Search

Mahubiri

Somo la 11: Maskani

[11-18] Meza ya Mikate ya Wonyesho (Kutoka 37:10-16)

Meza ya Mikate ya Wonyesho
(Kutoka 37:10-16)
“Kisha akafanya hiyo meza ya mti wa mshita; urefu wake ulikuwa ni dhiraa mbili, na upana wake ulikuwa ni dhiraa moja, na kwenda juu kwake kulikuwa ni dhiraa moja na nusu; naye akaifunika dhahabu safi, akaifanyia ukingo wa dhahabu kuizunguka pande zote. Kisha akaifanyia upapi wa upana wa shibiri kuizunguka pande zote, akauzungushia ukingo wa urembo wa dhahabu ule upapi. Naye akasubu vikuku vinne vya dhahabu kwa ajili yake, akavitia vile vikuku katika pembe nne, katika miguu yake minne. Vile vikuku vilikuwa karibu na ule upapi, ili viwe mahali pa kutilia ile miti, kuichukulia meza. Naye akaifanya hiyo miti ya kuichukulia, ya mti wa mshita, akaifunika dhahabu, ili kuichukua hiyo meza. Kisha, vile vyombo vilivyokuwa juu ya meza, sahani zake, na miiko yake, na bakuli zake, na makopo yake ya kumiminia, akavifanya vya dhahabu safi.”
 


Kwa Kuweka Ukingo katika Mioyo Yetu, Ni Lazima Tufanyike Wale Tunaokula Mkate wa Uzima

Jedwali la mkate wa wonyesho
Meza ya mikate ya wonyesho ambayo ni moja ya vifaa vinavyopatikana ndani ya Hema Takatifu la Kukutania iliundwa kwa mti wa mshita na kisha ikafunikwa kwa dhahabu safi. Ilikuwa na vipimo vya dhiraa mbili (sentimita 90: futi 3) kwa urefu, dhiraa moja na nusu (sentimita 67.5: futi 2.2) kwa kimo, na dhiraa moja (sentimita 45: futi 1.5) kwa upana. Juu ya meza ya mikate ya wonyesho kulikuwa na mikate 12 ambayo iliwekwa pale wakati wote, na mikate hii iliweza kuliwa na makuhani tu (Mambo ya Walawi 24:5-9). 
Miongoni mwa tabia za meza ya mkate wa wonyesho zilikuwa ni: ilikuwa na ukingo wa upana wa mkono kuizunguka meza yote; na kisha upapi wa dhahabu uliwekwa kuuzunguka ukingo huu; pete nne za dhahabu (vikuku) ziliwekwa katika kona nne; na pete hizi ziliishikilia ile miti (mihimili) ya mti wa mshita iliyokuwa imefunikwa kwa dhahabu ambayo ilitumika katika kuisafirishia ile meza. Vyombo katika ile meza—yaani sahani zake, vikombe, bakuli, na makopo ya kumiminia viliundwa pia kwa dhahabu.
Kutoka 37:11-12 inaeleza kuwa, “naye akaifunika dhahabu safi, akaifanyia ukingo wa dhahabu kuizunguka pande zote. Kisha akaifanyia upapi wa upana wa shibiri kuizunguka pande zote, akauzungushia ukogo wa urembo wa dhahabu ule upapi.” Meza ya mikate ya wonyesho katika Mahali Patakatifu pa Nyumba ya Mungu ilikuwa na ukingo uliokuwa na upana wa kiganja cha mkono, na kuuzunguka huo ukingo kulikuwa na upapi wa dhahabu. Kwa nini Mungu alimwamuru Musa kuuweka ukingo wa jinsi hiyo? Ukingo huu wenye upana wa kiganja cha mkono uliokuwa umeinuka kwa takribani sentimita 10 ulilenga kuzuia mikate isianguke. 
Kwa kuwa ni makuhani tu ndio walioweza kuila ile mikate iliyokuwa imewekwa juu ya meza ya mikate ya wonyesho, hivyo inatupasa na sisi tufanyike wale wanaoweza kuila mikate hii kiroho. Ni wale tu waliookolewa toka katika dhambi na kupokea uzima wa milele kwa kuamini katika ubatizo wa Yesu Kristo na damu yake Msalabani ndio wanaoweza kuila mikate ile. Kwa maneno mengine, ni wale tu wanaoamini katika injili ya maji na Roho kuwa ndio wokovu wao ndio wanaoweza kuila mikate hii. 
Kwa kuwa ukingo uliokuwa na upana wa kiganja cha mkono uliwekwa kuizunguka ile meza ya mikate ya wonyesho ya Hema Takatifu la Kukutania, ukingo huo ulihakikisha kuwa hakuna mkate utakaoteleza na kuanguka chini. Na katika kila Sabato, mikate ya moto na iliyookwa karibuni iliwekwa katika ile meza. Ni lazima tuzingatie ukweli kuwa ule ukingo wenye upana wa kiganja cha mkono uliwekwa kuizunguka ile meza ya mikate ya wonyesho, na kwamba ule ukingo ulizungukwa pia na upapi wa dhahabu. 
Ukingo wa meza ya mikate ya wonyesho unatufundisha sisi kuwa ni lazima tulishikilie Neno la ukweli katika mioyo yetu ambalo linatuletea uzima ili kwamba tupokee uzima wa milele. Hii inatueleza sisi kuwa tunaweza kuwa na imani ya kiroho ya nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa zilizotumika katika mlango wa Hema Takatifu la Kukutania pale tunapoamini katika ubatizo wa Yesu Kristo na damu ya Msalabani. Kwa kupitia ufunuo huu tulikuja kufahamu kuwa ni wale tu wanaoamini katika ukweli huu uliodhihirishwa katika nyuzi hizi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa wamefanyika kuwa wana wa Mungu. 
Kwa kuwa hatutakuwa na jambo lolote la kufanya na Bwana mpaka pale tutakapoamini kwa namna hii, hivyo sisi sote ambao tunataka kuupata mkate wa uzima ni lazima tuwe na imani inayoamini katika injili ya maji na Roho iliyodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Ni lazima tuamini kuwa injili ya maji na Roho ndiyo ukweli pekee wa wokovu. Kwa kifupi, Mungu anatuambia sisi kuuinua ukingo wa imani katika mioyo yetu ili kwamba Neno la wokovu lisiweze kutelezea mbali toka kwetu. 
Injili hii ya maji na Roho imeletwa kwetu toka katika kipindi cha Kanisa la Kwanza. Toka katika kipindi hiki cha Kanisa la Kwanza hadi sasa, Mungu amezisafishia mbali dhambi za wale wote ambao wanaamini katika injili hii. Tunaweza kuona sasa kama ilivyokuwa hapo kabla kuwa Mungu anaziokoa nafsi za wale wanaoamini katika ukweli wa injili hii ya maji na Roho. Sisi tumeokolewa kwa kuamini katika ukweli uliodhihirishwa katika mlango wa Hema Takatifu la Kukutania, na Mungu ametuwezesha kuishi kiroho kwa kuuinua ukingo katika mioyo yetu. 
Toka katika imani yetu ya injili ya maji na Roho iliyotolewa na Bwana, sisi tumepokea uzima wa milele, na kwa injili hii ya ukweli tumeweza kuwashirikisha wengine kuhusiana na huu mkate wa uzima. Pia tumefikia hatua ya kuzitumikia kazi za haki za Mungu. Hata pale tunapoamini katika injili ya maji na Roho, ikiwa tutashinda kuushika kwa ukakamavu ukweli wa injili hii na kisha kuupoteza, basi hii itamaanisha kuwa ni sawa ya kuyapoteza maisha yetu binafsi. Kwa hiyo, ni lazima tuuinue ukingo wa imani katika mioyo yetu kwa kuitafakari injili ya maji na Roho kwa imani.
 


Katika Mioyo Yetu ni Lazima Kuwe na Imani Inayoamini Katika Injili Inayopatikana Katika Nyuzi za Bluu, Zambarau, na Nyekundu

 
Ikiwa watu hawana imani katika ukweli huu, basi kwa kweli hawawezi kuokolewa toka katika dhambi zao. Wanaweza kusisitiza wao wenyewe kuwa wameokolewa, lakini kwa kuwa mioyo yao haiwezi kuishikilia na kuiamini injili ya maji na Roho iliyodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu, basi wokovu huu ambao wanao ni wokovu usio sahihi. 
Kutoamini katika injili ya maji na Roho kuwa ni kweli ni sawa na kumkataa Bwana sisi wenyewe. Mkate wa uzima si kitu ambacho tunakihitaji kuwa nacho kama kitu, bali ni kitu ambacho ni lazima tukiweke katika vinywa vyetu, tuutafune, na kisha tuule, na kisha tuufanye ule ukweli wake kuwa ni mali yetu. Tunapoenenda pasipo kuamini katika Neno la Mungu na pasipo kulishikilia katika mioyo yetu, basi ukweli wa wokovu utapotea toka katika mioyo yetu mara moja. 
Unaweza kushangaa jinsi inavyowezekana kwa wewe kuupoteza wokovu wa thamani kiasi hicho wakati ambapo umekwisha okolewa toka katika dhambi. Lakini kwa bahati mbaya, wengi wasiolishikilia Neno la Mungu, ingawa walikuwa wameupokea ule ukweli kwa furaha wataishia kifoni, kwa kuwa hawana mizizi ya imani iliyosimikwa katika injili ya kweli. 
Kuhusiana na suala hili, Yesu alizungumzia juu ya tofauti za misingi yetu ya kiroho katika ule ‘mfano wa mpanzi’ (Mathayo 13:3-9, 18-23). Katika mfano huu, mbegu za ukweli wa Mungu zilipandwa katika aina nne tofauti za ardhi za moyo wa mwanadamu. Ardhi ya kwanza ilikuwa ni barabarani, na ya pili ilikuwa ni mahali penye miamba na mawe, na aina ya tatu ilikuwa ni mahali penye miiba na michongoma, na uwanja ule wa nne ulikuwa ni mzuri wenye rutuba. Katika aina hizi, zile mbegu zilizoanguka katika viwanja vile vitatu vya kwanza zilishindwa kuzaa matunda yoyote. Hii inamaanisha kuwa watu wengi wanaweza kuupoteza wokovu wao katikati hata kama waliwahi wakati fulani kuisikia na kuikubali injili ya maji na Roho ambayo ni injili ya kweli ya wokovu. Kwa hiyo, ni lazima tukumbuke kuwa ikiwa ardhi ya mioyo yetu si nzuri, inawezekana kwetu sisi kuupoteza wokovu wetu ambao Bwana ametupatia. 
Ikiwa katika mioyo yetu tunaamini katika wokovu ambao umekuja kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu, basi ardhi za mioyo yetu zinaweza kuwa nzuri. Lakini kwa nyakati fulani tunaona kuwa baadhi ya watu wanapoteza wokovu wao kwa sababu ya kushindwa kuilinda imani yao kwa sababu imani yao haina mizizi katika Neno la Mungu. Hii ndiyo sababu inayotufanya tukae katika Kanisa la Mungu, ili tuupate mkate wa uzima kila siku, na kisha kukua katika imani. Kwa kupitia ukweli uliodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu, Mungu anatulea sisi kila siku ili kwamba imani yetu iweze kukua.
Ni lazima tukubali na kukiri katika mioyo yetu kila siku juu ya ondoleo la dhambi ambalo tumelipokea. Ukweli ambao ni lazima upatikane katika mioyo yetu ni wokovu wa injili ya maji na Roho uliodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Ukweli huu wa wokovu upo katika mioyo ya wale ambao wamepokea ondoleo la dhambi. Kwa kuinoa imani yetu katika injili hii ya kweli ya maji na Roho, basi tunaweza kuishi siku hadi siku kama watoto wa Mungu. 
Kwa hiyo, hata wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho ni lazima pia watafakari kila siku juu ya injili ya haki ya Mungu iliyodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa, pia ni lazima waithibitishe imani yao kila siku. Kwa nini? Kwa sababu ikiwa hatuishikilii kila wakati injili ya maji na Roho kwa mkazo na kuithibitisha, basi tunaweza kuipoteza wakati wowote. Ni lazima tukumbuke daima kile ambacho mwandishi wa Waebrania aliwaambia Wayahudi waliokuwa wametawanyika: “Kwa hiyo imetupasa kuyaangalia zaidi hayo yaliyosikiwa tusije tukayakosa” (Waebrania 2:1).
Siku hizi, hata miongoni mwa wale wanaoifahamu injili ya maji na Roho, tunaona kuwa kuna baadhi ambao imani yao katika injili inapotelea mbali kadri muda unavyozidi kwenda. Hii ni kwa sababu, pamoja na kuwa walikwisha amini katika injili ya maji na Roho, wameshindwa kuendelea kuula mkate wa uzima siku zote katika Mahali Patakatifu, kitu ambacho kimesababisha mioyo yao kutojazwa na kusafishwa kwa imani ya kweli. 
Pia kuna watumishi wengi wa Shetani katika ulimwengu huu ambao wanajaribu kuwaua wenye haki kwa kuwalisha mkate uliochacha ambao ni mafundisho ya miili yao tu. Ikiwa injili potofu na ya uongo ikiletwa katika Kanisa la Mungu, basi ukweli unachanganywa na uongo na hivyo unawafanya waamini kuwa wale ambao hawawezi kupokelewa na Bwana. Watu wa jinsi hiyo wanaufahamu ukweli lakini hawauamini kwa sababu ya kushindwa kuukuza ule ukingo wa imani, na hivyo hatimaye wanaishia kuwa ni watu ambao hawajaokolewa kikamilifu toka katika dhambi. Mithali 22:28 inasema, “Usiiondoe alama ya mpaka wa zamani, Uliowekwa na baba zako.” 
Kwa hiyo ni suala la muhimu sana kwetu kuhakikisha kuwa hatuuondoi mpaka wa imani yetu. Ni lazima tuwe na mpaka wa imani yetu ya kweli na kisha tuulinde hadi siku ile Bwana atakaporudi. Ni hapo tu ndipo tunapoweza kujilisha katika mkate wa uzima, na ndipo hapo Mungu anapoweza kufanya kazi katikati ya mioyo yetu, na ndipo hapo tunapoweza kuupata uzima wa milele. Haijalishi kuwa ni kiasi gani cha mkate Mungu anatupatia, ikiwa hatutakiri na kuthamini uthamani wake na kisha tukashindwa kuushikilia kwa mioyo yetu, au ikiwa tutaondoa ukingo na kisha kuufanya mkate kuteleza na kuanguka toka katika meza, basi hatimaye tutaishia kubadilika kuwa wana wa uharibifu.
Baadhi yetu tumepokea ondoleo la dhambi hivi karibuni, wakati kwa wengine imeshakuwa ni miongo kadhaa tangu pale waliposikia kwa mara ya kwanza injili ya maji na Roho na kisha wakaondolewa dhambi zao. Kwa kuwa kile tunachokisikia kila siku ni Neno la injili ya maji na Roho, basi inawezekana sana kuwa baadhi yetu tukachoka sana kadri neno “maji” ya injili ya maji na Roho linapotamkwa. Lakini hata hivyo, ni lazima tuendelee kuula mkate wa ukweli wa injili. Je, tufanye hivi kwa muda gani? Ni hadi siku ile Bwana atakaporudi. 
Baadhi yenu mnaweza kulalamika kuwa ninarudiarudia na kuhubiri kila mara injili ya maji na Roho, lakini mnahitaji kutambua kuwa ni kwa nini ninahubiri kwa namna hii. Ni kwa sababu imani yetu ni lazima iimarishwe zaidi na zaidi kwa kutafakari juu ya injili ya maji na Roho ili tuweze kufanyika kuwa watumishi wa Mungu. Ni lazima tulitimize jukumu la mlinzi mwaminifu na aliye makini kwa ajili ya nafsi za nyakati hizi. Kwa nafsi za waliozaliwa upya, injili hii ya kweli ya maji na Roho ni mkate wa uzima na chakula cha kweli cha imani. Kwa hiyo, ni lazima tuupate mkate huu kila siku, na sio hivyo tu—bali, hatupaswi kuupata na kuula kwa ajili yetu tu—bali na tuwashirikishe wengine pia kila siku ili kwamba nao waweze kupokea ondoleo la dhambi zao. 
Mkate wa wenye haki ni kulieneza Neno la injili ya maji na Roho ili kwamba watu wakombolewe toka katika nguvu za giza na kisha kuwaingiza katika Ufalme wa Mwana wake mpendwa (Yohana 4:34, Wakolosai 1:13). Ikiwa tutadharau kuula mkate wa injili ya maji na Roho, basi kwa hakika tutaanguka tukiwa wagonjwa au wafu. Kwa baadhi ya nyakati, kwa sababu ya udhaifu wa miili yetu, imani yetu katika injili ya maji na Roho inaweza kudhoofika. Lakini ikiwa tutaishikilia injili ya maji na Roho katika nyakati za shida, basi hali hiyo inaweza kubadilishwa kuwa katika hali ya fursa kwa nafsi zetu kuwa na nguvu zaidi. 
Tunapoisikia na kuitafakari injili hii ya kweli, kadri tunavyoisikia ndivyo nafsi zetu zinavyozidi kuwa imara, na kadri imani yetu inavyozidi kuwa na nguvu, basi ndivyo tunavyozidi kuona nguvu mpya ikiinuka katika mioyo yetu. Tunahitaji kuisikia injili ya maji na Roho kila siku, na kuithibitisha na kuisafisha imani yetu katika injili. Kama Mungu alivyosema, “Ondoa takataka katika fedha, na chombo kitatokea kwa mtakasaji” (Mithali 25:4), tunahitaji utakaso wa imani—ambayo ni kusema kuwa, tunahitaji kuendelea kuisikia injili ya maji na Roho, kuikubali katika mioyo yetu, na kuitafakari muda baada ya muda—kwa kuwa injili ya maji na Roho ni mkate wa uzima unaotufanya sisi kuwa hai! Kama ambavyo Yesu alisema katika Sala ya Bwana, “utupe mkate wetu wa kila siku,” kwa kweli Bwana wetu ametupatia sisi Neno la injili ya maji na Roho. Na hii ndio sababu alituambia kuomba kwa namna hii. 
Inapofikia sasa katika wokovu wa ondoleo la dhambi ambao Mungu ametupatia, ni lazima tuweke wazi jinsi ambavyo imani yetu ilikuwa kabla hatujaokolewa toka katika dhambi. “Kabla sijaufahamu ukweli huu, nilikuwa sijaokolewa toka katika dhambi.” Ni lazima tukiri kuwa kwa wakati huo, ingawa tulikuwa tukiamini katika Yesu, bado tulikuwa hatujaokolewa toka katika dhambi. “Nilikuwa sijaokolewa kikamilifu toka katika dhambi kwa wakati huo, lakini nilipoendelea kuisikia injili hii ya maji na Roho, basi nilikuja kuiamini injili hii katika moyo wangu kwa wakati wake. 
Pamoja na kuwa hapo kabla nilikuwa nikimwamini Yesu kuwa ni Mwokozi wangu, wokovu wangu haukuwa mkamilifu hadi wakati huo ulipowadia, lakini sasa, kwa kuisikiliza injili ya kweli ya maji na Roho, kwa kweli nimeokolewa kikamilifu. Sasa ninaweza kuamini kikwelikweli katika injili ya maji na Roho, na kwa kweli ninaiamini injili hiyo kiukweli.” Ni pale tu unapotambua na kuamini kuwa Bwana amekuokoa kikamilifu toka katika dhambi kwa ubatizo wake na damu yake Msalabani ndipo ile karama ya wokovu wa kweli inashuka katika moyo wako toka Mbinguni. Imani hii inayoamini katika ukweli ni imani ya kweli inayokuokoa wewe. 
Injili ya maji na Roho iliyofunuliwa katika Biblia ni tofauti na imani ile ambayo tulikuwa nayo hapo kabla. Kwa wakati fulani, sisi tuliamini katika injili ya damu ya Msalaba tu badala ya kuamini katika injili hii sahihi ya maji na Roho. Imani katika injili ya Msalaba tu na imani katika injili ya maji na Roho vinaweza kuonekana kuwa vinafanana katika hatua zake za awali, lakini injili hizo mbili ni tofauti kabisa hasa zinapofikia mwishoni. Kabla ya kuja kuifahamu injili hii ya maji na Roho, je, hukuamini tu katika damu ya Msalaba tu? Je, dhambi zako ziliondolewa zote wakati huo? Kwa kweli sivyo! Unapoamini katika damu ya Yesu tu Msalabani bado unabakia kuwa na dhambi halisi katika moyo wako. Hii ndiyo tofauti kati ya imani inayoamini katika injili ya maji na Roho na imani inayoamini katika Msalaba tu. 
Tofauti ya wazi ni kuwa wale wanaoamini katika damu ya Msalaba tu hawajaokolewa wakati wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho wameokolewa toka katika dhambi zao zote. Kwa hiyo, roho zao zina tofauti kabisa. Lakini watu wa kawaida hawalitambui jambo hili. Ingawa injili hizi mbili zinaweza kuonekana kuwa zinafanana, bado kuna pengo kubwa sana la kiimani kati ya injili hizi mbili ambalo haliwezi kuwekewa daraja. Wakati tofauti ndogo ya kuwa ikiwa tunaamini au hatuamini katika ubatizo wa Yesu ndiyo inayotufanya tupokee au tuupoteze uzima wa milele, basi kwa hakika tunaweza kukiri kuwa kuna tofauti kati ya imani hizi mbili ambazo haziwezi kurukwa. 
Ni lazima tufahamu kiusahihi kuwa ni imani ipi ambayo inao mpaka wa wokovu toka katika dhambi. Ili tuweze kuokolewa toka katika dhambi, ni lazima tuiamini injili ya maji na Roho. Injili hii ya maji na Roho ni ukweli wa ondoleo la dhambi. Hali yako angavu ya wokovu itakuwa yako pale utakapokiri kuwa kwa hakika ulikuwa haujaokoka kabla hujaamini katika injili ya maji na Roho, na kwamba sasa unaamini katika injili ya kweli kwa moyo wako wote. 
Ikiwa unaamini katika injili ya maji na Roho katika kina cha moyo wako, basi ni lazima ulikiri jambo hili mbele za Mungu kwamba umepokea ondoleo la dhambi zako kwa kusikia na kuamini katika injili ya maji na Roho. Ikiwa haujaamini katika ukweli huu wa injili ya maji na Roho, basi kwa hakika na pasipo shaka unaweza kuupata ushahidi wake katika moyo wako. 
Ni lazima tuichunguze imani yetu kwa uangalifu mbele za Mungu. Kwa hakika hakuna aibu yoyote ya kuichunguza imani yetu. Ikiwa ilikuchukua miaka mitano tangu pale ulipomwamini Yesu kwa mara ya kwanza hadi kufikia hatua ya kuamini katika injili ya maji na Roho katika kina cha moyo wako, basi kwa hakika hakuna aibu yoyote. Ikiwa ilikuchukua miaka 10 hadi kuokoka, basi hakuna aibu katika hili, na kama ilikuchukua wewe hata miaka 20 hadi kuokolewa, basi kwa hakika hakuna aibu katika hili. Kinyume cha jambo hili ni baraka tupu. 
Hata hivyo, ukweli ni kuwa kuna watu wengi ambao wanajifanya kuwa wameokolewa toka katika dhambi. Lakini Roho Mtakatifu, anayekagua kila kitu hawezi kuithibitisha imani yao kwa sababu hawauchori mstari sahihi wa wokovu wao kwa uaminifu. Ni busara zaidi hata sasa, kuweka mchoro wa mpaka wa wokovu wetu kwa wazi—si kuifahamu siku kamili ambayo tuliokolewa bali ni kuweza kutofautisha kwa wazi kabisa kati ya ilivyokuwa hapo kabla na baada ya kuokolewa—na kisha kuikiri imani yako sahihi kipekee.
 
 

Baba Zetu wa Imani Pia Waliamini katika Injili Hii Tunayoiamini

 
Baada ya kuwa wameivuka Bahari Nyekundu, wakati watu wa Israeli walipokuwa wakielekea kuuvuka Mto Yordani ili kuingia katika nchi ya Kanaani, waliweza kuvuka salama pale walipowafuata makuhani wao ambao walikuwa wamelibeba Sanduku la Mungu la Ushuhuda. Ikiwa tutajifikiria sisi wenyewe, “Aha, hivyo ndivyo ninavyoweza kuuvuka Mto wa Yordani,” halafu usiuvuke huo mto, basi kwa hakika huwezi kuingia katika nchi ya Kanaani, kwa kuwa utakuwa bado umebakia katika upande mwingine wa mto. Ili kuingia katika nchi ya Kanaani, ni lazima na kwa hakika tuivuke Bahari Nyekundu na Mto Yordani kwa imani yetu katika Bwana. 
Tukiongea kiroho, Mto Yordani ni mto wa mauti na ufufuo. Imani ambayo imetuokoa sisi toka katika dhambi ni imani inayoamini kama hivi, “Ni lazima nitatupwa kuzimu, lakini Bwana alikuja hapa duniani na ameniokoa mimi kwa ubatizo wake na damu yake Msalabani.” Ili kutuokoa kikamilifu, Bwana wetu alibatizwa katika Mto Yordani na kisha akaimwaga damu yake Msalabani. Kwa njia hii Yesu alizichukua dhambi zetu katika mwili wake na akalipa mshahara wa dhambi kwa kuyatoa maisha yake kwa niaba yetu. Sasa, ni lazima tuamini katika ukweli huu na kisha kuuchora mstari wa imani na mstari wa wokovu vizuri katika mioyo yetu. 
Kadri ninavyolihubiri Neno la Mungu, ninaweza kuona kuwa kuna watu wengi katika Kanisa la Mungu ambao bado hawajachora vizuri mstari wa wokovu katika kina cha mioyo yao na kwa hiyo hawawezi kumfuata Bwana. Wanashangaa jinsi wanavyoweza kuuchora mstari huu kati ya kabla na baada ya wokovu wao. Wanatoa udhuru kwa kusema, “Je, kumekuwapo na mtu yeyote katika dunia hii aliyewahi kuchora mstari huu? Je, Mtume Paulo alifanya hivyo? Je, Petro alifanya hivyo? Hakuna hata mmoja aliyefanya hivi.” Lakini Mitume wa imani kama vile Paulo na Petro wote walichora mstari wa wokovu. 
Kwa mfano Paulo, aliweza kuuchora mstari huo alipokuwa njiani kuelekea Dameski. Kwa hiyo aliyataja sana maneno haya huku akiyarudia, “mara, wakati uliopita, au kabla” hali aliyalinganisha na neno “sasa.” Pia kwa Petro, pia alitumia maneno yaleyale kama hayo hapo juu (1 Petro 2:10, 14, 25). Tunaweza kuona kuwa aliuchora mstari huu tunapoutazama ukiri huu: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai” (Mathayo 16:16), na, “Mfano wa mambo hayo ni ubatizo, unaowaokoa ninyi pia siku hizi; (siyo kuwekea mbali uchafu wa mwili, bali jibu la dhamiri safi mbele za Mungu), kwa kufufuka kwake Yesu Kristo” (1 Petro 3:21). Paulo na Petro wote walichora kwa wazi kabisa mstari wa imani kati ya kabla na baada ya wokovu wao. 
Kwa hiyo, hili swali la kuwa ikiwa unaamini au hauamini katika injili ya maji na Roho si tatizo la mtu fulani, bali kwa hakika ni tatizo la nafsi yako mwenyewe. Watumishi wa Mungu katika Biblia wote walishughulikia tatizo la dhambi. Kwa sababu hili ni tatizo la msingi kwenu nyote, sisi wenyewe ni lazime tulitatue tatizo hili kwa imani. Tunapoamini katika injili ya maji na Roho na kwahiyo kuweza kulitatua tatizo la dhambi toka katika kina cha mioyo yetu, basi Mungu anafurahishwa sana. Je, unapenda kumfurahisha Mungu? Basi kile unachotakiwa kukifanya ni kuitambua hali yako ya dhambi na kisha kulitatua tatizo hili kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. Ikiwa wakati huu wote hujaokolewa bado, basi ni lazima ukiri, “Mungu, mimi bado sijaokolewa.”
Yesu alisema, “Na lolote utakalolifunga duniani litakuwa limefungwa mbinguni; na lolote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni” (Mathayo 16:19). Katika upande wetu, ni lazima kwanza tukiri, “Mungu ameniokoa mimi kwa maji na Roho. Kwa sasa, katika kina cha moyo wangu, ninaamini katika ukweli wa injili ya maji na Roho. Hakuna mashaka yoyote kuwa Bwana ameniokoa mimi kwa kupitia injili ya maji na Roho.” 
Sisi sote ni lazima tuikubali injili ya maji na Roho katika mioyo yetu. “Ninaamini katika injili hii. Kwa sababu ni kweli, kwa sababu Bwana amezitoweshea mbali dhambi zangu kuliko kawaida, sasa ninaamini katika injili hii. Mimi sijaokolewa kwa imani.” Wakati tunapotambua na kuamini katika injili iliyotolewa na Bwana, basi Mungu anatueleza sisi kuwa, “Ninaithibitisha imani yako.”
Wakati Mungu anapokuwa amekwisha kutupatia ukweli wa maji na Roho ambavyo vinaweza kutuokoa kikamilifu, sisi, kwa upande wetu, ikiwa tutashindwa kuuchora mstari wa wokovu na kuukubali wokovu huu kwa kuamini katika ukweli huu, basi Mungu, kwa upande wake, hawezi kututambua sisi kama watu tuliookolewa. Kwa kuwa Mungu anatuchukulia sisi kwa mwonekano wetu na si kwa ulazima, ikiwa hauamini katika injili ya maji na Roho katika kiini cha moyo wako, basi hawezi kukupatia wewe ondoleo la dhambi. Kwa maneno mengine, ikiwa hauikiri injili ya maji na Roho katika moyo wako, basi Roho Mtakatifu hawezi kukaa katika moyo wako.
Je, tunazikataa injili zote kuwa zina makosa isipokuwa injili ya maji na Roho? Au je, tunafikiria kuwa hata hizo injili nyingine za uongo ni za muhimu, na kwamba hakuna sababu ya kuzitupilia mbali? Tunahitaji kujichunguza sisi wenyewe na kisha kuona jinsi ambavyo tunaamini. Hebu tufikirie kwa muda kidogo kwamba tumelifikia lundo la vifaa vya majumbani na vya umeme vilivyotumika. Hebu tufikirie tena kuwa tumevileta baadhi ya vifaa hivi nyumbani tukidhani kuwa vinaweza kutusaidia, lakini baadaye tukagundua kuwa hakuna hata kimoja kinachofanya kazi na kwamba vifaa hivyo vyote vilikuwa havina maana. Je, tuendelee kuvitunza vifaa hivyo au tuvitupilie mbali? Mara tunapokuwa tumeshaamua kuwa vifaa hivi havina kazi yoyote, basi kwa hakika ni sharti tuvitupilie mbali. Unapokuwa umefikia hitimisho kwamba kitu fulani hakikufai na kwamba hakina maana kabisa, basi pia ni lazima uruhusu juu ya namna ya kukitupilia mbali kimaamuzi. 
Ikiwa hivi ndivyo inavyotupasa kufanya katika masuala ya kidunia, je, inatupasa kufanya nini inapofikia kushughulika na mambo ya kiroho? Ni lazima basi tuwe na maamuzi zaidi katika kukataa uongo katika mambo yetu ya kiroho. Ni lazima tuchore mstari wa wazi ambao unaitofautisha imani yetu katika injili ya maji na Roho toka katika imani za uongo ambazo zinaamini katika damu ya Msalabala tu; ni lazima tutambue kuwa imani katika damu ya Msalaba tu haiwezi kutuletea wokovu; na ni lazima kwa maamuzi sahihi tuliondolee mbali fundisho hili bovu. Je, ipi ni injili ambayo inapatana na Biblia? Je, ni injili ya damu ya Msalaba tu? Au je ni injili ya maji na Roho? Imani yako inayoamini katika injili ya maji na Roho na ambayo ndiyo iliyokuokoa toka katika dhambi zako ndiyo imani inayomfurahisha Mungu. 
Kwa kifupi, kuna aina mbili za Wakristo: Wale wanaofahamu na kuamini katika injili ya maji na Roho na wale ambao hawaamini. Inaweza kuonekana kana kwamba wote wanaishi maisha mamoja ya kiimani, lakini ukweli wa mambo ni kuwa makundi hayo mawili ni tofauti kabisa. Je, kwa namna yoyote unafikiri kuwa injili isiyo sahihi ambayo umekuwa ukiiamini hapo kabla bado ina maana yoyote? Je, ulikuwa bado umeitunza injili hii muda huu wote ukidhani kuwa siku moja itakuja kuwa na maana? 
Imani ya jinsi hiyo ni imani ya uongo, ni kitu ambacho kimekuja kutokana na mawazo ya mwanadamu, na kwa hiyo ni lazima uyatupilie mbali mawazo yote ya uchafu ya zamani. Unapata shida katika kina cha moyo wako kwa sababu bado haujatupilia mbali mambo ambayo si ya kweli na ya uongo. Ninakushauri kukumbuka Neno lake: “Mtazishika amri zangu. Usiwaache wanyama wako wa mfugo wakazaana kwa namna mbalimbali; usipande shamba lako mbegu za namna mbili pamoja; wala usivae mwilini mwako nguvu ya namna mbili zilizochanganywa pamoja” (Mambo ya Walawi 19:19).
 

Ili Kupaingia Mahali Patakatifu, Ni Lazima Tuingie Kwa Kupitia Mlango Wake Tu.
 
Ni vifaa gani ambavyo vilitumika katika kutengenezea mlango wa Hema Takatifu la Kukutania? Mlango ulikuwa umefumwa kwa nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa. Wale waliozaliwa tena upya kwa maji na Roho ni lazima waufungue mlango huu wa Hema Takatifu la Kukutania na kisha kupaingia Mahali Patakatifu. Chini ya nguzo za mlango wa Hema Takatifu la Kukutania kulikuwa na vitako vya shaba. Vitako hivi vinatufanya tukiri kuwa injili ya maji na Roho ni ukweli wa wokovu. 
Vitako hivyo vinatufundisha sisi kuwa pamoja na kuwa tulikuwa hatuna chaguo bali kuadhibiwa na Mungu na kisha kufa kwa ajili ya dhambi zetu, kwa kupokea baraka ya kuzaliwa upya kwa maji kwa kupitia injili ya maji na Roho, sisi tumefanyika kuwa watu wa Mungu mwenyewe. Tunaweza kuingia katika Hema Takatifu la Kukutania pale tu tutakapouachilia mbali ufahamu wenye makosa kuwa, katika zile nyuzi za rangi nne zilizotumika katika ule mlango wa Hema Takatifu la Kukutania tunaweza kuokolewa kwa kuiamini huduma ya Yesu iliyodhihirishwa katika nyuzi nyekundu tu. 
Ni mpaka pale tutakapoyaachilia mbali mawazo yetu na imani binafsi, ama sivyo hatuwezi kuamini katika wokovu uliodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu. Ni lazima tutambue kuwa ukweli uliodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa ndiyo injili ya maji na Roho, na ni lazima tuikiri nadharia yetu yenye makosa pale tulipoamini katika damu ya Msalaba tu. 
Kama Mungu akipenda, basi atakuongoza katika kweli ya injili ya maji na Roho. Ni wale tu wanaoamini katika ukweli huu wa injili ya maji na Roho ndio wanaoweza kuondolewa dhambi zao zote na kisha kupokea ondoleo la uzima wa milele. Ni wakati huo tu ndipo tunapoweza kuufungua mlango wa wokovu kwa kuamini katika ukweli huu katika kina cha mioyo yetu na kisha kupaingia Mahali Patakatifu. 
Ikiwa utashindwa kuitofautisha ile dhana yenye makosa ya imani yako ya zamani ambayo ulikuwa ukiiamini kabla hujaifahamu injili ya maji na Roho, basi utakutana na adhabu ya dhambi, kwa sababu hutaweza kuokolewa. Ikiwa hili litatokea, basi huwezi kuingia katika Mahali Patakatifu na kuupata mkate wa uzima. Ni pale tu utakapoingia Mahali Patakatifu kwa kuamini katika injili ya maji na Roho ndipo unapoweza kuupata mkate bora wa uzima. 
Ni lazima mtambue kuwa Bwana amewafanya ninyi kuwa wana wake kwa kuzioshelea mbali dhambi zenu kwa ubatizo wake, ambao ni nyuzi za bluu, na kwa kubeba adhabu ya dhambi zenu kwa kuimwaga damu Msalabani, ambayo ni nyuzi nyekundu. Na ni lazima utambue kwa wazi kuwa injili ya maji na Roho ni ukweli ambao ni wa muhimu sana kwako. Unaweza kuja katika Kanisa la Mungu na kisha ukashiriki katika kuula mkate wa uzima pamoja na wenye haki pale tu utakapofahamu kuwa Mungu ndiye aliyekupatia injili ya maji na Roho na hasa pale utakapoamini katika ukweli huu. 
 


Mwili wa Bwana Ni Mkate wa Uzima na wa Ondoleo la Dhambi

 
Hebu tugeukie Yohana 6:49-53: “‘Baba zenu waliila mana jangwani; wakafa. Hiki ni chakula kishukacho kutoka mbinguni, kwamba mtu akile wala asife. Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu. Basi Wayahudi walishindana wao kwa wao wakisema, Awezaje mtu huyu kutupa sisi mwili wake ili tuule? Basi Yesu akwaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.’” Yesu alisema kuwa wale watakaoula mwili wake na kuinywa damu yake wana uzima wa milele. Kifungu hiki cha maandiko kinamaanisha kuwa sisi sote ni lazima tuule mwili na kuinywa damu ya Yesu. 
Je, inawezekanaje basi tukaula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake? Ni kwa kuamini katika injili ya maji na Roho ndipo tunapoweza kuula mwili na kuinywa damu ya Yesu. Kwa kuamini kuwa Yesu alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake kwa ubatizo wake ndipo tunapoweza kuula mwili wake, na kwa kuamini kuwa Yesu alizibeba dhambi zetu na kuhukumiwa adhabu Msalabani kwa ajili ya dhambi hizo, ndipo tunapoweza kuinywa damu ya Yesu. 
Ni lazima tuamini kuwa kwa kupitia kazi za wokovu zilizodhihirishwa katika nyuzi za bluu, zambarau, na nyekundu na kitani safi ya kusokotwa, Yesu amezitoweshea mbali dhambi zetu zote na ametufanya sisi kuwa wana wake Mungu mwenyewe. Haijalishi jinsi ambavyo umekuwa ukiamini hapo kabla haujaamini katika injili ya maji na Roho, ni lazima ukubali kuwa hii imani yako ya zamani imekuwa na makosa, na sasa ni lazima uukuze ukingo wa imani kwa kuula mwili wa Yesu na kuula mkate wa Neno. 
Yohana 6:53 inasema kuwa, “Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.” Hata sasa, kuna watu wanaokitumia kifungu hiki katika kutoa hoja zao juu ya fundisho la mageuzo kuwa mkate na divai huwa mwili halisi na damu halisi ya Yesu. Fundisho hili linashikilia kuwa mkate na divai vinavyotumika katika Ushirika Mtakatifu vinabadilika kuwa mwili halisi na damu halisi ya Yesu baada ya kuombewa kwa taratibu ile ya kiimani. Lakini ni lazima tutambue na kuamini kuwa kifungu cha Yohana 6:23, mbali na kuzungumzia juu ya nadharia hiyo ya mageuzo, ni kweli kuwa kinazungumzia juu ya injili ya maji na Roho. 
Wakati wa Ushirika Mtakatifu, ikiwa unasubiria katika mstari halafu kuhani anakupatia kile kipande cha mkate katika mdomo wako, je mkate huu ni kweli kuwa utabadilika kabisa kuwa mwili wa Yesu? Kwa kweli hauwezi! Tunaweza kuula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake kwa kuamini kwamba Yesu alikuja hapa duniani, akazichukua dhambi za ulimwengu katika mwili wake na akazisafishilia mbali kwa kubatizwa, alizibeba dhambi hizi Msalabani na akafa juu yake, na kwa hiyo ametuokoa sisi toka katika kifo. 
Wale wanaoula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake kwa imani ni wale wanaoamini katika ukweli kuwa Yesu, kwa kupitia nyuzi za bluu na nyekundu ametuokoa sisi toka katika dhambi kwa kuzichukua dhambi zetu katika mwili wake na kwa kubeba adhabu ya dhambi hizi katika mwili wake. Ni lazima tuule mwili wa Yesu na kuinywa damu yake kwa imani yetu katika ubatizo na damu ya Yesu Kristo.
Yesu alibatizwa na Yohana Mbatizaji katika Mto Yordani ili kuzipokea dhambi zetu zilizopitishwa kwake. Hebu tugeukie Mathayo 3:15-17: “Yesu akajibu akamwambia, Kubali hivi sasa; kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote. Basi akamkubali. Naye Yesu alipokwisha kubatizwa mara akapanda kutoka majini; na tazama, mbingu zikamfunukia, akamwona Roho wa Mungu akishuka kama hua, akija juu yake; na tazama, sauti kutoka mbinguni ikisema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.”
Yesu ameitimiza haki yote ya Mungu kwa sababu Yesu alizichukua dhambi zote katika mwili wake pale alipobatizwa na Yohana na akafa Msalabani. Imani yetu inayoamini katika ukweli wa injili ni kwamba dhambi zote za ulimwengu zilipitishwa kwa Yesu Kristo wakati alipobatizwa na Yohana, hii ni imani ya kweli ambayo kwa hiyo tunaweza kuula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake.
Ikiwa unautambua ukweli huu, basi kwa hakika umeshaula mwili wa Yesu kwa imani. Kule kusema kuwa dhambi zako zote za ulimwengu zilipitishwa kwa Yesu Kristo mara moja na kwa wote huo ni ukweli, na kwa hiyo ni muhimu sana kwako kuuamini ukweli huu katika kina cha moyo wako. Imani hii ni imani inayokuwezesha kuula mwili wa Yesu. Je, dhambi zako zilipitishwa kwa Yesu kwa kupitia ubatizo wake? Ni pale tu utakapoamini hivyo ndipo unapoweza kuula mwili wa Yesu. Baada ya kumbatiza Yesu, Yohana Mbatizaji alipiga kelele, “Tazama! Mwana Kondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu!” (Yohana 1:29). 
Na kwa sababu Yesu alikuwa amezipokea dhambi za ulimwengu kwa kupitia ubatizo wake, Yesu alizibeba dhambi hizo zote katika mwili wake, alisulubiwa na akamwaga damu yake na kufa. Baada ya kusulubiwa, kupigiliwa misumari katika mikono na miguu yake yote na kisha kuimwaga damu yake, Yesu alipiga kelele wakati alipokuwa akifa, “Imekwisha!” Kisha akafufuka tena toka wafu siku ya tatu, akabeba ushuhuda kwa siku 40, akapaa mbinguni kama alivyotazamia, na sasa anaketi katika mkono wa kuume wa Mungu Baba. Pia ameahidi kuwa atarudi kama alivyopaa kwenda Mbinguni. Je, unaamini katika ukweli huu katika kina cha moyo wako? Ni kwa kuamini katika ukweli huu ndipo unapoweza kuula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake. Ni pale tunapoamini kwa kweli katika vina vya mioyo yetu ndipo tunapoweza kuula mwili wa Yesu na damu yake. Ni kwa imani hii ndipo tunapoweza kuula mkate wa Mahali Patakatifu. 
Bwana alituamuru sisi kuukumbuka mwili na damu yake kila tunapokusanyika pamoja (1 Wakorintho 11:26). Kwa hiyo, kila wakati tunapokusanyika pamoja, ni lazima tuusherehekee mwili na damu ya Yesu wakati wote. Tunawezaje kuushikilia Ushirika Mtakatifu kama ni taratibu ya kiibada wakati tunapaswa kuula mwili na damu ya Yesu kwa imani kila tunapokusanyika pamoja? 
Kwa sababu tunaamini katika ubatizo ambao kwa huo Yesu alizichukua dhambi zetu katika mwili wake na katika damu yake ya thamani Msalabani, basi ni kwa imani ndio maana tunaukumbuka mwili wake na damu yake kila siku. Ni kwa sababu tunaamini katika ukweli wa maji na Rono ndio maana kila siku tunaula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake. Kama Yesu alivyosema, “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele” (Yohana 6:54), Yesu atawawafua wale wanaoula mwili wake na kuinywa damu yake siku ya mwisho. 
Ni lazima tukiri kuwa ikiwa imani yetu haituwezeshi kuula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake, basi imani ya jinsi hiyo ni potofu. Bwana wetu alisema, “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi” (Yohana 6:54-57). 
Wale wanaoula mwili wa Bwana na kuinywa damu yake kwa imani wataishi kwa sababu yake. Kwa upande mwingine, wale wasioula mwili wa Bwana na kuinywa damu yake watakufa kwa sababu hawajaamini. Lakini sio kitu kigumu kwetu sisi kuula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake kwa imani. 
Hebu tudhanie kwa muda kidogo kuwa kuna mtihani wa wokovu ambao tunapaswa kuufanya ili tuweze kuingia katika ufalme wa Mungu. Moja ya swali lake linauliza, “Ni imani gani inayokuwezesha kuula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake?” Je, tutalijibuje swali hili? Wakati mwili na damu ya Yesu vinauunda ukweli, je tutasema kuwa tuliula mwili wake wakati tuliinywa damu yake tu? Ni lazima tujibu kwa kuandika kuhusu ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani kama jibu letu sahihi. Tunaweza kuingia katika Ufalme wa Mbinguni pale tu tutakapoula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake. Hata kama tuliamini vibaya na kuelewa vibaya hapo kabla, ikiwa tutaigeuza mioyo yetu, tukaula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake, basi kwa hakika tunaweza kushinda katika jaribio hilo. Ikiwa tunaamini katika mwili an damu ya Yesu hadi sasa, kwa wakati huu huu, basi kwa hakika tunashinda katika mtihani vizuri kabisa. 
Watu wanaangalia mwonekano wa nje, lakini Mungu anauangalia moyo, na kwa hiyo tunapoamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani, basi hapo tunaula mwili wa Yesu na kuinywa damu yake. Mungu anaangalia katika kina cha mioyo kuona ikiwa tuna imani katika mwili na damu ya Yesu. Kwa hiyo, ikiwa hatuamini katika mwili na damu ya Yesu katika vina vya mioyo yetu, basi hatujaokolewa toka katika dhambi. Haijalishi jinsi ambavyo umekuwa ukiamini hapo kabla, ikiwa sasa una ile imani inayoamini katika mwili na damu ya Yesu, basi unaweza kuingia katika Ufalme wa Mungu. 
Wanadini wengi wa ulimwengu huu wanabishana sana kuhusu ukweli na uhalali wa fundisho la mageuzo ya mkate na divai katika ushirika mtakatifu. Kinachohitajika hasa ni imani inayotuwezesha sisi kuula mwili na kuinywa damu yake. Lakini hili linawezekana pale tunapoamini katika injili ya maji na Roho katika mioyo yetu. Kumwamini Yesu katika kina cha mioyo yetu kwa kupitia injili ya maji na Roho ndiko kuula mkate wa kweli na kukinywa kinywaji cha kweli. 
 

Ni Lazima Tuamini katika Ubatizo na Damu ya Yesu kuwa ni Ondoleo Letu la Dhambi
 
Bwana wetu alisema, “Damu yangu ni kinywaji cha kweli” (Yohana 6:55). Bwana wetu alibeba adhabu ya dhambi Msalabani. Imani inayoamini kuwa Yesu alizichukua katika mwili wake kwa kubatizwa na kuimwaga damu yake Msalabani ni imani inayotuwezesha kuinywa damu ya Yesu. Kwa kupitia ubatizo ambao aliupokea toka kwa Yohana, Yesu alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake, zikiwemo dhambi za watoto wako, wazazi wako, na kila mmoja wetu, Yesu alibeba adhabu ya dhambi hizi kwa kuimwaga damu yake Msalabani. Kwa ubatizo na damu yake, Yesu amelitatua tatizo la dhambi kikamilifu kwa kila mtu katika ulimwengu mzima. Kule kuamini kuwa Yesu alizichukua dhambi zetu kwa ubatizo wake na kuwa alihukumiwa adhabu kwa ajili ya dhambi zetu kwa damu yake ya Msalaba, basi huko ndiko kuinywa damu ya Yesu kwa imani. 
Katika ulimwengu wa leo, kuna wengi wanaosema kuwa wanaamini katika injili ya maji na Roho kwa maneno yao tu. Lakini hawaamini kikamilifu katika mwili na damu ya Yesu. Mtu yeyote ambaye hana imani hii kamilifu inayoamini katika mwili na damu ya Yesu hawezi kuondolewa dhambi zake. Bila shaka ulikwisha amini hapo kabla kuwa damu ya Yesu ndio ukweli pekee, lakini sasa kwa kuwa umeupata ukweli, ni lazima uwe na imani inayoamini vizuri katika mwili na damu ya Yesu. Ni hapo utakapoamini hivyo ndipo Mungu atakapokutambua kuwa wewe umeokolewa. Lakini kwa upande mwingine, ikiwa hauchori mstari wa wazi wa wokovu katika jambo hili—yaani kuhusu ondoleo la dhambi linalopokelewa kwa imani inayoamini katika mwili na damu ya Yesu katika kina cha moyo—basi imani yako haiwezi kuthibitishwa na Mungu.
Bwana wetu alisema, “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake” (Yohana 6:56). Hatuwezi kuingia katika uwepo wa Mungu hadi pale tutakapoula mwili na kuinywa damu ya Yesu kwa imani. Na kila mtu asiye na imani hii inayoamini katika mwili na damu ya Yesu hawezi kukaa ndani ya Bwana. Nimatumaini yangu kuwa hakuna yeyote miongoni mwa watakatifu, wafanyakazi na watumishi wa Mungu katika Kanisa letu ambaye ataangukia mbali toka katika imani hii inayoamini katika mwili na damu ya Yesu. 
Wakati Sodoma na Gomora zilipoteketezwa kwa moto, wakwe za Lutu walilichukulia Neno la Mungu la uzima ambalo Lutu aliwaambia kuwa ni kitu cha mzaha. Kwa kuwa wale wasiolichukulia Neno la Mungu kwa umakini, hukumu ya Mungu itakuja juu yao kama ambavyo imeandikwa. Wasioamini watahukumiwa kwa dhambi yao ya kutoamini. Wataharibiwa kwa dhambi zao. Hili si jambo la kuchekesha linaweza kupitwa au kurukwa kwa hila chache. 
Injili ya maji na Roho inazungumzia juu ya imani katika mwili na damu ya Yesu. Ni kwa kuamini katika ukweli huu ndipo tumeweza kuondolewa dhambi zetu na kupokea uzima wa milele. Kwa sababu imani ya mwili na damu ya Yesu ambayo tunaiamini ni injili ya kweli na ukweli halisi, basi ni lazima tuitunze imani hii katika mioyo yetu. Ni lazima tuitunze imani hii kwa kuuinua ukingo wa imani katika mioyo yetu, ni lazima tulishikilie vilivyo Neno lote la Mungu na tusiliruhusu liteleze toka kwetu. Ni lazima tuukubali ukweli kuwa Mungu ameyatoweshea mbali maovu yote ya wenye dhambi kwa mwili na damu ya Yesu kwa kuamini hivyo katika mioyo yetu. 
Ninatumaini na kuomba kuwa ninyi nyote mtaamini katika injili ya maji na Roho iliyotimizwa na Bwana, mtaula mkate wa wokovu unaowaokoa ninyi toka katika dhambi zenu na kisha kupokea uzima wa milele.