Search

Mahubiri

Somo la 9: Warumi (Maoni juu ya Kitabu cha Warumi)

[SURA YA 7-2] Kiini cha Imani ya Paulo: Ungana na Kristo Baada ya Kuifia Dhambi (Warumi 7:1-4)

(Warumi 7:1-4)
“Ndugu zangu, hamjui (maana nasema na hao waijuao sheria) ya kuwa torati humtawala mtu wakati anapokuwa yu hai? Kwa maana mwanamke aliye na mume amefungwa na sheria kwa yule mume wakati anapokuwa yu hai; bali akifa yule mume, amefunguliwa ile sheria ya mume. Basi wakati awapo hai mumewe, kama akiwa na mume mwingine huitwa mzinzi. Ila mumewe akifa, amekuwa huru, hafungwi na sheria hiyo, hata yeye si mzinzi, ajapoolewa na mume mwingine. Kadhalika, ndugu zangu, ninyi pia mmeifia torati, kwa njia ya mwili wa Kristo, mpate kuwa mali ya mwingine, tumzalie Mungu matunda.”
 

Je, umewahi kuona bunda la nyuzi zilizojisokota? Ikiwa unajaribu kuifahamu sura hii pasipo kuufahamu ukweli wa ubatizo wa Yesu ambao Mtume Paulo aliuamini, basi ni hakika kuwa imani yako itakuwa katika wakati mgumu kuliko hapo kabla. 
Katika sura hii Paulo anasema kwa kuwa kila mtu ni mwenye dhambi mbele ya Sheria ya Mungu, basi mtu anaweza kwenda kwa Yesu Kristo na kisha kuzaliwa upya baada ya kuwa amekufa kifo cha kiroho. 
 

Ukweli Ambao Paulo Alikuja Kuutambua
 
Warumi 7:7 inasema, “Tusemeje, basi? Torati ni dhambi? Hasha! Walakini singalitambua dhambi ila kwa sheria.” Paulo anaendelea, “kwa kuwa singalijua kutamani, kama torati isingalisema, Usitamani.” Tena anaongezea zaidi, “Lakini dhambi ilipata nafasi kwa ile amri, ikafanya ndani yangu kila namna ya kutamani.” Paulo alitambua kuwa amekuwa akizikosea amri zote 613 za Mungu. Kwa maneno mengine, yeye hakuwa lolote zaidi ya kuwa lundo la dhambi ambaye hakuweza kufanya lolote zaidi ya kuendelea kutenda dhambi, hii ni kwa sababu yeye alikuwa ni uzao wa mwanadamu wa kwanza Adamu na kwamba alikuwa ameingizwa katika dhambi na alikuwa ametungwa mimba katika dhambi. 
Kila mtu aliyezaliwa katika ulimwengu huu anatenda dhambi tangu wakati ule anapozaliwa hadi kifo. Na kwa sababu hiyo wanadamu hawawezi kuzitunza na kuzifuata sheria na amri za Mungu. Inawezekanaje kwa malundo haya ya dhambi kuweza kuzifuata amri zote 613 na sheria ya Mungu? Ni pale tu tunapojitambua kuwa sisi ni wenye dhambi mbele ya Sheria ya Mungu ndipo tunapoweza kwenda mbele za Yesu Kristo, ambaye ni haki ya Mungu, na hapo ndipo tunapoweza hatimaye kutambua kuwa tunaweza kukombolewa toka katika dhambi zetu kwa kupitia Kristo Yesu. Yesu Kristo amefanyika kuwa haki ya Mungu. Yesu ametuletea hii haki ya Mungu kwa kupitia ubatizo wake toka kwa Yohana na damu yake Msalabani. Kwa hiyo ni lazima sisi sote tufahamu na kuamini katika haki ya Mungu. Sababu ambayo inatufanya tumwamini Yesu ni kwa sababu hii haki ya Mungu inapatikana ndani yake. 
Je, unafahamu na kuamini katika haki ya Mungu? Haki ya Mungu ni siri ambayo imefichwa katika injili ya maji na Roho. Siri hii inajumuishwa katika ubatizo ambao Yesu aliupokea toka kwa Yohana katika Mto Yordani. Je, unapenda kuifahamu siri hii? Ikiwa unapenda kuamini katika ukweli huu, basi utaipata haki ya Mungu kwa kupitia imani yako. 
Kabla hatujafahamu kuhusu Sheria ya Mungu na amri zake ilionekana kana kwamba hatukuwa ni wenye dhambi pamoja na kuwa tulikuwa tukitenda dhambi kila siku. Lakini baada ya kuanza kuhudhuria kanisani tulifikia hatua ya kutambua kuwa tulikuwa ni wenye dhambi sana na kwamba tungekifikia kifo cha kiroho kwa sababu ya dhambi zilizokuwa ndani yetu. Kwa hiyo, ili kuweze kuziongoza nafsi kwenda kwa Yesu Kristo, Mtume Paulo alizitazama siku zake za zamani wakati alipokuwa akiielewa vibaya Sheria ya Mungu na amri zake. 
Hapa kuna mfano ambao utakusaidia ili uweze kuifahamu kazi ya Sheria ya Mungu. Sasa nimeishikilia Biblia. Ikiwa nitakificha kitu fulani cha muhimu katika kurasa hizi za Biblia hali nikisema, “Usijaribu kamwe kuangalia ndani ya kitabu hiki ili kuona kilichofichwa ndani yake,” halafu nikaiacha Biblia hii hapa mezani kwa muda kidogo, je, utafanyaje? Ukweli ni kuwa mara utakapoyasikia maneno yangu utapata hamu ya kutambua kile kilichofichwa katika Biblia na kama matokeo ya udadisi huu hatimaye utaivunja amri niliyokupa ya kutojaribu kuangalia ndani ya Biblia. Wakati utakapokuwa ukishangaa na kutaka kufahamu kilichomo katika Biblia ndio kipindi ambacho utaamua kwa dhati kujua kilicho ndani ya Biblia. Lakini kama nisinge kuamuru kuwa usiangalie ndani ya Biblia basi usingeweza kupatwa na jaribu la kuangalia ndani ya Biblia. Vivyo hivyo, wakati Mungu anapotuamuru, basi zile dhambi ambazo zilikuwa hazifahamiki ndani yetu zitajidhihirisha ndani yetu kulingana na matukio. 
Sheria ambayo Mungu alimpatia mwanadamu ina jukumu la kuifunua dhambi katika mioyo ya watu. Mungu hakutupatia sheria hiyo ili tuweze kuitunza na kuifuata; bali sisi tulipewa Sheria ili iweze kuzidhihirisha dhambi zetu na hivyo kutufanya sisi kuwa ni wenye dhambi. Sisi sote tutaangamia ikiwa hatutamwendea Yesu Kristo na kuiamini haki ya Mungu inayopatikana katika ubatizo wa Yesu alioupokea toka kwa Yohana na damu yake aliyoimwaga Msalabani. Ni lazima tukumbuke kuwa kazi ya Sheria ni kutuleta kwa Kristo na kutusaidia ili tuweze kuiamini haki ya Mungu kwa kupitia Kristo. 
Hii ndiyo sababu Mtume Paulo alishuhudia, “Lakini dhambi ilipata nafasi kwa ile amri, ikafanya ndani yangu kila namna ya kutamani.” (Warumi 7:8). Kwa kupitia Sheria ya Mungu Mtume Paulo alituonyesha juu ya misingi ya dhambi jinsi ilivyo. Paulo alikiri kuwa kimsingi yeye alikuwa ni mwenye dhambi, lakini alifikia hatua ya kupata uzima wa milele kwa kuamini katika haki ya Mungu iliyotolewa na Yesu Kristo. 
 

Maombolezo ya Paulo na Imani
 
Paulo alisema hivi, “Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti? Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” (Warumi 7:24-25).
Paulo aliukiri ule ukweli kuwa hata yeye ambaye alikuwa na haki ya Mungu bado aliendelea kutenda dhambi na kwamba katika hali hiyo haki ya Mungu ilihitajika zaidi na zaidi si tu kwa ajili yake bali na kwa ajili ya wanadamu wengine. 
Ni lazima tuipate haki ya Mungu kwa kuifahamu kiusahihi siri iliyofichwa katika ubatizo wa Yesu alioupokea na kisha kuuamini. Wewe na mimi tunapaswa kufahamu na kuamini katika haki ya Mungu inayopatikana katika ubatizo wa Kristo na damu yake Msalabani. Ni hapo tu ndipo nafsi zetu na miili yetu, ambayo haina chaguo jingine zaidi ya kuendelea kutenda dhambi itakapokombolewa toka katika dhambi zetu. Hatupaswi kuusahau ukweli kuwa ubatizo wa Kristo na damu yake Msalabani viliitimiza haki ya Mungu. 
Wale wasioifahamu haki ya Mungu wanaweza kubakia kuwa wenye dhambi hadi mwisho hata kama wakijaribu kiasi gani kuitunza na kuifuata Sheria. Ni lazima tutambue kuwa Sheria ya Mungu haikutolewa ili sisi tuweze kuitunza na kuifuata. Lakini washika sheria hawafahamu kuwa siri ya ukombozi ipo katika “ubatizo” ambao Yesu aliupokea pamoja na damu yake Msalabani. Kama matokeo ya kutokufahamu kwao wanaielewa vibaya Sheria ya Mungu hali wakifikiri kuwa walipewa sheria hiyo ili waitii na kwa sababu hiyo wanaendelea kuishi katika machafuko. Lakini ni lazima tuzitambue dhambi zetu kwa kupitia Sheria na kisha kuishi kwa imani yetu katika haki ya Mungu. Hatupaswi kuwa kinyume na hii haki ya Mungu na kisha kuzifuata haki zetu wenyewe. Bali tunapaswa kuishi katika haki ya Mungu iliyotimizwa kwa ubatizo wa Kristo na damu yake Msalabani. Kwa maneno mengine, tunahitaji kujifunza kumtolea Bwana shukrani, Bwana aliyeitimiza haki ya Mungu. 
Hii ndiyo sababu Paulo, hali akiungalia mwili wake binafsi, alilia na kusema, “Ole wangu, maskini mimi!” lakini bado alimtolea shukrani Mungu katika Yesu Kristo. Sababu iliyomfanya Paulo kufanya ukiri wa jinsi hii ni kwa sababu kadri alivyofanya dhambi zaidi, basi ndivyo ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani vilivyozidi kuikamilisha kikamilifu haki ya Mungu. Sisi pia tunaweza kupiga kelele kwa furaha na ushindi kwa sababu tumeokolewa kwa imani yetu katika Yesu Kristo hata pale ambapo tunaishi maisha magumu kati ya sheria na mwili na ile haki ya Mungu. Imani aliyokuwanayo Paulo ni ile iliyokuwa ikiamini katika ubatizo wa Yesu Kristo na damu yake Msalabani. Hivi ndivyo Paulo alivyoweza kuishi katika imani yake katika haki ya Mungu, na kutokana na kuamini katika haki hii ya Mungu, basi Paulo alifanyika kuwa mmoja wa wale wanaomtolea Mungu sifa. 
Katika Warumi sura ya 7 Paulo anazungumzia juu ya hali yake ya umaskini katika nyakati za kale hali akiilinganisha na imani yake ya sasa ya ushindi katika haki ya Mungu. Ushindi wa Paulo wa kiimani ulikuwa ni kwa sababu ya imani yake katika hii haki ya Mungu. 
“Ndugu zangu, hamjui (maana nasema na hao waijuao sheria) ya kuwa torati humtawala mtu wakati anapokuwa yu hai?” (Warumi 7:1).
Kilele cha sura ya 7 kinapatikana katika aya za 24 na 25. Paulo aliandika hivi, “Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti? Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.”
Katika Warumi sura ya 6, Paulo alizungumzia juu ya imani inayotuongoza sisi kuzikwa na kufufuka katika umoja na Kristo. Sisi tunaweza kuipata imani hii kwa kuungana na ubatizo wake na kifo chake Msalabani. 
Paulo alitambua kuwa alikuwa ni mtu maskini ambaye mwili wake ulikuwa na mapungufu mengi kiasi kuwa aliivunja Sheria ya Mungu sio tu kabla ya kukutana na Yesu bali aliendelea kuivunja sheria hiyo hata baada ya kuonana na Yesu. Ndio maana Paulo aliomboleza, “Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti?” Kisha akahitimisha kuwa anaweza kukombolewa toka katika mwili wa mauti kwa kuamini katika haki ya Mungu hali akisema, “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu” Paulo aliwekwa huru toka katika dhambi za mwili na mawazo kwa kuamini katika haki ya Mungu kwa kupitia Kristo na kwa kuungana naye. 
Ukiri wa mwisho wa Paulo ulikuwa ni, “Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.” (Warumi 7:25). Na mwanzoni mwa sura ya 8, Paulo alikiri kuwa, “Sasa, basi, hakuna hukumu ya adhabu juu yao walio katika Kristo Yesu. Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti” (Warumi 8:1-2). 
Kwa asili kulikuwa na sheria mbili zilizotolewa na Mungu: sheria ya dhambi na mauti na ile sheria ya Roho wa uzima. Sheria ya Roho wa uzima ilimuokoa Paulo toka katika sheria ya dhambi na mauti. Hii ilimaanisha kuwa kwa kuamini katika ubatizo wa Yesu na na kifo chake Msalabani, ambavyo vilichukulia mbali dhambi zake zote, Paulo aliungana na Yesu na kisha akaokolewa toka katika dhambi zake zote. Sisi sote ni lazima tuwe na imani inayotuunganisha na ubatizo wa wa Bwana na kifo chake Msalabani. 
Katika Warumi sura ya 7 Paulo alikiri kuwa hapo kabla alikuwa amepangiwa kuhukumiwa adhabu chini ya Sheria, lakini kwa kupitia Yesu Kristo aliweza kuokolewa toka katika adhabu yake hiyo. Kwa hiyo, Paulo aliweza kumtumikia Mungu kwa kupitia Roho Mtakatifu aliyekuwa akikaa ndani yake. 
 

Ukweli Ambao Paulo Aliutambua
 
Paulo alikiri, “Tusemeje, basi? Torati ni dhambi? Hasha! Walakini singalitambua dhambi ila kwa sheria.” (Warumi 7:7). Paulo asingalitambua kutamani ikiwa sheria isingalisema “Usitamani”. Hali akiuelezea uhusiano kati ya Sheria na dhambi Paulo alisema, “Lakini dhambi ilipata nafasi kwa ile amri, ikafanya ndani yangu kila namna ya kutamani.” Hii ina maanisha kuwa kimsingi mioyo ya wanadamu imejaa dhambi. Tangu wakati ule watu wanapotungwa mimba katika matumbo ya mama zao wanakuwa wametungwa mimba katika dhambi, na kwa hiyo watazaliwa na aina kumi na mbili za dhambi. 
Aina hizi kumi na mbili za dhambi ni uasherati, uzinzi, wizi, tamaa, uovu, uongo, ubaya, kijicho, machukizo, majivuno, na ujinga. Kila mtu anatenda dhambi hizi hadi atakapokufa. Inawezekanaje basi kila mtu duniani akaitii Sheria na amri za Mungu wakati yeye akiwa amezaliwa katika ulimwengu huu akiwa na aina kumi na mbili za dhambi? Mara tunapoyasikia maneno ya Sheria na amri zikitueleza yale tunayopaswa “kufanya” na yale “tusiyopaswa kuyafanya” basi dhambi inaanza kufanya kazi ndani yetu. 
Tulipokuwa hatuifahamu Sheria na amri za Mungu, dhambi zilizo ndani yetu zilikuwa zimelala kimya. Lakini baada ya kuzisikia amri zilizokuwa zikitueleza tunachopaswa kukifanya na kile tusichopaswa kukifanya, dhambi hizi zilijitokeza na zikatufanya tutende dhambi zaidi. 
Yeyote ambaye hajazaliwa tena upya au ambaye haamini na kuufahamu ukweli wa maji na Roho ana dhambi ndani yake. Basi baada ya kuwa zimeamshwa na amri, dhambi hizi zinazaa dhambi zaidi. Sheria ambayo inawaeleza watu wanachopaswa kukifanya au kile wasichopaswa kukifanya ni kama mkufunzi anayejaribu kuifuga dhambi. Hata hivyo, dhambi inakwenda kinyume na amri za Mungu na haitii maagizo ya Mungu. Wakati mwenye dhambi anapozisikia amri, basi zile dhambi zilizo ndani ya moyo wake zinaamshwa na zinamwongoza kutenda dhambi zaidi. 
Tunaweza kutambua kwa kupitia zile Amri Kumi kuwa tuna dhambi ndani yetu. Kwa hiyo kazi ya Sheria ni kuifunua dhambi ndani ya mioyo yetu, na kutufanya tutambue kuwa amri za Mungu ni takatifu na kisha kutuamsha sisi katika dhambi. Kimsingi, sisi tulizaliwa na tamaa na kuwa na uchoyo juu ya kila kitu ambacho Mungu amekiumba vikiwemo vitu vya kawaida au wapenzi ambao si wetu. Kwa hiyo, ile amri inayosema “Usitamani,” inatueleza sisi kuwa tulizaliwa tukiwa ni wenye dhambi na kwamba tulikuwa tumepangiwa kwenda kuzimu tangu siku ile tulipozaliwa. Pia inatuonyesha umuhimu wa Mwokozi ambaye ameitimiza haki ya Mungu. 
Hii ndiyo sababu Paulo alikiri kuwa dhambi ilipata nafasi kwa ile amri kisha ikazaa kila namna ya tamaa mbaya. Paulo alitambua kuwa alikuwa ni mwenye dhambi mkubwa aliyekuwa akizivunja amri za Mungu kwa kuwa alikuwa amezaliwa akiwa na asili ya dhambi na kwamba kabla ya kuamini katika haki ya Mungu alikuwa ni mwenye dhambi. 
Tunapoitazama sura ya 7 tunaona kuwa Mtume Paulo alikuwa ni mtu wa kiroho sana, alikuwa na ufahamu mpana wa Biblia, na alikuwa na uzoefu na uelewa mkubwa sana wa mambo ya kiroho. Paulo alitambua wazi kuwa kwa kupitia Sheria kulikuwa na dhambi ndani yake ambayo kwa hiyo zile amri ziliamsha kila namna ya tamaa mbaya. Alitambua kuwa Sheria ya Mungu ilikuwa na kazi ya kuzifunua dhambi ndani yake. Na kadri dhambi hizi zilivyoamshwa, basi Paulo alikiri kuwa ile amri ambayo ilipaswa kumletea uzima pia ilimletea mauti. 
Je, imani yako ikoje? Je, imani yako iko kama ya Paulo? Hata kama unamwamini Yesu au la, Je, kuna dhambi ndani ya moyo wako? Ikiwa ni hivyo, basi ina maanisha kuwa bado hauifahamu haki ya Mungu, hujampokea Roho Mtakatifu, na kuwa wewe ni mwenye dhambi ulipangiwa kwenda kuzimu ili kuhukumiwa kwa dhambi zako binafsi. Je, unakubaliana na ukweli huu? Ikiwa unakubaliana, basi amini katika injili ya maji na Roho ambamo haki ya Mungu imefunuliwa. Utaokolewa toka katika dhambi zako zote, utaipata haki ya Mungu, na kisha utampata Roho Mtakatifu juu yako. Ni lazima tuamini katika injili ya maji na Roho. 
 

Dhambi, Hali Ikipata Nafasi Kwa ile Amri Ilimdanganya Paulo
 
Mtume Paulo alisema, “Nikaona ile amri iletayo uzima ya kuwa kwangu mimi ilileta mauti. Kwa maana dhambi, kwa kupata nafasi kwa ile amri, ilinidanganya, na kwa hiyo ikaniua” (Warumi 7:10-11). Kwa maneno mengine, dhambi ilimdanganya Paulo kwa kupata nafasi katika amri. Paulo aliamini katika amri ambayo ilikuwa kwa kweli ni nzuri na ya haki, lakini aina kumi na mbili za dhambi zilikuwa hai na zikizidi kuwa mbaya zaidi ndani ya moyo wake. Hii ilimaanisha kuwa Paulo alikuwa amedanganywa na dhambi kwa sababu alikuwa hafahamu dhumuni la amri za Mungu. 
Mara ya kwanza, Paulo alifikiri kuwa Mungu alimpatia amri ili aweze kuitunza na kuifuata. Lakini baadaye alitambua kuwa Sheria haikutolewa ili iheshimiwe bali kwa ajili ya kuzifunua dhambi ndani ya mioyo ya watu; pia hali ikiambatana na utakatifu wa Mungu sheria iliwalenga wasioamini ili waweze kuhukumiwa na Mungu. Hii ndiyo sababu Paulo alifikiri kuwa alikuwa amedanganywa na dhambi kwa kuwa alikuwa hajazifahamu amri za Mungu na Sheria yake kwa usahihi. Siku hizi kuna watu wengi ambao nao wanadanganywa kwa jinsi hii. 
Ni lazima tutambue kuwa sababu iliyomfanya Mungu akatupatia amri na Sheria haikuwa kwa dhumuni la sisi kuitii bali ili tuweze kuzitambua dhambi zetu binafsi na kisha kuifikia haki ya Mungu kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. Lakini kwa kuwa tunajaribu kuishi kwa mujibu wa Sheria kwa miili yetu basi tunajikuta tukiishia kuifunua asili yetu ya dhambi. 
Kwa hiyo, mwenye dhambi anatambua kwa kupitia Sheria kuwa hata kama Sheria ni takatifu, yeye hana nguvu yoyote au uwezo wowote wa kuishi maisha matakatifu. Kwa wakati huo, mtu huyo anakuwa ni mwenye dhambi ambaye hana chaguo zaidi ya kupelekwa kuzimu na ile Sheria. Lakini wenye dhambi ambao hawaamini katika injili ya maji na Roho wanaendelea kufikiri kuwa Mungu aliwapatia Sheria ili waitii. Wao wanaendelea kujaribu kuitii Sheria, lakini ukweli ni kuwa watajidanganya wao wenyewe na hatimaye kuangukia katika maangamizi. 
Wale ambao hawajazaliwa tena upya kwa kubakia pasipo ufahamu wa haki ya Mungu wanatenda dhambi na kisha wanajaribu kusamehewa kwa kutoa sala za toba. Hata hivyo, mwishoni wanafikia hatua ya kutambua kuwa walilielewa vibaya dhumuni la Sheria ya Mungu na kwamba walijidanganya wao wenyewe. Dhambi, hali ikichukua nafasi kwa ile amri iliwadanganya wao. Sheria ya Mungu ni takatifu, lakini dhambi zilizo ndani yao zinawaongoza wao kwenda katika mauti. 
Paulo alisema, “Basi torati ni takatifu, na ile amri ni takatifu, na ya haki, na njema. Basi je! Ile iliyo njema ilikuwa mauti kwangu mimi? Hasha! Bali dhambi, ili ionekane kuwa ni dhambi hasa, ilifanya mauti ndani yangu kwa njia ya ile njema, kusudi kwa ile amri dhambi izidi kuwa mbaya mno” (Warumi 7:12-13). Wale wanaoufahamu ukweli huu wanatambua hitaji lao la haki ya Mungu na wanaamini kuwa injili ya maji na Roho ndiyo ukweli halisi. Mtu anayeamini katika injili ya maji na Roho pia anaamini katika haki ya Mungu. Hebu tukombolewe toka katika dhambi zetu zote na kisha tuufikie utakatifu wa Mungu kwa kuamini katika haki yake. Ninapenda ninyi nyote muweze kubarikiwa na injili hii. 
 

Je, Mwili na Mawazo ya Paulo Vilikuwaje? 
 
Paulo alikuwa amejawa na Roho na alikuwa na uelewa wa kina wa Neno la Mungu. Aliuzungumzia mwili wake kwa maneno yafuatayo: “Kwa maana twajua ya kuwa torati asili yake ni ya rohoni; bali mimi ni mtu wa mwilini, nimeuzwa chini ya dhambi. Maana sijui nifanyalo, kwa sababu lile nilipendalo, silitendi; bali lile nilichukialo ndilo ninalolitenda. Lakini kama nikilitenda lile nisilolipenda, naikiri ile sheria ya kuwa ni njema. Basi sasa si mimi nafsi yangu ninayetenda hilo, bali ni ile dhambi ikaayo ndani yangu” (Warumi 7:14-17). Paulo alisema kuwa alitenda dhambi kwa kuwa kwa asili yeye alikuwa ni mtu wa mwilini. Na kwa kuwa alikuwa ni wa mwilini, alijikuta yeye mwenyewe akizifuata tamaa za mwili hata pale alipokuwa akitamani kutenda mema. 
Hivyo Paulo alitambua kuwa, “Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kufanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu” (Warumi 7:22-23). Hii ndiyo sababu Paulo aliomboleza juu ya mwili wake hali akilia, “Ole wangu, maskini mimi!” (Warumi 7:24). Hata baada ya Paulo kuzaliwa tena mara ya pili bado aliendelea kujisikia vibaya kwa kuwa kulikuwa na maovu ndani yake ijapokuwa yeye alipenda kutenda mema. Wakati Paulo aliposema kuwa maovu yalikuwa ndani yake alikuwa akizungumzia juu ya mwili wake. Yeye aliiona sheria nyingine katika viungo vyake ikiwa inapigana vita na ile sheria ya Roho na hali ikimfanya yeye kuwa mateka wa mwili na kisha ikamuongoza katika kutenda dhambi. Paulo aliweza kukiri kuwa alikuwa hana chaguo zaidi ya kuikubali hukumu kwa vile aliuona mwili wake ukimuongoza katika kutenda dhambi. Kwa kuwa Paulo alikuwa na mwili basi ndio maana aliomboleza juu ya dhambi iliyokuwa ikiinuka toka katika mwili wake. 
Hii ndiyo sababu Paulo alitangaza akisema, “Ole wangu, maskini mimi!” Lakini pia alimshukuru Yesu Kristo kwa kuitimiza haki ya Mungu. Hii ni kwa kuwa Paulo aliamini kuwa Yesu alikuja hapa duniani, alibatizwa na akasulubiwa ili kutoa msamaha wa dhambi kwa wanadamu wote. Hivyo Paulo aliweza kumshukuru Mungu kwa moyo kwa kuwa alikuwa na imani iliyokuwa ikimuunganisha yeye na ubatizo na damu ya Yesu Kristo. 
Paulo alifahamu kuwa wakati Yohana alipombatiza Yesu, dhambi zake zote pamoja na dhambi za ulimwengu wote zilipitishwa kwa Yesu mara moja na kwa ajili ya wote. Pia alitambua kuwa wakati Yesu alipokufa Msalabani, sisi sote pia tuliifia dhambi pamoja na Kristo. Hivyo ni lazima tuwe na imani moja yenye ukweli wa maji na Roho. Je, moyo wako umeunganishwa pamoja na ubatizo na damu ya Yesu Kristo? Kwa maneno mengine, Je, umeuunganisha moyo wako na injili ya maji na Roho ambayo imeitimiza haki ya Mungu? Ni lazima tuwe na imani inayoungana na ule ubatizo ambao Bwana wetu aliupokea toka kwa Yohana na damu yake aliyoimwaga Msalabani. Ni muhimu sana kwetu kuwa na imani yenye muunganiko huu kwa sababu kule kuungana na injili ya maji na Roho ni kuungana na haki ya Mungu. 
Warumi 6:3 inasema, “Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake?” Hii ina maanisha kuwa kwa kuamini katika ubatizo wa Yesu basi sisi sote tumebatizwa pamoja naye, maana yake ni kuwa sisi sote tumeunganishwa pamoja na kifo cha Bwana wetu. Hii ni sawa na kusema kuwa kwa kubatizwa na kuungana kwa kupitia imani, basi sisi tulibatizwa kiroho na kukishiriki kifo chake. Kuunganishwa na Bwana ni kuunganishwa katika ubatizo wake na kushiriki mauti pamoja naye. 
Hivyo ni lazima tuamini na kuungana pamoja na ubatizo wa Yesu na kifo chake Msalabani ambavyo vimeitimiza haki ya Mungu. Ikiwa huiamini injili ya maji na Roho, injili ambayo inaishikilia haki ya Mungu, basi wewe haujaungana pamoja na ubatizo na kifo cha Yesu. Na ni katika injili hii ndipo ambapo haki ya Mungu inafunuliwa. 
Ikiwa mioyo yetu haiungani na ubatizo wa Yesu na kifo chake Msalabani, basi kwa kweli imani yetu ni kama vile nadharia tu na haina maana yoyote. Ungana na ubatizo na damu ya Yesu Msalabani na kisha uamini. Hivyo ndivyo inavyotupasa kuamini. Imani ya kinadharia haina maana yoyote. Kwa mfano, kuna uzuri gani wa nyumba nzuri ambayo si mali yako? Ili kuifanya haki ya Mungu iweze kuwa mali yetu tunapaswa kulifahamu dhumuni la ubatizo wa Yesu ambalo lilikuwa ni kuzioshelea mbali dhambi zetu, na kwamba kifo chake Msalabani kilikuwa ni kwa ajili ya mauti ya miili yetu. Ni lazima tukombolewe mara moja na kisha tutembee katika upya wa maisha kwa kupitia imani yetu katika haki ya Mungu iliyotimizwa na Bwana wetu. 
Hivyo, kwa kupitia imani yako iliyokuunganisha pamoja na ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani, basi kwa hakika haki ya Mungu itakuwa yako. Ni lazima tuungane na ubatizo wa Yesu, kwa kuwa ikiwa hatutaungana, basi imani yetu haitakuwa na maana yoyote ile. 
“Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti?” (Warumi 7:24). Kwa kweli haya siyo maombolezo ya Paulo tu bali ni maombolezo yetu pia mimi na wewe na hata wale ambao bado wamejitenga na Kristo. Yeye ambaye anaweza kutuokoa toka katika mahangaiko haya ni Yesu, na tatizo hili linaweza kutatuliwa kwa kumwamini Bwana ambaye alibatizwa, akasulubiwa, na kisha akafufuka kwa ajili yetu. 
Paulo alisema, “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” Hii ina maanisha kuwa Paulo aliungana na Bwana. Ni lazima tuamini kuwa ikiwa tutaungana na kuwa na imani kuwa Bwana wetu alituokoa toka katika dhambi zetu zote kwa kupitia ubatizo na damu yake, basi tunaweza kusamehewa na kupokea uzima wa milele. Dhambi zako zote zitapitishwa kwa Yesu kwa moyo ule ulioungana na Yesu. Baada ya kuipata imani inayounganishwa na Yesu pamoja na kifo chake Msalabani utakuwa umekwisha kufa na kufufuka pamoja naye. 
Yesu alianza huduma yake duniani akiwa na umri wa miaka thelathini. Jambo la kwanza kabisa ambalo Yesu alilifanya katika utume wake lilikuwa ni kuzioshelea mbali dhambi zetu kwa kubatizwa na Yohana Mbatizaji. Kwa nini Yesu alibatizwa? Ili aweze kuzibeba dhambi zote za mwanadamu. Kwa hiyo, tulipoiunganisha mioyo yetu pamoja na haki ya Mungu iliyotekelezwa na Yesu, basi dhambi zetu zote zilipitishwa kwa Yesu kwa kupitia ubatizo wake. Dhambi zetu zote zilipitishwa kwa Yesu na zilioshelewa mbali mara moja na kwa ajili ya wote. 
Kwa kweli Bwana wetu alikuja hapa ulimwenguni na akabatizwa ili kuzibeba dhambi zetu zote na akafa ili kulipa mshahara wa dhambi hizo. Yesu alimwambia Yohana mara kabla hajabatizwa, “Kwa kuwa ndivyo itupasavyo kuitimiza haki yote” (Mathayo 3:15). “Haki yote” ina maanisha ni lile tendo la Yesu la kuupokea ubatizo ambao ulizioshelea mbali dhambi zote za wanadamu ambao walikuwa wamepangiwa kwenda kuzimu, pia haki yote ina maanisha ni kifo chake na ufufuo wake. Je, haki ya Mungu ni nini? Kwa mujibu wa ahadi katika Agano la Kale, ubatizo wa Yesu na kifo chake msalabani ambavyo vimewaokoa wenye dhambi wote ndio haki ya Mungu. Sababu iliyomfanya Yesu akaja hapa duniani katika mwonekano wa mwanadamu na kisha akaupokea ubatizo ilikuwa ni kwa lengo la kuzichukua dhambi zote za mwanadamu katika mwili wake na kisha kuzioshelea mbali. 
Kwa nini Yohana alimbatiza Yesu? Ilikuwa ni kwa lengo la kuitimiza haki yote ya Mungu kwa kuzichukua dhambi zote za wanadamu. Sisi ambao tulibatizwa katika Kristo Yesu pia tulibatizwa katika kifo chake na sasa tunatembea katika upya wa maisha kwa kuwa Yesu alifufuka toka kwa wafu. Kuwa na imani katika haki ya Mungu ni kuamini na kuiunganisha mioyo yetu pamoja na ubatizo wa Yesu, kifo chake Msalabani, na ufufuo wake. Ni muhimu sana kwetu kuamini kuwa Yesu alizichukua dhambi zetu zote katika mwili wake wakati alipobatizwa. Sisi tulizikwa pamoja naye wakati alipokufa Msalabani kwa kuwa tulikuwa tumeungana naye kwa kupitia ubatizo. Ni muhimu sana kwetu kuiunganisha mioyo yetu na Bwana kwa kuamini katika haki ya Mungu hata baada ya kuwa tumekombolewa toka katika dhambi zetu zote. Tunaweza kumtolea Mungu shukrani kwa sababu sisi sote tumekufa pamoja na Kristo wakati alipokufa Msalabani, kwa kuwa alikwisha zichukua dhambi zetu zote kwa kupitia ubatizo wake. 
Kuungana na Yesu kwa imani ni muhimu hata baada ya kuipata haki ya Mungu kwa kupitia ukombozi wetu. Baada ya kuipokea karama ya ukombozi, imani yetu inaweza kupungua na kufifia na kuwa ni kama mabadiliko ya kawaida. Lakini ikiwa tutaiunganisha mioyo yetu na haki ya Mungu, basi mioyo yetu itaishi pamoja na Mungu. Ikiwa tutaungana na haki ya Mungu, basi tutaishi pamoja naye lakini ikiwa hatutaungana na haki ya Mungu, basi hatutaweza kufanya lolote zaidi ya kuwa watu tusio na maana mbele za Mungu. Ikiwa hatutaungana na Bwana Mungu na kisha tukabaki kama watazamaji kana kwamba tunaitamani bustani ya jirani yetu, basi sisi tutakuwa ni watu tusio na maana mbele za Mungu na kisha tutatenganishwa naye. Kwa hiyo, ni lazima tuungane na Neno la Bwana pamoja na haki ya Mungu kwa imani. 
 

Ikiwa Tuna Imani Katika Kuungana na Ubatizo wa Yesu na Kifo Chake Msalabani, Basi Sisi ni Wakristo Ambao Tumeunganishwa na Bwana
 
Kuamini katika haki ya Mungu ni kuungana na Bwana na kuwa na imani ya kuikiri haki yake. Kila sehemu ya maisha yetu ni lazima iungane na haki ya Mungu. Na hivyo ndivyo inavyotupasa kuishi. Ikiwa hatuungani na haki ya Mungu, basi sisi tutakuwa ni watumwa wa miili yetu na kisha tutakufa, lakini mara tu tutakapokuwa tumeungana na haki ya Mungu basi dhambi zetu zote zitasamehewa. Ni pale tu tunapoiunganisha mioyo yetu pamoja na haki ya Mungu ndipo tunapofanyika kuwa watumishi wa Mungu. Na hapo ndipo kazi zote za Mungu zitakapokuwa dhahiri ndani yetu na kwa hiyo matendo yake yote na nguvu zake zote zitakuwa ni zetu. Hata hivyo, ikiwa hatuungani pamoja naye, basi sisi tutabakia kuwa ni watu tusio na maana mbele zake. 
Sisi ni wenye mapungufuu na wadhaifu katika mwili kama ambavyo Paulo alikuwa, hivyo ni lazima tuiunganishe mioyo yetu pamoja na haki ya Mungu. Ni lazima tuungane na kuamini kuwa Yesu alibatizwa na Yohana na alisulubiwa ili kutuokoa wanadamu toka katika dhambi zetu zote. Hii ndiyo aina ya imani inayompendeza Mungu na inayoleta baraka kwa miili na nafsi zetu. Ikiwa tunaamini katika yale ambayo Bwana aliyatenda kwa mioyo yetu iliyoungana katika imani, basi baraka zote za Mbinguni zitakuwa ni mali yetu. Hii ndiyo sababu kwamba tunapaswa kuungana na Bwana. 
Kwa upande mwingine, ikiwa hatuiunganishi mioyo yetu pamoja na haki ya Mungu, basi tutakuwa hatumtumikii yeye. Wale wakristo ambao hawaiunganishi mioyo yao pamoja na haki ya Mungu wanapenda mambo ya kidunia zaidi ya kitu chochote kile. Wao hawana tofauti na wasioamini katika ulimwengu. Wao hufikia hatua ya kuifahamu haki ya Mungu wakati mali zao wanazozipenda kama wanavyoupenda uhai wao zinapochukuliwa kwao. Mali haina nguvu ya kuweza kutawala maisha ya watu. Ni haki ya Mungu tu ndiyo inayoweza kutupatia msamaha wa dhambi, uzima wa milele na baraka. Mali haiwezi kulingana na maisha yetu. Ni lazima tutambue kuwa ikiwa tutaungana na haki ya Mungu, basi sisi pamoja na jirani zetu tutaishi. 
Mioyo yetu ni lazima iungane na haki ya Mungu. Ni lazima tuishi kwa imani na kisha tuiunganishe mioyo yetu pamoja na Kristo. Imani ambayo imeunganishwa na haki ya Kristo ni nzuri. Hatimaye jambo ambalo Paulo analisema katika mwisho wa sura ya saba ni kwamba tunapaswa kuishi maisha ya kiroho hali tukiwa tumeungana na Bwana. 
Je, umewahi kumuona mtu yeyote ambaye amefanyika kuwa mtumishi wa Mungu wakati moyo wake haujaungana na haki ya Mungu? Hakuna hata mmoja! Je, umemwona yeyote ambaye anaikiri injili ya maji na Roho kuwa ni kitu cha muhimu kwa ajili ya msamaha wa dhambi hali akiwa hajaungana na haki ya Mungu? Hakuna hata mmoja. Hata kama tunaifahamu Biblia kwa kiwango gani, imani yetu itakuwa haina maana hadi pale tutakapokuwa tumeungana na haki ya Mungu na kuamini kuwa kwa kuamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani tunaweza kukombolewa toka katika dhambi zetu zote. 
Hata kama tuliwahi kupokea ondoleo la dhambi na kwamba tunahudhuria kanisani, ikiwa hatujaunganishwa na haki ya Mungu basi ukweli utabaki kuwa sisi ni wenye dhambi ambao hatuna sehemu katika mpango wa Mungu. Ingawa tunasema kuwa tunamwamini Mungu, basi ni hakika kuwa tungeweza kutengwa na Mungu ikiwa tusingalikuwa tumeunganishwa na haki yake. Ikiwa tunapenda kuongozwa, kusaidiwa, na kufarijiwa na Kristo basi ni lazima tuunganishwe na haki ya Mungu. 
Je, umepokea haki ya Mungu na msamaha wa dhambi zako zote kwa kuamini katika injili ya maji na Roho? Kama Paulo alivyosema, je unaitumikia sheria ya Mungu kwa akili zako hali mwili wako ukiitumikia sheria ya dhambi kila siku? Ni lazima tuunganishwe na haki ya Mungu wakati wote. Je, nini kitatokea ikiwa hatutaunganishwa na haki ya Mungu? Kwa hakika tutaangamizwa. Lakini wale ambao wameunganishwa na haki ya Mungu wataishi maisha yao hali wakiwa wameunganishwa na kanisa la Mungu. 
Kuiamini haki ya Mungu maana yake ni kuungana na kanisa na watumishi wa Mungu. Tunaweza kuendelea kuishi kwa imani pale tu tunapokuwa tumeunganishwa na haki ya Mungu kila siku. Wale ambao wamesamehewa dhambi zao kwa kuamini katika haki ya Mungu ni lazima waungane na kanisa la Mungu kila siku. Kwa kuwa siku zote mwili unataka kuitumikia sheria ya dhambi, basi ni lazima wakati wote tuitafakari sheria ya Mungu na kisha tuishi kwa imani. Tunaweza kuunganishwa na Bwana ikiwa tutaendelea kutafakari na kuizingatia haki ya Mungu. 
Sisi ambao tunaamini katika haki ya Mungu ni lazima tuungane na kanisa na watumishi wa Mungu katika msingi wa kila siku. Ili kufanya hivyo, inatupasa siku zote kuikumbuka haki ya Mungu. Ni lazima tuifikirie haki hiyo na kuungana na kanisa la Mungu kila siku. Ni lazima tuutafakari ukweli kuwa Bwana alibatizwa ili kuzibeba dhambi zetu zote badala yetu. Tunapokuwa tumeunganishwa katika imani hii na haki ya Mungu, basi tutakuwa na amani toka kwa Mungu na tutaweza kufanywa upya, kubarikiwa na kutiwa nguvu na Mungu. 
Jiunge na haki ya Mungu. Ukifanya hivyo ndipo utaipata nguvu mpya. Ungana na ubatizo wa Yesu na haki ya Mungu sasa. Dhambi zako zote zitachukuliwa mbali. Uunganishe moyo wako na kifo cha Kristo Msalabani. Wewe pia utakufa pamoja naye. Ungana na ufufuo wake. Wewe pia utaishi tena upya. Kwa kifupi, unapoungana na Kristo katika moyo wako, utakufa na kufufuka pamoja na Kristo na kwa sababu hiyo utakombolewa toka katika dhambi zako zote. 
Nini kinatokea ikiwa hatuungani na Kristo? Tunaweza kuchanganywa na kisha tukajiuliza, “kwa nini Yesu alibatizwa? Tofauti pekee kati ya Agano la Kale na Agano Jipya ni kuwa Agano la Kale linazungumzia juu ya ‘kuwekea mikono’ na Agano Jipya linazungumzia kuhusu ubatizo. Sasa jambo kubwa ni lipi? Imani ya kiufahamu au imani ya kinadharia si imani ya kweli na imani hii huishia kuwapeleka waamini kutangatanga mbali na Mungu. 
Wale wanaoamini kwa jinsi hiyo ni kama wanafunzi ambao wanapokea ufahamu toka kwa walimu wao. Ikiwa mwanafunzi anawaheshimu kweli walimu wake, basi ataweza pia kujifunza tabia zao njema, uongozi, au hata haiba kuu. Kwa kweli hatupaswi kulipokea Neno la Mungu kama ni sehemu nyingine ya ufahamu bali tunapaswa kujifunza kwa mioyo yetu juu ya haiba ya Mungu, upendo, rehema, na haki. Tunapaswa kuondokana na ile dhana ya kujaribu kujifunza Neno la Mungu kama sehemu ya ufahamu bali tunapaswa kuungana na haki yake. Kule kuungana na haki ya Mungu kunawaongoza waamini kupata maisha ya kweli. Imani ya kinadharia na kiufahamu si imani iliyoungana na Mungu bali ni imani ya juu juu tu. 
“Rehema ya Mungu,” kama inavyoimbwa katika wimbo, “ni bahari ya kimungu, ni gharika isiyo na mipaka na isiyoweza kupimika.” Wakati mioyo yetu inapokuwa imeunganishwa na haki ya Mungu, basi kutakuwa na amani isiyo na mipaka na isiyopimika kama ilivyo kwa rehema ya Mungu ambayo imetupatia haki ya Mungu. Lakini imani ya kinadharia na kiufahamu ambayo haijaungana na Mungu ni kama maji ya ufukweni yenye kina kifupi. Ikiwa bahari haina kina ni rahisi sana kuvutwa, lakini mtiririko wa mawimbi ya bluu pale mahali ambapo bahari ina kina kirefu ni jambo lisiloelezeka. Lakini katika maji yenye kina kifupi, wakati mawimbi yanapoupiga ufukwe huvunjika, hutengeneza povu na kisha hutawanyika katika muundo mbaya. Imani ya wale ambao hawajaungana na haki ya Mungu ni kama mawimbi haya katika maji ya ufukweni. 
Mioyo ya wale walioungana na Neno la Mungu ni yenye kina na ikiwa imejikita katika Bwana, yenye nguvu na isiyotikisika katika mazingira yote. Mioyo yao inasonga mbele hali ikizingatia mapenzi ya Mungu. Lakini mioyo ya wale ambao hawajaungana na haki ya Mungu inatikisika kirahisi mara inapokutana na tatizo dogo. 
Ni lazima tuwe na imani ambayo imeungana na Bwana. Ni lazima tuungane na Neno la Mungu. Hatupaswi kutikisika tunapokutana na mambo au matatizo madogomadogo. Wale ambao wameungana na Bwana wamebatizwa pamoja na Kristo, wamekufa pamoja na Kristo, na wamefufuka tena pamoja Kristo toka mautini. Kwa kuwa sisi si wa ulimwengu, basi ni lazima tuungane na haki ya Mungu ili tuweze kumfurahisha Mungu ambaye ametupokea sisi kama watumishi wa haki. 
Ikiwa tutaungana na haki ya Mungu, basi kwa hakika tutakuwa na amani wakati wote, tutakuwa na furaha, na tutakuwa na nguvu nyingi kwa sababu nguvu za Bwana zitakuwa ni zetu pia. Kwa nguvu za Mungu na baraka zake tutaweza kuishi kwa baraka nyingi. Ikiwa tumeunganishwa na ubatizo wa Yesu na kifo chake Msalabani kwa imani, basi nguvu zake zote zitakuwa ni zetu pia. 
Unganisha moyo wako na Bwana. Ikiwa utaungana na Bwana, basi utaunganishwa pia na kanisa la Mungu. Na wale ambao wameunganishwa na Mungu wataweza kuungana wao kwa wao hali wakiifanya kazi ya Mungu kwa pamoja katika ushirika huku wakikua katika imani yao katika Neno la Mungu. 
Ikiwa hatuiunganishi mioyo yetu pamoja na Kristo, basi kwa hakika tutapoteza kila kitu. Hata kama imani yetu ni ndogo kama punje ya haradali, Bwana amekwisha zisamehe dhambi zetu mara moja na kwa ajili ya wote. Bado tunapaswa kuungana na ukweli huu kila siku bila kujali madhaifu tuliyonayo. Imani yenye kuungana na Bwana ndiyo inayoweza kukufanya wewe uishi na kumtolea Mungu shukrani katika Yesu Kristo. 
Tunapoungana na haki ya Mungu, tunapata nguvu mpya na mioyo yetu inafanyika kuwa imara zaidi. Mioyo yetu inahesabiwa haki tunapokuwa tumeungana na Neno la Mungu. Ni vigumu kupata maamuzi ya kumtumikia Mungu kwa kuyafuata mawazo yetu pekee. Tunapoungana na ubatizo wa Yesu, Msalaba wake na ufufuko wake, imani yetu itakua na kusimama imara katika maandiko. 
Ni lazima tuiunganishe mioyo yetu pamoja na Bwana. Imani iliyounganishwa na Bwana ndiyo imani ya kweli pekee; na imani ile ambayo haijaungana na Bwana ni imani potofu. 
Tunamtolea Mungu shukrani kwa kuturuhusu kuiunganisha imani yetu na Bwana kwa kutupatia ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani. Ni lazima tuiunganishe mioyo yetu pamoja na Bwana tangu leo na kuendelea hadi siku ya mwisho wakati tutakapokutana na Bwana kwa mara nyingine tena. Hebu tuungane na Bwana. 
Tunahitaji kuiunganisha mioyo yetu na Mungu kwa sababu sisi ni dhaifu mbele zake. Paulo alikuwa ameunganishwa na Mungu na pia alikuwa amekombolewa toka katika dhambi zake. Paulo alifanyika kuwa mtumishi wa Mungu wa thamani sana ambaye aliihubiri injili katika ulimwengu mzima kwa kufahamu na kuamini katika injili ya maji na Roho iliyotolewa na Yesu Kristo ambaye ni haki ya Mungu. Kwa kuwa sisi tu wadhaifu, ambao tunaitumikia sheria ya Mungu kwa akili zetu hali tukiitumikia sheria ya dhambi kwa miili yetu, basi ukweli ni kuwa tunaweza kuishi kwa kuungana na Bwana tu. 
Je, umejifunza sasa kuhusu imani ambayo inatuunganisha na haki ya Yesu? Je, imani yako imeunganishwa na ubatizo wa Yesu? Sasa ni wakati wako kuwa na imani iliyounganishwa na inayoamini katika ubatizo na damu ya Yesu. Wale ambao imani zao bado hazijaunganishwa na haki ya Mungu wameshindwa katika imani yao, wameshindwa katika wokovu wao na katika maisha yao. 
Kwa hiyo, haki ya Mungu ni hitaji la msingi sana kwa ajili ya ukombozi wako. Kule kuunganishwa na Bwana ni baraka inayotuongoza sisi sote kuupokea msamaha wa dhambi na kufanyika watoto wa Mungu. Pokea haki ya Mungu kwa kuungana na kuamini katika haki ya Mungu. Kisha haki ya Mungu itakuwa yako na baraka za Mungu zitakuwa juu yako daima. 
 

Asante Mungu Kwa Yesu Kristo!
 
Mtume Paulo alisema kuwa anamshukuru Mungu katika Yesu Kristo Bwana wetu. Alishukuru kwa ajili ya haki ya Mungu inayopokelewa kwa imani katika Yesu Kristo. Hata baada ya Paulo kuiamini haki ya Mungu, hakuweza kufanya lolote zaidi ya kuitumikia sheria ya Mungu kwa akili zake na kuitumikia sheria ya dhambi kwa mwili wake. Lakini kwa kuwa alikuwa ameamini katika haki ya Mungu kwa moyo wake wote, basi moyo wake haukuwa na dhambi. 
Paulo alikiri kuwa alikuwa amehukumiwa na Sheria katika Yesu Kristo na kwamba alikuwa ameokolewa toka katika dhambi kwa imani kwa sababu ya haki ya Mungu. Pia alisema kuwa wale ambao walikuwa wakikutana na hasira ya Mungu na adhabu ya Sheria yake bado wanaweza kuzaa matunda ya wokovu kwa kuamini katika haki ya Mungu ndani ya mioyo yao. Ndani ya mioyo ya waliozaliwa tena upya kuna mapenzi ya Roho Mtakatifu na pia kuna mapenzi ya mwili. Lakini mtu ambaye hajazaliwa tena upya mtu huyo ana tamaa za mwili tu ndani ya moyo wake. Kwa hiyo, wenye dhambi wanatamani kutenda dhambi tu, na kwa kupitia tabia zao za asili wanajaribu kuzirembesha dhambi zao mbele za macho ya wengine. 
Kwa kawaida mashemasi na wazee wa kanisa ambao hawajazaliwa tena upya huwa wanasema, “Ninapenda kuishi maisha mazuri, lakini sifahamu kwa nini ni vigumu sana kufanya hivyo.” Ni lazima tutafakari kuwa ni kwa nini hawawezi kufanya lolote zaidi ya kuendelea kuishi katika hali kama hii. Hii ni kwa sababu ni wenye dhambi ambao hawajaupokea wokovu kwa kuamini katika haki ya Mungu. Ndani ya mioyo yao kuna dhambi kwa sababu haki ya Mungu haimo ndani yao. Lakini katika mioyo ya waliozaliwa tena upya kuna haki ya Mungu na Roho Mtakatifu na wala hakuna dhambi. 
Wakati Paulo alipokuwa na dhambi katika moyo wake aliomboleza akisema, “Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. Ole wangu, maskini mimi! Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti?” Hata hivyo, Paulo alisema tena, “Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu!” (Warumi 7:25). Hii ina maanisha kuwa Paulo aliupokea wokovu toka katika dhambi zake kwa kuamini katika Yesu Kristo ambaye ameitimiza haki ya Mungu. 
Kitu ambacho Paulo alijaribu kukisema katika sura ya 7 ni kuwa, hapo kabla wakati alipokuwa mtu wa dini wakati hajazaliwa tena upya alikuwa hafahamu kazi ya sheria ilivyokuwa. Lakini Paulo alisema kuwa yeye aliyemkomboa toka katika hali ya ole ya umaskini iliyosababishwa na dhambi ni Yesu Kristo ambaye alikuwa ameitimiza haki ya Mungu. Yeyote anayeamini kuwa Yesu Kristo aliitimiza haki ya Mungu ili kutukomboa sisi toka katika dhambi ataokolewa. 
Wale wanaoamini katika haki ya Mungu wanaitumikia sheria ya Mungu kwa akili zao lakini wanaitumikia sheria ya dhambi kwa miili yao. Miili yao bado inaelemea kule kwenye dhambi kwa kuwa bado haijabadilishwa ingawa wao wamezaliwa tena upya. Mwili unatamani dhambi, lakini akili ambazo zinaiamini haki ya Mungu zinatamani kuifuata haki ya Mungu. Kwa upande mwingine, wale ambao bado hawajapokea msamaha wa dhambi wataongozwa kwa akili na miili yao ili kutenda dhambi kwa kuwa katika misingi ya mioyo yao kuna dhambi. Lakini wale ambao wanafahamu na kuamini katika haki ya Mungu wanaishikilia na kuifuata haki ya Mungu. 
Tunamshukuru Mungu katika Yesu Kristo, kwa kuwa Kristo ameitimiza haki ya Mungu. Shukrani apewe Bwana kwa kutupatia haki yake na kwa kutuongoza sisi ili tuweze kuiamini.