Search

Mahubiri

Somo la 9: Warumi (Maoni juu ya Kitabu cha Warumi)

[SURA YA 13] Ishi Kwa Ajili ya Haki ya Mungu 

Warumi 13:1 inasema, “Kila mtu na aitii mamlaka iliyo kuu; kwa maana hakuna mamlaka isiyotoka kwa Mungu; na ile iliyopo imeamriwa na Mungu.”
Ni lazima tuishi katika mipaka ya desturi za kijamii. Mungu alituamuru kuwaogopa na kuwaheshimu wale walio na mamlaka katika maisha yetu yote ya kimwili na kiroho. Mungu anatoa mamlaka kwa maofisa wa serikali kwa sababu maalumu na kwa hiyo hatupaswi kuwadharau. Ni lazima tuukumbuke msemo wa Paulo akisema, “Msiwiwe na mtu cho chote isipokuwa kupendana” (Warumi 13:8).
Hii ndiyo sababu tumekuwa tukichapisha vitabu vya bure na kuitoa injili hii nzuri kwa watu wote katika ulimwengu mzima. 
Bwana alisema, “Upendo ni utimilifu wa sheria.” Watu wamejazwa na dhana potofu kuwa wanaitunza na kuishikilia sheria kikamilifu katika maisha yao ya kidini. 
Mungu alitupatia sisi injili ya maji na Roho ambayo inaifunua haki yake ili kutuokoa toka katika dhambi. Tunahitaji kuamini katika haki ya Mungu inayoonyeshwa katika injili ya maji na Roho. 
Kuieneza injili hii nzuri ambayo Bwana wetu ametupatia ni sawa na kutoa maisha au uhai kwa wengine kwa sababu injili hii inawaokoa watu toka katika dhambi zao zote. Hatupaswi kuwiwa deni lolote zaidi ya deni la upendo linalopokelewa kwa upendo wa Yesu Kristo. 
 

Sasa ni Wakati Wetu wa Kuamka 
 
Aya ya 11 inasema, “Naam, tukiujua wakati, kwamba saa ya kuamka katika usingizi imekwisha kuwadia; kwa maana sasa wokovu wetu u karibu nasi kuliko tulipoanza kuamini.” Sisi tutatawala pamoja na Kristo kwa miaka elfu moja wakati miili yetu ya udhaifu itakapobadilishwa—ambayo ni sawa na kusema kuwa wakati miili yetu itakapokuwa imekombolewa pia. 
Tunaweza kuona kufanana kati ya kizazi chetu na kizazi cha Nuhu. Wimbi jipya la ushoga limechanua sana katika vyuo vikuu. Ulimwengu huu ni wa uovu sana kiasi kuwa mtu mmoja anamchoma mtu mwingine na kumuua kwa kutumia simu kwa muda mrefu. Ukatili na maovu mengi ya jinsi hiyo yanatokea sana katika kizazi hiki. 
Ni lazima tutambue kuwa sasa ni wakati wetu wa kuamka. Wakati wa kuja kwa Bwana wetu mara ya pili umekaribia sana. Ni lazima tuwe makini ili tuweze kutanabaisha jinsi nyakati hizi zilivyo na kutambua kuwa kuja kwa Bwana wetu mara ya pili kumekaribia. Lakini kwa wakati huo huo ni lazima utambue kuwa kuna watu wengi sana ambao bado hawajui lolote kuhusu nyakati hizi. 
“Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu” (Mathayo 24:37). Hata katika kipindi cha Nuhu watu walijenga nyumba, walioa na kuoana, walifanya kila aina ya dhambi, na waliendelea kufanya shughuli zao za kila siku hadi siku moja wakati hukumu ya Mungu ilipomwagwa juu yao kwa ghafla. Zaidi ya Nuhu hakuna yeyote aliyekuwa akitegemea kuja kwa mvua kubwa na gharika ambayo iliwamaliza wote isipokuwa wachache waliopata kimbilio katika safina. Wale walioangamia walikutana na hukumu ya Mungu ya kutisha na kuangamiza hali wakiwa bado wanaendelea kula na kunywa kwa uhuru pasipokuwa na matarajio yoyote. 
Ulimwengu huu upo wazi si kwa hatari za vita tu bali pia hata kwa majanga ya asili ya kutisha ambayo yanatokea katika ulimwengu mzima yakiambatana na mabadiliko ya hali ya hewa. Kuna hatari kubwa ambayo imo hata katika vyakula tunavyokula kiasi kuwa hatuwezi hata kuvifurahia vyakula vyetu kwa kuwa tunavihofia. Hii ndiyo sababu inatupasa tuishi kwa busara katika nyakati hizi hali tukikumbuka kuwa wokovu wa miili yetu upo karibu sana kuliko wakati tulipoanza kuamini. 
 

Je, Umejivika Wokovu wa Kristo? 
 
Unaweza kufikiria kuwa maangamizi ya ulimwengu huu hayana lolote kuhusiana na suala la kiimani, na kwamba maangamizi hayo yanahusiana zaidi ya masuala ya kisiasa na kiuchumi. Lakini ukweli ni kuwa machafuko katika ulimwengu mzima yanatoa onyo juu ya maangamizi ya ulimwengu. Ulimwengu huu unakaribia kukutana na magumu sana ya kiuchumi na kimazingira. Biblia inatueleza kuwa kadri kuja kwa Bwana wetu mara ya pili kunavyozidi kukaribia, basi ni lazima sisi “tusiwiwe chochote isipokuwa kupendana” —tukisaidiana, tukilindana, tukiongozana, na tukishirikiana sisi kwa sisi kwa upendo. Na ni lazima tutambue kuwa matumaini yetu yapo karibu sana kuliko tulipoanza kuamini. 
Sisi tunaishi katika kipindi ambacho tunahitaji kuishi kwa matumini hali tukisubiri kurudi kwa Yesu Kristo. 
Je, tumaini letu lipo wapi? Tumaini letu linapatikana katika kusubiri kurudi kwa Kristo ambaye atatufufua sisi na kutupatia zawadi ya kutawala pamoja naye katika Ufalme wa Milenia hali ukitanguliwa na miaka saba ya Mapigo Makuu. Kadri wakati unavyozidi kukaribia basi inatupasa sisi kuendelea kuishi kwa tumaini hali tukiwa na haki ya Kristo. Ni lazima tusimame imara zaidi na zaidi katika injili ya maji na Roho na kisha kuitumikia kwa mioyo yetu yote. Ni lazima tuipanue huduma yetu ili tuweze kuishirikisha injili kwa kila nafsi katika ulimwengu mzima. 
 

Ni Lazima Tusiwiwe Chochote Zaidi ya Kupendana 
 
Ninafahamu kuwa kutakuwa na mateso mengi kutokana na majanga ya asili kama vile volikeno na matetemeko ya nchi. Siku hizi kuna mikanda mingi ya filamu inatengenezwa ikiwa imebeba ujumbe unaohusiana na maangamizi ya dunia. Ninafikiri kuwa pengine ulimwengu unaweza kubadilika kama ambavyo waandishi wa Hollywood wanavyodhania, na huu ni uthibitisho wa jinsi watu wanavyojihisi kuhusiana na maangamizi yajayo ya ulimwengu. 
Kwa hiyo, tusijihangaishe sana kwa kazi za matendo ya mwili bali tujihangaishe na matendo ya Roho. 
Ni lazima tuamini kuwa maisha ya kuishi hali tukiieneza injili ya maji na Roho ndiyo maisha bora zaidi. Watu wengi katika ulimwengu mzima wanashangazwa sana na huduma yetu. Watu wengi wasio na hesabu wametuambia jinsi ambavyo wamepata changamoto kutokana na huduma yetu. Wengi wao bado hawaamini jinsi ambavyo sisi kama kikundi kidogo cha watumishi wa Mungu toka katika nchi ndogo ya Korea tunavyoweza kuieneza haki ya Mungu kwa nguvu kiasi hicho. Ni kweli, sisi ni kikundi kidogo na dhaifu lakini bado tunaieneza injili katika ulimwengu mzima kwa sababu tunaamini katika injili ya maji na Roho ambayo imo katika haki ya Mungu. 
Warumi sura ya 14:8 inasema, “Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana.” Pia katika aya zilizotangulia Paulo alisema, “Hakuna kati yetu anayeishi kwa ajili yake mwenyewe, na hakuna anayekufa kwa ajili yake mwenyewe.” Sisi tunaishi kwa sababu ya Bwana wetu. 
Kwa kuwa tulizaliwa na Bwana wetu katika ulimwengu huu kwa haki yake, basi sisi ni wa Kristo tukiwa hai ama tukiwa tumekufa. Tutaishi na kuuacha ulimwengu huu kama ambavyo Kristo aliyaishi maisha yetu kwa haki ya Mungu. Mungu anaridhishwa nasi na ametuchagua kututumia sisi kama vyombo katika kuzieneza habari za furaha katika ulimwengu mzima. Hivyo Mungu ameufungua mlango ule mkuu wa uinjilisti kwa ajili yetu. Ameturuhusu kuieneza injili kwa kupitia vitabu bila kuhitajika kwenda katika kila taifa kwa miguu. 
Mfululizo wa vitabu vilivyo na injili ya haki ya Mungu vimetafsiriwa na kupelekwa katika ulimwengu unaozungumza Kiingereza, katika nchi zinazozungumza Kihispania, na pia katika kila nchi katika Asia, Afrika, na Ulaya. Nina hakika kuwa mfululizo huu mpya wa vitabu vinavyoitwa Bwana Wetu Anayefanyika Kuwa Haki ya Mungu vitatoa baraka kuu za kiroho kwa kila nafsi katika ulimwengu. Ni jambo la kushangaza jinsi Mungu anavyotenda ili kuyakamilisha mapenzi yake kwa kupitia waamini katika haki yake. 
Muda si mrefu ulimwengu utafunikwa na injili nzuri, na mara baada ya injili hii ambayo ina haki ya Mungu itakapokuwa imeenezwa katika ulimwengu mzima, basi hapo ndipo Mungu atakapoutimiza kila mpango ambao ameuhifadhi kwa ajili yetu. 
Kipindi hiki kipo katika mwisho wa pepo za dhoruba. Matatizo ya mafuta na wasiwasi wa kidunia kuhusiana na masuala ya kifedha yanaweza kuipiga dunia mara nyingine tena. Tunapaswa kuwa waaminifu zaidi katika kile ambacho Mungu ametukabidhi kukifanya. Ni lazima tuieneze injili ya maji na Roho hadi mwisho wa ulimwengu huu utakapowadia. Hebu tuieneze injili ya maji na Roho kwa juhudi ili kwamba asiwepo mtu katika ulimwengu huu ambaye hajaisikia injili hii. Ni lazima tushirikiane na kufanya kazi kwa dhumuni moja. Ni lazima tufanye kazi kama walivyofanya wale mashujaa mia tatu wa Gidioni. Ingawa idadi yetu ni ndogo, sisi tu askari mashujaa wa Mbinguni na Mungu yupo pamoja nasi. 
Yeyote anayeupokea msamaha wa dhambi na ana shukrani kwa Mungu anaweza kustahili katika kuieneza haki ya Mungu. Sisi tutakuwa washindi kwa imani kwa sababu tunayo haki ya Mungu. Wale wanaoamini katika haki hii ya Mungu mara nyingi siku zote wanayatafuta matendo ya Roho na wanayaweka malengo yao katika matendo ya kiroho. 
Ninaomba kwamba haki ya Mungu iwe juu yako.