Search

Mahubiri

Somo la 10: Ufunuo (Ufafanuzi juu ya Ufunuo)

[2-6] Barua Kwa Kanisa la Pergamo (Ufunuo 2:12-17)

(Ufunuo 2:12-17)
“Na kwa malaika wa kanisa lililoko Pergamo andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye na huo upanga mkali, wenye makali kuwili. Napajua ukaapo, ndipo penye kiti cha enzi cha Shetani; nawe walishika sana jina langu, wala hukuikana imani yangu, hata katika siku za Antipa shahidi wangu, mwaminifu wangu, aliyeuawa kati yenu hapo akaapo Shetani. Lakini ninayo maneno machache juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini. Vivyo hivyo wewe nawe unao watu wayashikao mafundisho ya Wanikolai vile vile. Basi tubu; na usipotubu, naja kwako upesi, nami nitafanya vita juu yao kwa huo upanga wa kinywa changu. Yeye aliye na sikio na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye nitampa baadhi ya ile mana iliyofichwa, nami nitampa jiwe jeupe, na juu ya jiwe hilo limeandikwa jina jipya asilolijua mtu ila yeye anayelipokea. ”
 

Mafafanuzi
 
Aya ya 12: “Na kwa malaika wa kanisa lililoko Pergamo andika; Haya ndiyo anenayo yeye aliye na huo upanga mkali, wenye makali kuwili”
Pergamo ulikuwa ni mji mkuu wa wa kiutawala katika Asia Ndogo ambapo wakazi wake waliiabudu miungu mingi ya kipagani. Mji huu ulikuwa hasa ndio makao makuu ya kumwabudu mfalme. Kule kusema “Yeye aliye na huo upanga mkali, wenye makali kuwili,” kuna maanisha kuwa Bwana anapigana na maadui wa Mungu. 
 
Aya ya 13: “Napajua ukaapo, ndipo penye kiti cha enzi cha Shetani; nawe walishika sana jina langu, wala hukuikana imani yangu, hata katika siku za Antipa shahidi wangu, mwaminifu wangu, aliyeuawa kati yenu hapo akaapo Shetani.”
Pamoja na kuwa Pergamo ilikuwa ndio ngome kuu ya kumwabudu mfalme, pia ilikuwa ni mahali ambapo mtumishi wa Mungu aliyeitwa Antipa aliuawa na kuifia-dini kwa kukataa kumwabudu mfalme na kwa kuitetea imani yake kwa Bwana. Wakati utafika tena ambapo watu watashurutishwa kumwabudu Mpinga Kristo, lakini watakatifu na watumishi wa Mungu watailinda imani yao hadi mwisho kama vile Antipa alivyoilinda imani yake kwa kuutoa uhai wake. Ili kuwa na imani imara kama hiyo, basi tunapaswa kuanza kuiweka imani yetu katika matendo hata kama tukianza kwa hatua chache. Wakati wa mateso utakapowadia, watakatifu na watumishi wa Mungu ni lazima wamtegemee Roho Mtakatifu. Ni lazima watumishi hao wa Mungu wamtegemee Mungu na wawe tayari kukubali kuuawa na kuifia-dini hali wakiwa na tumaini ili kwamba waweze kumpatia Mungu utukufu na kisha kuipokea Mbingu na Nchi Mpya toka kwa Mungu.
 
Aya ya 14: “Lakini ninayo maneno machache juu yako, kwa kuwa unao huko watu washikao mafundisho ya Balaamu, yeye aliyemfundisha Balaki atie ukwazo mbele ya Waisraeli kwamba wavile vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na kuzini.”
Mungu alilikemea Kanisa la Pergamo kwa sababu baadhi ya wanachama wake walikuwa wakilishikilia fundisho la imani la Balaamu. Balaamu alikuwa ni nabii wa uongo aliyewaongoza Waisraeli kwenda mbali na Mungu na aliwafanya watende dhambi ya kuabudu miungu mingine na kwa kuwafanya Waisraeli wajaribiwe kufanya zinaa na makuhani wa kike wa Wamataifa waliokuwa wakiabudu miungu. Mungu aliwakemea wale ambao imani zao zilikuwa zimemwacha Mungu. Mioyo ya watu ilikuwa imemwacha Mungu na badala yake ilikuwa ikiiabudu miungu ya uongo. Dhambi ya kuabudu miungu mingine ni dhambi kubwa sana mbele za Mungu. 
 
Aya ya 15: “Vivyo hivyo wewe nawe unao watu wayashikao mafundisho ya Wanikolai vile vile.”
Kimsingi, maneno “Wanikolai” na “Balaamu” katika Biblia yanawiana, yakimaanisha “wale wanaowashawishi watu.” Wakati Mungu aliposema kuwa “kuna wale wayashikao mafundisho ya Wanikolai,” hii ilimaanisha kuwa kanisa la Mungu ni lazima liwakatae “wale wanaoyashikilia mafundisho ya Balaam.” Wale walioyafuata mafundisho ya Wanikolai na Balaamu pia walikuwa ndio waliotafuta kupata mali na kuabudu miungu. Kwa kweli watu wa jinsi hiyo ni lazima waondolewe nje ya kanisa la Mungu. 
 
Aya ya 16: “Basi tubu; na usipotubu, naja kwako upesi, nami nitafanya vita juu yao kwa huo upanga wa kinywa changu.”
Hivyo Mungu aliliambia Kanisa la Pergamo kuacha kuabudu miungu ya uongo na kufuatilia vitu vya kidunia na kurudi katika imani sahihi, na akawaaonya kuwa kama wasipotubu Mungu atafanya vita kwa upanga ulio katika kinywa chake. Kwa maneno mengine, hii ni lugha kali ambayo kwa hiyo alionya kuwa atawaadhibu wale ambao hawatubu na kuyaacha mafundisho ya Balaamu hata kama walikuwa ni waamini. Wale wote waliolisikia onyo hili la Mungu na kumrudia watahifadhiwa hai, kimwili na kiroho, lakini wale ambao hawakufanya hivyo walikuwa wakiyaita maangamizi yao wenyewe ya kimwili na kiroho. Ili kwamba watakatifu na watumishi wa Mungu waweze kubarikiwa katika dunia hii na baadaye, ni lazima walisikie Neno la Mungu na kumfuata Bwana kwa imani zao.
 
Verse 17: “Yeye aliye na sikio na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye ashindaye nitampa baadhi ya ile mana iliyofichwa, nami nitampa jiwe jeupe, na juu ya jiwe hilo limeandikwa jina jipya asilolijua mtu ila yeye anayelipokea.”
Watakatifu wa kweli watakubaliana na kuuawa kwa ajili ya kuifia-dini. Mungu anatueleza kuwa kwa wale ambao watauawa na kuifia-dini kwa ajili ya jina lake, basi Mungu atawapatia chakula cha Mbinguni na kuyaandika majina yao katika Ufalme wake. Ili sisi tuweze kuishi kimwili na kiroho, basi tunapaswa kusikiliza yale ambayo Roho Mtakatifu ameyaongea kwa Kanisa la Mungu. Kwa wale watakaoshinda—yaani wale watakaoshinda vita dhidi ya wafuasi wa Shetani—Mungu atawapatia haki ya imani inayowakomboa toka katika dhambi, na kwa ajili ya imani yao, Mungu atayaandika majina yao katika Kitabu cha Uzima.
Biblia inatueleza tena na tena katika vifungu mbalimbali vya maandiko kuwa wale watakaovumilia hadi mwisho watapokea wokovu. Kwa maneno mengine, watakatifu wanahitaji kuwa wavumilivu katika nyakati za mwisho ili kwamba waweze kuilinda imani yao katika injili ya maji na Roho. Majina ya waliozaliwa tena upya yanaandikwa katika Kitabu cha Uzima. Hivyo, waamini ni lazima waingie katika Ufalme wa Mungu si kwa kufuata mali au faida za kidunia bali kwa kushinda kwa imani hadi siku ile ambapo hatimaye watasimama mbele za Mungu.