaba, hatuwezi kuupoteza wokovu wetu kwa namna yoyote, na tunaweza kuurudisha mara inapotokea kuwa mioyo yetu imevamiwa na dhamiri mbaya.
Kwa sababu Yesu ametoweshea mbali hata zile dhambi halisi za kila siku zinazotendwa na wenye haki ambao wamepokea ondoleo la dhambi katika maisha yao ya kila siku, Mungu ameliruhusu birika la kunawia kwa ajili yao ili kwamba hawa wenye haki, ambao ondoleo lao la dhambi lilikuja kwa maji, na damu, na Roho, waweze kuoshwa dhambi zao halisi kwa kupitia imani katika injili ya maji na Roho.
Hii ndiyo sababu Mungu alilifanya birika la kunawia kwa kukusanya na kuyeyusha vioo vya mkononi vilivyotumika na wanawake waliokuwa wakihudumu katika Hema Takatifu la Kukutania, kwa kuwa vioo hivi vilikuwa vinatoa mtazamo wa mtu au kitu binafsi. Kila tunapofanya dhambi halisi na kuanguka katika kukata tamaa kwa sababu ya madhaifu yetu, ni lazima twende katika birika la kunawia na kuiosha mikono na miguu yetu. Jukumu la birika la kunawia ni kutukumbusha sisi kwamba Yesu alizichukua dhambi za mwanadamu katika mwili wake mara moja na kwa wote pale alipobatizwa na Yohana. Ilikuwa ni kuwafundisha ukweli huu kwa wenye haki ambao wamepokea ondoleo la dhambi, kwamba Bwana wetu aliwafanya waisraeli kulitengeneza birika la kunawia kwa kuyeyusha vioo vya mkononi vya wanawake hawa, na kisha kulijaza kwa maji, na kisha akawaruhusu makuhani kujisafisha uchafu wote wa mikono yao na miguu kwa maji haya.
Tunaamini kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu, Muumbaji, na Mwokozi wa wanadamu. Na ni lazima tukumbuke kuwa Masihi alikuja hapa duniani katika mwili wa mwanadamu na akazipokea dhambi zetu zote zilizopitishwa katika mwili wake kwa kupitia ubatizo alioupokea toka kwa Yohana—hii ni kusema kwamba, kila tunapofanya dhambi halisi katika ulimwengu huu, tunapoanguka katika udhaifu au udhaifu wetu unapofunuliwa, ni lazima tukumbuke kuwa Masihi alikuja katika mwili, alibatizwa na kusulubiwa, na kwa hiyo amekwisha zitowesha dhambi zetu zote.
Ikiwa hatulikumbuki hili na kuliamini, ingawa tumepokea ondoleo la dhambi, basi tutakuja kufungwa tena na dhambi zetu halisi na kisha tutarudi katika nafsi zetu za zamani za uovu. Kwa hiyo, ni lazima tuamini kila siku kwamba dhambi zetu zote zilizofanywa kwa sababu ya udhaifu wetu na mapungufu yetu vimekwishapitishwa kwa Yesu kwa kupitia ubatizo wake. Kila siku, ni lazima tukumbuke, tuamini tena, na kuthibitisha kuwa Masihi alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake kwa ubatizo alioupokea toka kwa Yohana na amezisafisha dhambi hizo zote.
Hakuna hata mmoja katika uso wa dunia hii anayeweza kupokea ondoleo la dhambi kwa kumwamini Yesu pasipo kuamini kuwa alibeba dhambi za ulimwengu kwa kubatizwa na Yohana na akaimwaga damu yake. Na hata kama watu wamepokea ondoleo la dhambi, hakuna hata mtu mmoja ambaye hatendi dhambi halisi. Kwa hiyo, pasipo kuuamini ubatizo wa Yesu, kila mmoja atakuwa ni mwenye dhambi, na mapenzi ya Mungu hayatakuwa yametimizwa kwa mtu yeyote. Hii ndiyo sababu Mungu alitupatia Mwana wake, akamfanya abatizwe na Yohana, na akamtoa ili kumwaga damu Msalabani.
Ikiwa tunamwamini Yesu Kristo kuwa ni Masihi wetu, ni lazima tuamini kuwa dhambi zetu zote zilipitishwa kwa Yesu kwa kupitia ubatizo wake alioupokea toka kwa Yohana, na kwamba alibeba adhabu yetu yote kwa kuzibeba dhambi za ulimwengu Msalabani, akasulubiwa, na akaimwaga damu yake. Tunapokea ondoleo letu la dhambi kwa kuamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake. Dhambi zetu zote zimetoweshwa mbali kwa kuuamini ukweli huu. Tumeifikia haki kwa kuamini katika upendo wa Mungu kwa mioyo yetu yote. Kwa sasa mioyo yetu haina dhambi, ni misafi na isiyo na madoa. Lakini bado kuna mapungufu mengi katika mwili wetu. Hii ndio sababu tunapaswa kuukumbuka ubatizo wa Yesu kila siku na kujikumbusha sisi wenyewe juu ya imani hii kila wakati. Kila inapotokea kuwa mapungufu yetu na udhaifu wetu umefunuliwa, inapotokea kuwa mawazo mabaya yanainuka na tunachafuliwa, na kila wakati matendo yetu yanapokwenda kinyume, Bwana wetu anapendezewa pale tu tunapokumbuka kuwa Yesu alizichukua dhambi hizi zote katika mwili wake kwa ubatizo alioupokea toka kwa Yohana na anaisafisha mioyo yetu kwa kuuamini ukweli huu mara nyingine tena.
Kila tunapofanya dhambi, ni lazima kwanza tuzikiri dhambi zetu mbele za Mungu. Kisha ni lazima tuamini tena kuwa dhambi hizi zote zilikwisha pelekwa kwa Yesu kwa kupitia ubatizo wake. Sisi ambao tumesafishwa kwa kazi ya ubatizo wa Yesu ni lazima tuzisafishe dhambi halisi kila siku kwa kuiamini kazi hii. Hii ndio sababu ni lazima tukumbuke na kuamini katika ukweli kwamba tunaweza kuosha dhambi zetu zote kwa kupitia ubatizo wa Yesu Kristo.
Sasa tumekwisha chunguza kuwa ni kwa nini Mungu aliliweka birika la kunawia kati ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na Hema Takatifu la Kukutania. Mungu aliliweka birika la kunawia kati ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na Hema Takatifu la Kukutania ili kwamba tunapokwenda mbele yake, twende tukiwa na miili na mioyo safi. Hata baada ya kufanyika wenye haki ambao tumepokea ondoleo la dhambi kamilifu kwa kupitia ubatizo wa Yesu Msalabani, mioyo yetu bado inaanguka na kuchafuliwa kila tunapofanya dhambi kwa kupenda au kwa kutopenda. Hii ndio sababu ni lazima tuusafishie mbali uchafu huu katika birika la kunawia tunapoipita madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na kwenda mbele za Mungu. Kwa sababu hatuwezi kwenda mbele za Mungu ikiwa tunayo hata chembe ndogo ya uchafu, Mungu aliweka birika la kunawia kati ya madhabahu ya sadaka ya kuteketezwa na Hema Takatifu la Kukutania ili tuweze kuingia katika uwepo wa Mungu kwa usafi baada ya kujiosha sisi wenyewe kwa maji ya birika la kunawia.
 
 
Je, Ni Aina Ipi ya Dhamiri Ambayo Ni Dhamiri Nzuri Mbele za Mungu?
 
1 Petro 3:21 pia inauelezea ubatizo wa Yesu kuwa ni “jibu la dhamiri safi mbele za Mungu.” Hapa, ‘dhamiri safi’ ni ile inayoamini kuwa Yesu alizioshelea mbali dhambi zote za wanadamu, zikiwemo dhambi halisi zinazotendwa kila siku, kwa ubatizo alioupokea toka kwa Yohana katika Mto Yordani. Ili kuzichukua dhambi katika mwili wake, Bwana wetu alibatizwa na Yohana na kwa hiyo alizipokea dhambi zetu katika mwili wake. Kwa sababu Yesu alibeba dhambi zetu zote katika mwili wake, ilimpasa kufa Msalabani. Ikiwa tutadharau na kutoamini kile ambacho alikifanya, basi dhamiri zetu zitabaki kuwa na uovu. Hii ndiyo sababu kuwa ni lazima tuamini katika ubatizo wake. Ni lazima tuwe na dhamiri safi mbele za Mungu. Ingawa katika mwili wetu tunaweza tusiishi vizuri kikamilifu kwa asilimia 100, lakini walau katika dhamiri zetu, tunaweza na ni lazima tuwe na dhamiri nzuri mbele ya macho ya Mungu.
Takribani nusu karne iliyopita, wakati Korea ilipopoteza kila kitu katika vita, mafuriko ya misaada ya nje yalikuja katika nchi ili kuikomboa toka katika tatizo lake. Ingawa yatima walipaswa kupokea misaada hiyo kwanza, badala ya kuwa hivyo, baadhi ya watu wabadhirifu waliiweka misaada hiyo katika mifuko yao na wakaujenga utajiri wao binafsi. Hawakuwa na dhamiri yoyote. Wakati nchi za kigeni zilipotoa maziwa ya unga, unga, mablakenti, viatu, nguo, na misaada mingine, hao waliotoa walitoa ili watu walio uchi na wasio na chakula waweze kuvishwa na kulishwa vizuri; hawakuweza kufikiria kuwa baadhi ya maofisa waovu na waongo watakwepesha bidhaa hizi za msaada.
Watu wenye dhamiri safi wangeigawanya misaada hiyo kwa haki miongoni mwa watu maskini. Wale ambao, badala ya kugeuza misaada ya nje kuwa ni fursa yao ya kuujenga utajiri wao, waliigawa misaada hiyo vizuri miongoni mwa maskini waliokuwa wanakufa kwa njaa wasingekuwa na kitu cha kuona aibu mbele za Mungu, kwa kuwa walikuwa wameishi kwa dhamiri nzuri. Lakini wale ambao hawakufanya hivyo wangekuwa wametuhumiwa kuwa ni wezi kwa dhamiri zao wenyewe. Kwa kweli, wezi hawa bado wangeweza kuoshwa dhambi zao zote ikiwa wangegeuka na kuuamini ubatizo wa Yesu hata sasa.
Ili kuzichukua dhambi zetu katika mwili wake na ili kuzitoweshea mbali dhambi zetu halisi, Yesu alikuja hapa duniani na alibatizwa. Baada ya kuwa amebatizwa hivyo na Yohana, Yesu aliziosha dhambi zetu zote mara moja. Ninapenda kuwakemea wasioamini katika ubatizo wake, kwa kusema, “Ni kitu gani basi, kinachokufanya wewe kuwa na majivuno kiasi cha kutokuamini katika ubatizo wa Yesu? Ni kwa ujasiri gani hata huwezi kuamini? Je, wewe ni mwema vya kutosha kuweza kuingia katika Ufalme pasipo imani katika ubatizo wake?”
Ikiwa kweli tunataka kuwa watu wa dhamiri nzuri, ni lazima tuzioshe dhambi zetu halisi kwa ubatizo ambao Yesu aliupokea toka kwa Yohana. Ili kufanya hivyo, ni lazima tuamini katika mioyo yetu kwamba Yesu alizichukua dhambi zetu zote tunazozifanya katika kipindi chetu cha maisha katika mwili wake ana amezioshelea mbali. Hii ndio sababu Yesu Masihi wetu alibatizwa na Yohana kabla ya kwenda Msalabani.
Yesu alimwambia mwanamke aliyekuwa amekamatwa katika uzinzi, “Hata mimi sikuadhibu. Wala pia sikuhukumu.” Kwa nini? Kwa sababu Yesu amekwishaichukua dhambi ya mwanamke huyu ya uzinzi katika mwili wake, na kwa sababu Yesu mwenyewe atabeba adhabu ya dhambi hii pia. Alisema, “Mimi ndiye ambaye nitaadhibiwa kwa dhambi zako. Lakini uoshwe dhambi zako zote kwa kuamini katika ubatizo wangu. Kwa hiyo, okolewa toka katika dhambi zako zote kwa kuniamini mimi. Okolewa toka katika adhabu yote ya dhambi kwa imani, na uoshwe dhambi zako zote. Usafishwe dhambi za dhamiri zako na unywe maji toka kwangu ambayo yatakufanya usione kiu tena.”
Leo hii, wewe na mimi tunaamini kwamba Yesu ndiye aliyetuokoa toka katika dhambi zetu. Je, unaamini kweli kwamba Yesu alizichukua dhambi zetu katika mwili wake kwa ubatizo wake na kwamba alizioshelea mbali? Bwana wetu alizisafisha dhambi zetu kwa kubatizwa. Sasa tunaweza kwenda mbele za Mungu katika dhamiri safi. Kwa nini? Kwa sababu Bwana wetu alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake na akazioshelea mbali kwa kubatizwa, akazibeba dhambi hizi Msalabani, akaadhibiwa kwa niaba yetu kwa kusulubiwa, na kisha akafufuka tena toka kwa wafu. Hapo zamani, Yesu alikuja hapa duniani, na alipokuwa na miaka 33 alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake na akaziosha dhambi hizo kwa ubatizo wake.
Kwa kuzichukua hata dhambi zetu halisi katika mwili wake na kuziosha, Bwana wetu ametuwezesha kwenda kwa Mungu na kufanyika wenye haki, na kuhukumiwa kwa dhambi zetu zote kwa kupitia sadaka ya kuteketezwa ya Yesu Kristo. Kwa maneno mengine, ni kwa kumwamini huyu Bwana, ndipo tunapoweza kumuita Mungu kuwa Baba yetu na kwenda mbele ya uwepo wake. Kwa hiyo, wale wanaoamini katika kazi za Yesu za maji, damu, na Roho Mtakatifu ndio wale ambao wenye dhamiri nzuri. Kwa upande mwingine, ni hakika kuwa ni dhamiri mbaya ndiyo ambayo haiamini katika matendo ya Bwana ya haki ambayo ni ubatizo na kusulubiwa kwake.
 
 
Siku Hizi Watu Wengi Hawalichukulii Neno la Mungu kwa Umakini Kwa Sababu ya Imani Zao za Kishirikina
 
Waongo wengi, wanalidharau Neno la Mungu kana kwamba ni kama pambo fulani, wanahubiri tu kuwa ni lazima tufanye matendo mema katika imani yetu kwa Mungu ili tuweze kuingia katika Ufalme wa Mbinguni. Na inapofika katika suala la wokovu, wanazungumzia tu suala la damu ya Msalaba, na kwa makosa wanafikiri kuwa wanatakiwa kupanda mlimani ili wakafunge na kuomba ili waweze kuonana na Mungu kwa kupitia uzoefu wao wa mwili. Ingawa kwa kweli imani hii ni potofu, watu hawa wanauhakika sana na imani hii. Wanasema, “mimi nilisumbuliwa sana na dhambi zangu, na kwa hiyo nilikaa usiku mzima nikiomba, ‘Mungu, nimefanya dhambi. Ninakuamini, Bwana.’ Siku hiyo, bado nilisumbuliwa wakati wa jioni, lakini baada ya kukaa usiku mzima nikiomba, wakati kulipopambazuka, ghafla nikahisi kana kwamba bunda la moto limetupwa kwangu, na mara ile mawazo yangu yote yalisafishwa―dhambi zote za moyo wangu zilisafishwa mbali na kuwa nyeupe kama theluji. Kwa hiyo, ilikuwa ni wakati huu ndipo nilipozaliwa upya. Halleluya!”
Mawazo ya jinsi hiyo ni yale yaliyoundwa na wanadamu tu, ni mawazo ya kijinga na ya kipuuzi yanayoligeuza Neno la Mungu kuwa halina maana. Ni lazima ukumbuke kuwa Mungu atawaadhibu wale wanaosema mambo ya jinsi hiyo ya kimafumbo na yasiyo na maana na ambayo yanawapotosha watu na kuwapeleka wengine katika moto wa kuzimu.
“Masiko yangu yanauma sana. Lakini niliamini katika kile ambacho Bwana wetu alikisema, kwamba tutaponywa ikiwa tutaamini, na kwa hiyo niliweza kuyavumilia maumivu yangu kwa kusema, ‘Bwana, Ninaamini!’ Basi nilipoamini hivi maumivu yangu yote yalitoweka!”
“Nilikuwa na vidonda vya tumbo, hivyo kila wakati nilipokula kitu fulani, nilipata maumivu makali ya tumbo. Hivyo kabla ya kula, niliomba, ‘Bwana, ninaumia hapa, lakini ulisema kuwa utasikia chochote tutakachokiomba kwa imani. Bado ninaliamini Neno lako.’ Kwa hakika, sikupata tatizo la myeyusho wa chakula!”
Je, haya yote ni mambo gani? Haya ni mazingira ambapo watu hawakutani na Mungu kwa kupitia Neno. Mazingira haya yanaonyesha anguko la imani yao ambayo haiamini kwa Neno. Haya sio majibu kwa maombi yao yaliyopatikana kwa kupitia Neno, bali ni imani yao ya kimafumbo na kishirikina. Wanamwamini Mungu si kwa Neno, bali katika mchanganyiko wao wa kimakosa uliojengwa katika hisia zao binafsi na uzoefu. Kinachojutisha na kusikitisha zaidi ni kuwa kuna mafumbo mengi ya jinsi hiyo miongoni mwa Wakristo wa leo.
Vivyo hivyo, kulisukumia pembeni Neno la Mungu na kumwamini Yesu kwa upofu kwa kutegemea hisia zao au uzoefu wao ni sawa na imani ya kishirikina. Watu wanaodai kumwamini Yesu hata pale ambapo hawaamini kwa Neno wanahitaji kujichunguza wao wenyewe ili kuona ikiwa wamepagawa na mapepo au la. “Nilikutana na Yesu nilipokuwa ninaomba. Yesu alinitokea katika ndoto. Niliomba kwa juhudi na ugonjwa wangu ukaponywa.” Mtu yeyote mwenye mdomo ulio nusu anaweza kudai hivyo, lakini jambo la wazi ni kuwa hii si imani ambayo ilitolewa na Mungu, bali ni imani potofu iliyotolewa na Shetani.
Kwa kupitia nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa, Bwana wetu amejifunua yeye mwenyewe kwetu sisi. Je, Bwana wetu anajifunua mwenyewe kwetu katika njia mpya na tofauti katika zama za leo? Je, ni kweli kuwa Mungu anatutokea katika ndoto au njozi? Hali akiwa anauburuza mnyororo mkubwa katika miguu yake, akitokwa na damu mwili mzima, akiwa na taji la miba katika kichwa chake, na anasema, “Unaona, hivi ndivyo nilivyoteseka sana kwa ajili yako. Sasa, utafanya nini kwa ajili yangu?”—je, hivi ndivyo Bwana wetu anavyojifunua kwetu? Kwa kweli huu ni upuuzi mtupu!
Hata hivyo bado kuna watu ambao baada ya kupata ndoto ya jinsi hii, wanaweka kiapo mbele za Mungu, “Bwana, nitakuwa mtumishi wako kwa moyo wangu wote kwa maisha yangu yote yaliyosalia. Nitajenga nyumba ya maombi hapa. Nitalijenga kanisa hapa. Nitaubeba msalaba katika muda wangu wa maisha uliosalia na nitakushuhudia wewe katika taifa zima na katika ulimwengu mzima.”
Kwa kweli, tunaweza kwa urahisi kukutana na wahuburi waliojitoa kama hao katika mitaa na katika maeneo ya halaiki. Bila shaka, watu hao ni wale washirikina wenye mafumbo ambao wanasema kuwa waliamua kuishi hivyo baada ya kumwona Yesu katika ndoto zao au baada ya kuisikia sauti ya Bwana walipokuwa wakiomba. Lakini Bwana anajifunua yeye mwenyewe kwa kupitia Neno lake tu; hazungumzi nasi katika njozi au pale tunapoomba, na hasa katika kipindi hiki ambapo Neno lake lote limetolewa kwa wanadamu kikamilifu. Ndoto zinatokana na mchanganyiko wa maisha ya kila siku na toka katika nusu ya ufahamu tuwapo usingizini. Watu hawa wana aina hii ya ndoto kwa sababu wana kila aina ya mawazo na fikra kuhusu Yesu katika upendo wao usio na majibu na kwa sababu wanafikiria kupitia kiasi.
Wakati mawazo yako yanapolifanyia kazi sana jambo fulani kabla ya kwenda kulala, inawezekana sana kujikuta wewe mwenyewe ukijihusisha na jambo hilo pia katika ndoto. Vivyo hivyo, ndoto zinatokana na nusu ufahamu. Hii ndio sababu ikiwa tunafikiria sana, tunapata aina zote za ndoto za ajabu na zisizo za kawaida. Ndoto hizo zote hazina lolote la kufanya kuhusina na imani, bali ni mwangwi wa mabadiliko ya kimwili au nusu ufahamu.
Hii ndio sababu ikiwa watu wanafikiria sana kuhusu kifo cha Yesu Msalabani, katika ndoto zao anaonekana akiwa na taji la miiba katika kichwa chake. Hakuna kitu kibaya katika ndoto za jinsi hiyo. Lakini kuichukulia ndogo hii kwa umakini ni kosa la mauti. Itakuwaje ikiwa Yesu atawatokea akitokwa na damu mwili mzima, na kisha akasema kikweli kweli, “Utafanya nini kwa ajili yangu? Utaishi maisha yako yote yaliyosalia kwa kujinyima raha za mwili. Kwa ajili yangu mimi, hutakuwa na mali yoyote”? Kuna watu wajinga ambapo kwa kweli wanaziacha mali zao zote ili waweze kuishi kama hivyo. Je, kuna mtu yeyote ambaye aliwahi kusitushwa kwa sababu ya ndoto, ambaye aliichukulia ndoto hiyo kwa makini, au ambaye maisha yake yalibadilishwa kwa sababu ya ndoto hiyo? Mambo ya jinsi hiyo ni mafumbo ya kishirikina.
Mungu anakutana nasi kwa kupitia Neno. Si kama mtu ambaye tunaweza kukutana naye katika ndoto au maono katika maombi yetu. Neno la Mungu limeandikwa katika Agano la Kale na Agano Jipya, na ni pale tunapolisikia Neno hili likihubiriwa kwetu na kisha tukalipokea katika mioyo yetu ndipo roho zetu zinapoweza kukutana na Mungu kwa kupitia Neno lake. Kwa maneno mengine, ni kwa kupitia Neno tu ndio roho zenu zinapoweza kukutana na Mungu.
Ni kutoka katika Neno ambalo tumekuja kulifahamu kwamba Yesu alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake kwa ubatizo wake; ni kwa kulisikia Neno hilo ndipo tumekuja kuamini katika mioyo yetu. Jibu la swali kuwa ni kwanini ilimpasa Yesu Kufa Msalabani pia linapatikana katika Neno. Ni kwa sababu Yesu alizichukua dhambi zake katika mwili wake kwa kubatizwa na kwamba alikufa Msalabani na ametuokoa sisi. Kwa Neno la Mungu tunamfahamu Mungu, na kwa Neno ndipo tunakuja kumwamini. Pia tunaamini kwamba Yesu Kristo kuwa ni Mungu kwa kupitia Neno.
 
 
Ikiwa Lisingekuwa Neno la Mungu Lililoandikwa, Tungewezaje Sisi Kumwamini Mungu?
 
Ikiwa kusingekuwa na Neno la Mungu, tungewezaje sisi kukutana na na kumwamini Yesu ambaye alizifanya dhambi zetu zote kutoweshwa? Ikiwa kusingekuwa na Neno la Mungu, imani yetu ingekuwa ni bure. “Hivi ndivyo ninavyofikiri”—tunaweza kuzungumza nje ya mawazo yetu, lakini huu si ukweli, na pale mioyo yetu inapokuwa imejazwa na yale yasiyo ya kweli, basi ule ukweli halisi hauwezi kuingia katika mioyo yetu. Kitu cha maana cha kukizungumza si kusema, “Hivi ndivyo ninavyofikiri,” bali ni kusema, “Hivi ndivyo Biblia inavyosema.” Tunapoisoma Biblia, ukweli uliozungumzwa na Mungu unakuja katika mioyo yetu na unasahihisha makosa ya mawazo yetu yaliyotangulia.
Imani yako katika injili ya maji na Roho ni ipi? Je, ni ile iliyojengwa kwa mawazo yako binafsi? Au je umefanyika mtu aliyezaliwa upya kwa kuifahamu na kuiamini imani hiyo kwa kulisikia Neno? Ni kwa kupitia Neno ndipo tumeweza kuamini na kukutana na Mungu katika mioyo yetu. Hii ndiyo sababu lango la ua wa Hema Takatifu la Kukutania lilifumwa kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa.
Maji yaliyokuwemo katika birika la kunawia yanamaanisha ubatizo wa Yesu ambao kwa huyo Yesu Kristo alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake. “Kubali hivi sasa; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote.” (Mathayo 3:15). Kwa kupitia Neno la Mungu, tulikuja kuufahamu ubatizo ambao kwa huo Yesu alizichukua dhambi za ulimwengu katika mwili wake. Kwa sababu ni kutoka katika Neno ndipo tumekuja kuufahamu ubatizo wa Yesu ambaye alizichukua dhambi zote ambazo wewe na mimi tunazifanya katika kipindi chote cha maisha yetu, Neno hili limetufanya sisi kuwa na imani ya ubatizo katika mioyo yetu. Ni kwa kupitia Neno ndipo tunapokuja kuupata ukweli uliodhihirishwa katika birika la kunawia.
Toka katika Neno la Mungu, tunaweza kuona kuwa birika la kunawia liliundwa kwa shaba. Katika Biblia, shaba inamaanisha hukumu. Kwa hiyo, maana ya birika la kunawia la shaba ni kuwa tunapojiangalia sisi wenyewe mbele ya Sheria, ambayo inatekeleza jukumu la kioo kinachotuonyesha sisi wenyewe, tunatambua kuwa sisi sote tunapaswa kuadhibiwa. Hii ndio sababu birika la kunawia liliundwa kwa vioo vya wanawake waliokuwa wakihudumu katika Hema Takatifu la Kukutania. Mungu ametuokoa sisi, ambao tusingeweza kukwepa bali kuadhibiwa kwa sababu ya dhambi zetu, ametuokoa kwa kuja hapa duniani, kwa kubatizwa, na kwa kufa Msalabani. Kwa kupitia Neno la Mungu lililoandikwa, tulikuja kufahamu kuwa ni kwa sababu Yesu alibatizwa ndio maana alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake, akauendea Msalaba, na akabeba adhabu ya dhambi. Na ni kwa kukubali katika mioyo yetu na kuuamini ukweli huu ndipo tumeweza kuokolewa. Vipi kuhusu wewe? Je, umeokolewa vipi?
Katika dhehebu fulani ambalo linafuata imani ya mafumbo ya kishirikina, wanadai kuwa wanachama wake ni lazima wafahamu tarehe maalum ya wokovu wao, kuwa ni tarehe ipi na mwezi upi walipookolewa. Na mchungaji katika dhehebu hili inasemekana aliwahi kushuhudia mbele ya waamini wengi kwamba alimwamini Yesu na kuokolewa pale alipopanda mlimani fulani kuomba na kisha akajitambua kuwa yeye si kitu. Alidai kwa majivuno kabisa kuwa hajawahi kusahau tarehe kamili na muda alipozaliwa kwa upya. Kwa hakika, jambo hili halihusiani chochote na kitani safi ya kusokotwa, bali ni kitu cha kihisia tu. Imani ya mchungaji huyu haijihusishi kwa lolote na nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Wokovu unaofundishwa na dhehebu hili hauna jambo lolote la kufanya kuhusiana na wokovu wa kweli ulioundwa na Neno la Mungu, bali ni ule waliojiundia wao wenyewe.
Kwa kweli inawezekana kumpumbaza mtu fulani. Ikiwa watu wanaendelea kusisitiza kuwa wao hawana dhambi, na kisha wakaendelea kufikiria hivyo mara kwa mara, basi wanaishia kupumbazwa na kuwa wasio na dhambi kwa mujibu wao wenyewe. Ikiwa wanaendelea kujiimbia manuizo haya wao wenyewe, basi wanaweza kujihisi kuwa kweli hawana dhambi, lakini mawazo ya jinsi hiyo hayawezi kudumu kwa muda mrefu. Kwa hiyo, baada ya muda mfupi watajipumbaza wenyewe tena, hali wakiimba, “Mimi’sina dhambi. Mimi’sina dhambi.” Imani hii ni ya ubinafsi sana, isiyo ya kweli, ya kijinga na ya kishirikina!
Kitani safi ya kusokotwa inamaanisha Neno la Mungu la Agano la Kale na Agano Jipya. Kwamba malango ya ua wa Hema Takatifu la Kukutania, ya Mahali Patakatifu, na Patakatifu pa Patakatifu yalifumwa kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa kunatueleza sisi kuwa Yesu alifanyika mlango wa wokovu wetu na Mwokozi wetu kamili kama ilivyoandikwa katika Agano la Kale na Agano Jipya. Kwa hiyo, kwa kweli ninamshukuru Mungu kwa jinsi ambavyo wokovu huu ni wa uhakika ambao Mungu ametuambia!
Hii ndio sababu wakati ninaomba, ninajitahidi nisitumie hisia na misukumo au kujionyesha. Ninaomba hali nikiacha vitu vyote kwa Mungu na kumwamini yeye. “Baba, tafadhali tusaidie sisi. Tusaidie ili tuihubiri injili katika ulimwengu mzima. Walinde na kuwatunza watumishi wenzangu wote na watakatifu. Tupatie watenda kazi ambao wataihudumia injili, iruhusu injili hii kuenea, na wafanye waamini waweze kutambua na kuliamini Neno lako.” Hivi ndivyo ninavyosema pale ninapoomba; Siombi hali nikijaribu kuziamsha hisia zangu na kulia, na aina yoyote ya marogonyo ya aina hii si sehemu ya maombi yangu.
Baadhi ya watu wanaposhindwa kuziamsha hisia na mihemko yao baada ya kujaribu sana, basi wanaanza kuwafikiria baba zao na mama zao waliofariki zamani ili kuvujisha machozi na kuyafanya maombi yao yachukuliwe kwa umakini na watu wengine. Maombi ya jinsi hivyo yalifanyizwa ni kama lundo la uchafu ambao utamfanya Mungu atapike. Pia watu wanaziamsha hisia zao kwa kufikiria juu ya kusulubiwa kwa Yesu na wanaendelea kupiga kelele kwa upofu, “Ninakuamini wewe Bwana!”
Je, ni kweli kuwa hii inamaanisha kuwa imani ya watu wa jinsi hiyo ni yenye nguvu? Ikiwa unafikiria kuhusu dhambi zako na unajaribu kuziamsha hisia zako, hali ukisema, “Bwana, nimetenda dhambi. Nisaidie ili niishi kwa haki,” basi inawezekana sana wewe mwenyewe ukajiamsha kihisia. Kwa sababu kuwa na uzoefu wa kihisia wa aina hiyo na kipindi kizuri cha kulia kunaweza kutoa na kupunguza mfadhaiko mkubwa, watu wengi baada ya kulia kihisia wanajisikia kuwa wameburudishwa, ndipo wanafikiria kuwa hivi ndivyo imani ilivyo. Ingawa maisha yao yamejawa na matatizo mengi, uzoefu wa aina hiyo wa kihisia unawafanya angalau wajisikie vizuri kwa kitambo, na kwa hiyo wanayaendeleza maisha yao ya kidini kwa namna hii.
 
 

Ni Lazima Uamini Kuwa Bwana Amekuja Kwetu Kwa Kupitia Nyuzi za Bluu, Zambarau, na Nyekundu na Kitani Safi ya Kusokotwa

 
Bwana wetu alikuja kwetu kwa kupitia Neno. Hivyo usisubiri hisia na fikra zako, bali ni lazima usikie kile ambacho Neno la Mungu linakuambia. Jambo la muhimu ni kuwa unaamini au hauamini Neno la Mungu katika moyo wako. Unapoomba, usijaribu kulowea na kuzama ndani katika hisia zako. Bali, ni lazima uzitawale hisia zako katika kiwango safi cha kawaida. Kwa nini? Kwa sababu kuna waongo wengi katika ulimwengu huu ambao wanawakaribia wale ambao wanapenda kuamshwa na kupambishwa kihisia ili kujipatia faida kutokana na mianya yao ya kihisia. Wakati mikutano ya uamsho inapofanyika chini ya bendera ya “Uamsho Mkuu wa Kiroho,” mara nyingi watu wanapoteza sehemu ya uwezo wao wa kiakili kwa kuikimbilia misukumo yao ya kihisia, kwa kweli mara nyingi lengo si kuamsha tu hisia za washiriki.
Hata hivyo, kwa kuwa sasa nimezaliwa upya, siwezi kushikilia uamsho wa jinsi hiyo hata kama ningetaka kujaribu, kwa kuwa kuhubiri Neno la Mungu si kuziamsha hisia za watu kama ambavyo mikutano hii mikuu ya uamsho ya kidunia inavyofanya. Kwa sababu nimezaliwa upya kwa Neno la kweli, nimezipa kwaheri hisia zangu ambazo zilikuwa zikiingilia maisha yangu ya kiroho.
Sisi wenye haki ambao tunalisikia Neno la Mungu, tunatumia akili zetu na ufahamu, na tunaamini katika mioyo yetu, na hatupendi kamwe kuamshwa na kupambishwa kihisia. Tunaamini katika kweli kwa kutambua mara moja ikiwa mtu anatuongelea Neno la Mungu kama lilivyo, na pia tunatambua mara moja ikiwa mtu anayetuambia hivi analiamini hilo Neno au la. Kwa sababu sisi ambao tunafahamu na kuamini katika ukweli wa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa tunaye Roho Mtakatifu katika mioyo yetu, sisi sote tunatambua kuwa mpambisho wa kihisia uko mbali kabisa na ukweli, na sisi tunaupokea ukweli halisi tu katika mioyo yetu.
Yesu alikuja kwetu kwa kupitia nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Ni jinsi gani ukweli huu jinsi ulivyo wa kushangaza? Ni jinsi gani upendo wa Bwana wetu uliotuokoa ulivyo wa kushangaza? Kwa kupitia kazi nne za Yesu zilizoandikwa katika Neno la Mungu, sisi sote tumekuja kuamini kwamba Yesu alizichukua dhambi zako zote katika mwili wake kwa ubatizo wake, alikufa Msalabani, na kwa hiyo amekuokoa kwa kule kuitimiza haki yote.
Je, unaamini katika ukweli huu katika moyo wako? Wale wanaoihubiri injili ni lazima waieneza kwa kupitia ndani ya kitani safi ya kusokotwa, ambayo ni Neno la Mungu la Agano la Kale na Agano Jipya, na katika yaliyomo ni lazima kuwe na nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu. Na wale wanaoisikia injili hiyo ni lazima waipokee katika mioyo yao na kisha waiamini kwa mioyo yao yote.
 
 

Maji ya Birika la Kunawia Yanazioshelea Mbali Dhambi Zetu

 
Kwa kupitia ubatizo wake, Yesu alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake na akazioshelea mbali. Ubatizo wa Yesu unamaanisha maji ya birika la kunawia; umetusafisha sisi ambao tulikuwa tumefungwa kuzimu kwa sababu ya dhambi, na umetuwezesha kusimama mbele za Mungu. Kwa sababu Yesu alizipokea dhambi zetu katika mwili wake kwa kupitia ubatizo wake, basi aliweza kwenda Msalabani na kuzioshelea mbali kwa kusulubiwa hadi kifo. Ubatizo wa Yesu na Msalaba vinashuhudia kuwa Yesu alibeba adhabu ya dhambi zetu zote. Kwa kupitia ubatizo na Msalaba, Yesu aliutimiza wokovu wetu wote.
Kutoa sala za toba hakuwezi kamwe kuzisafisha dhambi zetu. Ni kwa sababu Yesu alikwishazichukua dhambi zetu katika mwili wake kwa kupitia ubatizo wake ndio maana dhambi zetu zote zimeoshelewa mbali. Ni kwa kulisikia Neno hili na kuliamini katika yale ambayo Yesu ameyafanya kwa ajili yetu ndipo tunapoweza kuwekwa huru toka katika adhabu ya dhambi zetu zote. Shukrani kwa ajili ya adhabu ambazo Yesu alizibeba, sisi tumekwishaibeba adhabu yetu yote ya dhambi kwa kupitia imani yetu katika ubatizo wa Yesu. Kwa kweli, tumeokolewa kwa imani. Kwa hakika, wokovu ni kitu rahisi. Ikiwa tutaamini katika zawadi na upendo wa wokovu, tunaweza kuokolewa, lakini ikiwa hatuamini, basi hatuwezi kuokolewa.
 
 
Hakuna Tunachoweza Kukifanya Ili Tuokolewe Zaidi ya Wokovu Uliotimizwa na Mungu
 
Kama isingekuwa ni Mungu, tusingeweza kufanya kitu chochote kwa ajili ya wokovu wetu. Kwa kuwa Bwana wetu aliamua kutuokoa kwa njia hii hata kabla ya uumbaji na akautimiza wokovu wetu, hivyo basi vitu vyote vinategemea jinsi ambavyo Mungu anaamua. Mungu Baba aliamua kutuokoa sisi kwa kupitia Mwana wake na Roho Mtakatifu, na wakati ulipowadia alimtuma Mwana wake wa pekee Yesu kuja hapa duniani. Wakati Yesu alipofikisha umri wa miaka 30 na muda ulipowadia wa yeye kuzitimiza kazi hizi za wokovu, Baba alimfanya Yesu abatizwe na kufa Msalabani, akamfufua, na kwa hiyo ametuokoa sisi. Tunaokolewa kwa kujifunza na kufahamu yale ambayo Bwana ameyatenda kwa ajili yetu toka katika Neno la Agano la Kale na Agano Jipya, na kuliamini hilo Neno katika mioyo yetu. Kuokolewa kwa kuamini katika mioyo yetu si kitu kingine bali ni kuipokea imani katika mioyo yetu.
Je, unaamini kuwa Neno hili la Biblia ni Neno la Mungu? Hakuna kingine zaidi ya Biblia ambayo ni Mungu mwenyewe ambaye amekuwepo tangu mwanzo na Neno lake. Kwa kupitia Neno la Agano la Kale na Agano Jipya, ambalo ni Neno la Mungu, sasa tunaweza kumfahamu na kukutana na Mungu. Na kwa kupitia Neno la Agano la Kale na Agano Jipya, tunaweza kutambua na kuamini kwamba ametuokoa sisi kwa kupitia nyuzi za bluu, zambarau na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Pia, kwa sababu wale wanaoamini katika ukweli huu wameokolewa, basi wanaweza kushuhudia kuwa Neno hili lina nguvu kwa hakika. Hatupaswi kulihukumu na kulipima Neno la Mungu kwa mawazo yetu finyu, bali ni vema tutambue toka katika Neno hilo jinsi ambavyo Mungu ametuokoa sisi kikamilifu.
Toka katika Agano la Kale na Agano Jipya, ninatumaini na ninaomba kuwa ninyi nyote mtasikia na kuamini katika Neno la nyuzi za bluu (ubatizo wa Yesu), zambarau (Yesu ni Mfalme wa wafalme), na nyekundu (Msalaba), na kitani safi ya kusokotwa (Neno la Mungu la Agano la Kale na Agano Jipya). Ikiwa utaliweka kando Neno la Mungu na ukalihukumu Neno lake kwa vipimo vyako binafsi katika maisha yako yaliyosalia, basi huwezi kamwe kuokolewa.
Ikiwa unatambua wewe mwenyewe kwamba hulifahamu Neno la Mungu vizuri, basi ni lazima usikilize kwa makini kwa yale ambayo watangulizi wako wa imani wanasema. Kwamba ni wachungaji, wafanyakazi, au watu wa kawaida, unapolisikia Neno la Mungu likihubiriwa nao, na kwamba kile wanachokihubiri ni sahihi mbele za Mungu, unachotakiwa kufanya ni kutambua kuwa hilo ni sahihi na kisha uliamini hilo Neno katika moyo wako.
Wale wanaolieneza Neno hawalienezi ati kwa sababu ni rahisi sana, bali wanafanya hivyo kwa sababu kile wanachokieneza ni sahihi mbele za Mungu. Hii ndiyo sababu wanahubiri ufahamu sahihi mbele za Mungu—ambao ni, injili ya maji na Roho, ukweli wa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Bila kujali kuwa tulisikia hilo Neno toka kwa nani, ikiwa ni Neno la kweli la Mungu, basi hakuna tena tunachoweza kukifanya zaidi ya kulikubali kwa kusema ndiyo, kwa kuwa hakuna hata yodi moja au kitu kidogo ambacho kina makosa katika Neno la Mungu.
Ni lazima tuamini katika Neno la Mungu. Kuamini ni nini? Ni kukubali. Ni kutegemea. Kwa maneno mengine, kwa kuwa Bwana wetu alibatizwa kwa ajili yetu, basi tunaukabidhi udhaifu wetu kwake na kisha tunamtegemea. “Je, ni kweli kuwa Bwana ameniokoa kwa kufanya hivi? Ninakutegemea na kukuamini wewe.” Kuamini kwa jinsi hii ni imani ya kweli.
Miongoni mwa wanatheolojia wa ulimwengu huu, ni vigumu sana kumpata yeyote anayefahamu na kuamini kwa usahihi. Hata kabla ya kulifikia birika la kunawia, wanakwama katika lango la ua wa Hema Takatifu la Kukutania wakiwa hawawezi hata kuingia katika ua. Wanapotoa mahubiri yao juu ya Hema Takatifu la Kukutania, wanafanya juhudi ya kina na kwa uangalifu kulizunguka lango la ua kwa makusudi, na wanapochapisha vitabu juu ya Hema Takatifu la Kukutania, wanaweka vielelezo ambavyo vinaliacha kabisa lango kubwa ambalo lilikuwa limechukua takribani mita 9 za uzio wa ua.
Mara chache, wapo baadhi ambao kwa ujasiri wanahubiri kuhusu lango la ua wa Hema Takatifu la Kukutania, lakini kwa sababu hawafahmu kiini cha msingi cha nyuzi za bluu, basi wao wanazungumzia hivi, “rangi ya bluu ni rangi ya anga.” Kwa hiyo wanadai kuwa nyuzi za bluu ni rangi ya anga ambayo inadhihirisha kuwa Yesu ni Mungu mwenyewe, na kwamba nyuzi nyekundu zinamaanisha damu ya Yesu aliyoimwaga Msalabani alipokuwa hapa duniani, na kwa hiyo kwa makusudi kabisa wanauzunguka ukweli wa lango la ua wa Hema Takatifu la Kukutania. Vipi kuhusu rangi ya zambarau? Zambarau inatueleza sisi kuwa Yesu ni Mfalme wa wafalme na Mungu mwenyewe. Uungu wa Yesu umeshikiliwa katika nyuzi za zambarau kikamilifu, kiasi kwamba hakuna sababu ya kurudia kusema mara kwa mara kuhusu ukweli huo kwa nyuzi za rangi nyingine.
Ukweli wa nyuzi za bluu ni kwamba Yesu alikuja hapa duniani na akazichukua dhambi zote za mwanadamu katika mwili wake mara moja na kwa wote kwa kubatizwa na Yohana. Lakini wanatheolojia wa ulimwengu huu, kwa sababu hawautambui ubatizo huu wa Yesu, ndio maana hawawezi kuufahamu wala kuuhubiri, bali watazungumza mambo yao ya kipuuzi. Wale ambao hawajazaliwa upya kwa kutomwamini Yesu aliyekuja kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa hawafahamu kuwa Yesu alizichukua dhambi zote katika mwili wake kwa kupitia ubatizo na kwamba alibeba adhabu zao. Kwa hiyo, wamekuwa ni wapofu kiroho na hawawezi kulitatua Neno, na kwa hiyo wamelipa udini Neno la Mungu kwa kulifafanua ovyo ovyo kwa kutegemea mawazo yao binafsi. Wanafundisha wakisema, “Mwamini Yesu. Ndipo utaokolewa. Na uwe mwema na mnyenyekevu tangu sasa na kuendelea.” Wameigeuza imani katika Yesu Kristo kuwa dini ya kawaida ambayo inasisitiza matendo yao mema.
Kwa sababu watu wanafahamu kuwa hawawezi kuwa wema hata kama wakijiaribu kiasi gani, wanadanganywa kwa urahisi na maneno ya jinsi hiyo ambayo yanainua mapenzi ya mwanadamu kujaribu kuwa mwema. Dini zinafuata mtindo huohuo wa zamani, “Ikiwa utajaribu, basi unaweza kufanya,” au “Jitahidi kadri uwezavyo kuwa mtakatifu.” Mada ya kawaida ambayo inazunguka katika dini zote ni kwamba wanayapima mawazo mazuri, juhudi nzuri, na mapenzi ya mwanadamu kwa kiwango cha juu. Kwa mfano, vipi kuhusu Ubudha? Ubudha unasisitiza juhudi zisizokoma na nia ya mwanadamu na unawafundisha wafuasi wake kujaribu kuwa watakatifu kwa juhudi zao, Ubudha unasema, “Usiue; utafute ukweli na uwe mwema.” Kwa namna fulani, mafundisho yake yanakaribiana sana na yale mafundisho ya Kikristo. Sababu inayofanya Ukristo na Ubudha kuonekana kuwa vinafanana ingawa dini hizo zipo katika maeneo tofauti ni kwa sababu zote ni dini tu.
Dini na imani ni vitu tofauti kabisa. Imani ya kweli ni kutambua na kukubali katika mioyo yetu zawadi ambayo Bwana wetu, ambaye ametuokoa sisi kikamilifu kwa kupitia haki ya Mungu, ametupatia. Imani ni kupokea ondoleo la dhambi kwa kuamini katika mioyo yetu kwamba Bwana alikuja hapa duniani na alibatizwa ili kuzichukua dhambi zetu katika mwili wake, na kwamba alibeba adhabu yetu yote ya dhambi zetu kwa kusulubiwa. Kuamini kwamba Bwana ametukomboa toka katika dhambi zetu zote na adhabu, na kwamba ametuokoa sisi kwa kupitia maji na Roho, basi hiyo ndio imani. Je, unaamini? Ni lazima tuamini kweli katika mioyo yetu.
 
 

Mungu Amekwisha Tuokoa Mimi Na Wewe Toka Katika Dhambi Zetu Zote

 
Kwa hiyo, tunachotakiwa kukifanya ni kuuamini ukweli huu katika mioyo yetu na kuupokea. Hivi ndivyo watoto wa kweli wanyenyekevu wa Mungu wanavyopaswa kufanya mbele za Mungu, na vitu vingine havina umuhimu. Kwa sababu Mungu amekupenda wewe, alimtuma Mwana wake pekee hapa duniani, alimfanya kuzichukua dhambi zako katika mwili wake kwa kubatizwa, alimfanya asulubiwe na kumwaga damu, na akamruhusu kufa kwa kumpa adhabu, akamfufua, na kwa hiyo amekuokoa wewe toka katika dhambi zako zote.
Basi, ikiwa hauamini katika ukweli huu, je, Mungu atajisikiaje? Hata sasa, ikiwa unataka kuwa mtoto wake mnyenyekevu unayeweza kuupendezesha moyo wake, basi ni lazima uamini kuwa Mungu, kwa kupitia Mwana wake, amezitowesha dhambi zako zote na amekuokoa toka katika dhambi hizo. Ikiwa unaamini katika moyo wako na katika shukrani, basi ni lazima ukiri kwa kinywa chako. Je, unapenda pia kumwamini Mungu, lakini inaonekana kuwa ni vigumu sana kwako kuamini katika moyo wako? Basi, jaribu kuikiri imani yako kwa kinywa chako vizuri. Basi ukisha kiri hivyo kwamba unaamini, imani itapandwa na kukua taratibu. Imani ni ya wale ambao wanaipokea na kuichukua kwa ujasiri.
Hebu tufikirie kwa muda kuwa mimi nina pete halisi ya almasi. Hebu pia tufikirie kuwa nitawapatia ninyi pete hiyo, lakini mmoja wenu anakataa kuipokea hali akisema haamini kuwa hiyo pete imetengenezwa kutokana na almasi halisi. Ingawa pete hiyo ni pete halisi ya almasi, kwa sababu mtu huyu hakuamini, kwake yeye pete hiyo halisi inakuwa si almasi, na kwa hiyo anakuwa ameipoteza nafasi ya kuipata pete hiyo ya almasi.
Imani iko kama hivi. Ikiwa mtaalamu wa vito mwenye mamlaka amethibitisha kwa maandishi kuwa pete hiyo imetengenezwa kutokana na almasi halisi, wangeweza kuamini hivyo. Mungu ametueleza kwa kina kwa kupitia Neno lake lililoandikwa kuwa wokovu aliotupatia ni wa kweli. Na wale wanaoamini katika wokovu wake kwa sababu Neno linashuhudia hivyo hao ni watu wa imani. “Ni vigumu kwangu kuamini kuwa hivyo ni kweli, lakini kwa kuwa wewe ambaye ni Mkamilifu unasema kuwa ni kweli, basi mimi ninaamini hivyo.” Hivyo, watu wanapoamini kama hivyo, basi wanaweza kufanyika watu wa imani, na ile zawadi kuu ya thamani itakuwa yao kama ilivyoahidiwa.
Kwa upande mwingine, pia kuna aina nyingine tofauti ya imani. Hebu tufikirie kuwa msanii mbabaishaji ameigilizia pete ya dhahabu, na kwamba mtu fulani ameinunua baada ya kuleweshwa na rangi zake za ajabu, akaamini kuwa ni almasi halisi. Mtu huyu atakuwa anaamini kuwa amefanya chaguo sahihi, lakini kwa kweli, mtu huyo amedanganywa. Wakati watu wanawaamini mashahidi wa uongo wanaodai kuwa pete hiyo imeundwa kwa almasi wakati si kweli, basi almasi hii ya uongo ni sawa na almasi halisi kwa watu hawa waliodanganywa, kwa kuwa wanaamini kwa upofu kwamba pete hiyo imeundwa kwa almasi. Lakini kwa kweli kile walichokuwa nacho si kitu halisi. Vivyo hivyo, kuna watu ambao wana imani potofu isiyo sahihi. Japokuwa wanauhakika na imani yao, ni imani potofu, isiyo na msingi na ya kimafumbo, kwa kuwa haitoki katika Neno la Mungu.
Mungu alisema, “Msiiabudu miungu mingine bali Mimi.” Neno la Mungu ni Mungu mwenyewe, na Neno linatuambia sisi kuwa ni hadi pale tutakapozaliwa kwa maji na Roho, ndipo tunapoweza kuuona Ufalme wa Mungu (Yohana 3:5). Mungu anatueleza sisi kuwa pasipo kupitia kwanza katika lango la ua wa Hema Takatifu la Kukutania lililofumwa kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa, hatuwezi kuingia katika ua wa Hema Takatifu la Kukutania, na kwamba wale wasioosha kwanza mikono na miguu yao katika birika la kunawia hawawezi kuingia katika Hema Takatifu la Kukutania. Kwa kuwa Neno hili ni la kweli, basi kitu kingine chochote zaidi ya hiki ni uongo.
Imani pekee katika ukweli huu ndiyo imani halisi, na imani katika kitu kingine chochote ni uongo. Haijalishi kuwa watu wanaamini kwa nguvu na juhudi kiasi gani, kitu ambacho si Neno la Mungu kinabaki kuwa si Neno la Mungu hadi mwisho. Wakati Yesu anakueleza wewe kuwa amezifanya dhambi zako zote kutoweka kwa ubatizo wake na damu Msalabani, unachotakia kukifanya ni kuamini tu. Kwa kuwa anayekuambia kuwa amefanya hivyo ni Mungu, basi imani hii katika Neno lake ni halisi. Ikiwa Bwana wetu kwa hakika hajafanya hivi, basi hili ni kosa lake, na imani yako mwenyewe haina kosa. Kwa upande mwingine, ikiwa kwa hakika Bwana amefanya hivyo, lakini bado wewe hauamini na kwamba haujaokolewa, basi kwa hakika huu ni wajibu wako binafsi wa kuwajibika. Hii ndiyo sababu tunachotakiwa kukifanya ni kuamini. Ni lazima tuamini kile ambacho Mungu anakiongea kwetu kwa kupitia Kanisa lake. Je, unaamini?
Je, ni Neno gani lililozungumzwa kupitia Kanisa? Ni Neno la Yesu Kristo aliyekuja kwetu kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Kanisa linaeneza Neno lote la Mungu, kwamba Yesu alizichukua dhambi zetu katika mwili wake, kwa kubatizwa, kwamba Yesu ni Mungu mwenyewe, na kwamba alibeba adhabu yote ya dhambi zetu Msalabani. Imani katika ukweli huu kwamba Yesu ametuokoa sisi, ni imani ya almasi halisi iliyohakikishwa na Mungu.
Tunapoifahamu kwanza nia ya Mungu na maana ya kiroho iliyodhihirishwa katika Hema Takatifu la Kukutania na kisha kuizungumzia, ni rahisi kiasi hiki. Lakini ikiwa tungefuatia halafu tukashindwa kuifahamu, tukabakia na elimu ya kawaida kuhusu muundo wake wa nje wa Hema Takatifu la Kukutania, tukalifahamu neno la asili la Kiebrania linalomaanisha Hema Takatifu la Kukutania, au ikiwa tungeufahamu msingi wake wa kihistoria, basi kwa hakika tusingepata faida yoyote zaidi ya kuishia kuwa na maumivu ya kichwa.
Amini katika ubatizo wa Yesu. Yesu aliupokea ubatizo unaosafisha giza lote, uchafu wa dhambi ambazo zimo hata katika mioyo yetu. Ubatizo maana yake ni kuzioshelea mbali dhambi, kuzipitisha kwa mtu au kitu kingine, kufukia, kuhamishia, na au kufunika. Ni kwa sababu Yesu aliupokea ubatizo wa jinsi hiyo ndio maana aliweza kuzichukua dhambi zetu zote katika mwili wake. Wale wasioamini katika ukweli huu wote wataangamizwa na kutupwa kuzimu. “Fanya na shaba, na kitako chake cha shaba, ili kuogea... basi wataosha mikono yao na miguu yao ili kwamba wasife; na neno hili litakuwa amri kwao milele, kwake yeye na kwa wazao wake katika vizazi vyao vyote” (Kutoka 30:18, 21). Kutoamini ni kulaaniwa. Kutoamini ni kutupwa kuzimu. Ikiwa hauamini, laana ya Yehova na uharibifu utakushukia wewe, na utatupwa katika moto wa milele.
“Basi wataosha mikono yao na miguu yao ili kwamba wasife.” Mungu alisema hivi kwa Kuhani Mkuu, akasema kuwa ni amri ya milele ambayo yeye na wana wake na vizazi vyake vyote ni lazima waifuate. Mtu yeyote ambaye anataka kumwamini Yesu kuwa ni Mwokozi wake ni lazima aamini katika ubatizo wake na damu ya Msalaba. Imani ni ya wale ambao wanaipokea na kuichukua kwa ujasiri. Wokovu unakuwa wako pale unapoukubali na kuupokea katika moyo wako kwa kuamini. Ukweli unaweza kuwa na faida kwetu pale tu tunapouamini. Ni lazima tuamini katika lile ambalo Mungu ametueleza. Hakuna kizuizi kwa moyo kilicho kikuu zaidi ya kutoamini.
Mungu alisema kuwa wakati makuhani wanakwenda mbele zake, ni lazima kwanza waoshe mikono na miguu yao ili iwe safi katika birika la shaba la kunawia, lakini bado kuna watu wengi ambao hawana imani ya kuosha mikono na miguu yao kwa maji ya birika la kunawia. Kila mtu ambaye hana imani hii iliyodhihirishwa katika birika la kunawia atauawa mbele za Mungu. Amini katika injili ya maji na Roho katika moyo wako na usafishwe uwe safi, ili kwamba uweze kwenda mbele za Mungu, ili uepuke kifo, na kisha upokee Ufalme wa Mungu kuwa zawadi yako. Haijalishi utahoji kwa kiasi gani na kung’ang’ania mbele za Mungu, kwa hakika utaadhibiwa kwa sababu ya kutoamini pale ulipopewa nafasi ya kufanya hivyo. Ninatumaini na kuomba kuwa asiwepo kati yenu hata mmoja ambaye atakumbana na kifo kwa sababu ya kutouamini ukweli huu.
Ikiwa hauamini ukweli wa wokovu uliozitowesha dhambi zako kwa ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani, kwa hakika utajeruhiwa vibaya. Je, unaamini? Ni lazima tumshukuru Mungu kwa kutuokoa toka katika dhambi zetu na adhabu kwa kupitia birika la kunawia.
Sehemu iliyobakia ya Hema Takatifu la Kukutania itajadiliwa kwa mfuatano na kitabu hiki, yaani katika kitabu kingine kinachofuata kuhusu Hema Takatifu la Kukutania. Ninaamini kuwa ninyi nyote mtakuwa na fursa ya kufanyika wana wa Mungu kwa kupitia ujumbe wa vitabu hivi.