Search

Mahubiri

Somo la 10: Ufunuo (Ufafanuzi juu ya Ufunuo)

[8-2] Je, Mapigo ya Matarumbeta Saba ni Halisi? (Ufunuo 8:1-13)

(Ufunuo 8:1-13)
 
Katika Ufunuo 5 kunaonekana andiko liliwekwa mihuri saba, ambalo Yesu alilichukua. Hii ilimaanisha kwamba Yesu alipewa mamlaka yote na nguvu za Mungu, na kwamba atauongoza ulimwengu kwa mujibu wa mpango wa Mungu kuanzia hapo na kuendelea. Ufunuo 8 inaanza kwa kifungu hiki, “Hata alipoifungua muhuri ya saba, kukawa kimya mbinguni kama muda wa nusu saa. Nami nikawaona wale malaika saba wasimamao mbele za Mungu, nao wakapewa baragumu saba.” Hivyo, Yesu anaifungua muhuri ya saba, kisha anatuonyesha vitu vitakavyokuja. 
Sura ya 8 inaanza kwa kutueleza kwamba mapigo ya matarumbeta saba yataanza kwa maombi ya watakatifu. Kuanzia aya ya 6 na kundelea, sura hii inaanza kuongelea juu ya mapigo ya matarumbeta saba ambayo yataletwa hapa ulimwenguni. 
 

Pigo la Tarumbeta la Kwanza
 
Tarumbeta la Kwanza—Aya ya 7: “Malaika wa kwanza akapiga baragumu, kukawa mvua ya mawe na moto vilivyotangamana na damu, vikatupwa juu ya nchi; theluthi ya nchi ikateketea, na theluthi ya miti ikateketea, na majani mabichi yote yakateketea.”
Kitu cha kwanza kukifahamu ni ule ukweli ikiwa watakatifu tutakuwepo katikati ya mapigo ya matarumbeta saba yatakapokuwa yakiletwa hapa duniani. 
Hapa wanakuja malaika saba ili kuyapiga matarumbeta saba. Tunapaswa kutambua kwamba, kati ya haya mapigo saba, sisi tutabakia hapa duniani na kuyapitia mapigo sita ya kwanza. Pia tunapaswa kutambua kwamba wakati tarumbeta la saba litakapolia, tutanyakuliwa, na kwamba baada ya hapo itafuatiwa na mapigo ya mabakuli saba. 
Aya ya 7 inatueleza kwamba wakati malaika wa kwanza alipolipiga tarumbeta lake, mvua ya mawe na moto vilivyochangamana na damu vilishuka duniani, vikaiunguza theluthi ya ulimwengu na theluthi ya miti. Kwa maneno mengine, theluthi ya mazingira ya asili ya ulimwengu yaliunguzwa. 
Je, tunaweza kuishi katika ulimwengu ambao mazingira ya asili yameunguzwa na kuwa moshi kiasi hicho? Hali mvua ya mawe iliyochanganyikana na damu ikitunyeshea, na wakati miti ikiungua na kuwa majivu, je, tunaweza kweli kuishi hali tumezungukwa na aina hiyo ya mazingira ya asili yaliyounguzwa hadi ardhini? Wakati tutakapokuwa tukipambana kwa kupoteza makazi yetu kwa sababu ya mvua hii ya mawe na moto na iliyochangamana na damu, na wakati misitu minene na vilima vikiungua, ukweli ni kuwa hakuna miongoni mwetu atakayetamani kuendelea kuishi katika ulimwengu wa jinsi hiyo. 
Usisahau kwamba wewe na mimi tunapaswa kulipitia hili pigo la kwanza. Itakapofikia kwamba ndio tunaingia katika pigo hili la kwanza, basi hapo tutapaswa kutambua kwamba Mpinga Kristo yupo tayari duniani. Kwa kuwa mapigo haya yataanza kabla Mpinga Kristo hajatokea kikamilifu ili kudai umiliki kamili wa ulimwengu, basi viongozi wa ulimwengu watatengeneza muungano ili kukabiliana na mapigo, na kiongozi fulani atawakusanya viongozi wengine saba ili kutengeneza nguvu kuu. 
Kisha Mpinga Kristo atatokea katika hali ya kawaida tu kama kiongozi katika mchakato huu. Kadri Mpinga Kristo atakavyoonyesha uwezo mkubwa wa kukabiliana na kuihuisha dunia toka katika uharibifu huu wa mazingira ya kiasili, basi watu wengi hali wakivutiwa na nguvu zake, wataanza kumfuata hali wakifikiri kuwa yeye ni kiumbe wa kiroho, na kwa sababu hiyo wafuasi wake watatokea. 
Biblia inatueleza kwamba wakati malaika wa kwanza atakapolipiga tarumbeta lake, tarumbeta hilo litaleta pigo la kwanza kati ya yale mapigo saba ya matarumbeta, pigo hilo litaunguza theluthi ya dunia. Sisi watakatifu na watu wa ulimwengu huu tutakuwa tukiishi hapa duniani wakati pigo hili likipigwa. Ni nini basi kitatokea kwa ulimwengu? Machafuko yatakuwa mengi sana ulimwenguni, huku magofu, maiti, na majeruhi wakiwa wamelala sehemu mbalimbali; hali ya hewa itakuwa imejawa na moshi na gesi yenye sumu ikizalishwa na ziwa la moto ambalo litakuwa limeugubika ulimwengu wote; hewa itakosa oksijeni na ukuaji wa jangwa kutokana na moto utakuwa ni mkubwa kiasi kwamba utasababisha uwezo duni kwa sayari kuzalisha hewa ya oksijeni. Pigo la kwanza peke yake litauweka ulimwengu huu sehemu kubwa kuwa ni majivu, litaleta uharibifu mkubwa kiasi cha kutuondolea hamu ya kuendelea kuishi hapa duniani. 
Hivyo, kutokana na pigo hili ni lazima tufanye chaguo la busara. Tukiwa tunaishi katika ulimwengu huu wa kawaida, basi tunaweza kuyahofia mapigo makuu na dhiki itakayokuja. Lakini tunaweza kuwekwa huru toka katika hofu hii na badala yake kuwa na ujasiri, kwa kuwa mara baada ya theluthi ya mazingira ya ulimwengu kuungua huku watu wakipiga yote huku na kule, basi sisi tutambua kwamba hili pigo limekwisha na kwamba mapigo mengine bado yanakuja. Kwa kuwa tuna tumaini, basi tunaweza kujazwa na hil tumaini, lakini kwa kuwa pia tuna miili, wakati mwingine tunaweza kutikiswa na hofu. Lakini kwa kuwa tunaifahamu hatma ya dunia hii, basi hatuliweki tumaini letu katika dunia hii, bali katika Ufalme wa Mungu. Kwa imani kama hiyo, na kwa kudumu katika Roho Mtakatifu, tunaweza kuwa wajasiri na imara. 
Kilio cha watu wa ulimwengu kitakuwa kikubwa sana, na sisi pia, tunaweza kujikuta tukiomboleza hasa ikiwa wanafamilia wetu watakuwa ni miongoni mwa wale ambao hawajapokea ondoleo la dhambi zao. Baadhi ya wanafamilia wetu katika mwili, ambao hawajakombolewa dhambi zao, wanaweza pengine kutuuza kwa Mpinga Kristo ili wapate chakula. Kwa upande mwingine, wengine wanaweza kuja kwetu na kutuuliza jinsi wanavyoweza kupokea ondoleo la dhambi zao. Hili linawezekana kabisa, hii ni kwa sababu fursa ya wao kukombolewa itakuwa bado ipo. Biblia inatueleza kwamba wakati mapigo ya matarumbeta saba yatakapowadia, theluthi ya ulimwengu mzima itakufa. Hii pia ina maanisha kwamba theluthi mbili ya ulimwengu itakuwa hai. Wakati theluthi ya idadi ya watu ulimwenguni itakapokuwa imeungua na kufa, basi tutapaswa kutambua kwamba muda wa sisi kuuawa na kuifia-dini na wa kurudi kwa Bwana haupo mbali. Mungu alisema kwamba ataleta mvua ya mawe na moto ikiwa imechangamana na damu toka angani. 
Wakati Mungu atakapouleta moto na mvua ya mawe juu yetu, ukweli ni kuwa hatutaweza kufanya lolote kuikwepa mvua hiyo. Haitawezekana pia, hata kwa kutumia mbinu za kisayansi, yaani kutengeneza ngao ya ulinzi angani ambayo inaweza kuufunika ulimwengu mzima dhidi ya kumiminwa kwa mvua ya mawe na moto. Hata kama tutaweza kutengeneza chombo kama hicho, chombo hicho hakitaweza kabisa kulinganishwa na nguvu za hilo pigo toka kwa Bwana. Tunapaswa kupokea katika mioyo yetu kwamba ni kweli mapigo haya yatakuja kutoka kiuhalisia, na kisha tuishi maisha yetu ya sasa kwa kuamini katika ahadi zote za Neno la Mungu kwa mioyo yetu yote. 
Hivi karibuni, nilisikia katika taarifa kwamba mawe yatokanayo na mvua ya mawe ambayo ni makubwa kama kichwa cha mtu, yakiwa na kipenyo cha sentimita 45 yalianguka huko China. Huku yakishuka kwa kasi toka huko juu, haya mawe ya mvua, yenye ukubwa kama kichwa cha mtu yalikuwa yakianguka kwa nguvu ya kushangaza, huku yakivunja mapaa na kuharibu kila kitu yalimopitia. Kile kitachoanguka na pigo la kwanza ni kikubwa kuliko nguvu ya haya mawe ya mvua. Tunapaswa kuamini kwa mioyo yetu kwamba moto utakaounguza theluthi ya dunia, ambao ni makubwa kuliko haya mawe ya mvua yaliyodondoka huko China, utakuja; na kwamba ni lazima tuitunze imani hii katika mioyo yetu; na kwamba ni lazima tutende kulingana na imani yetu mara pigo hili litakapowadia. Tunapaswa kuamini kwamba ulimwengu huu utaangamizwa hivi karibuni, na pia ni lazima tudhamirie kukabiliana na pigo lolote kwa imani hii, huku tukikubaliana na mauaji ya kuwa wafia-dini. Wakati matarumbeta saba yatakapolia, ukweli ni kwamba mapigo saba yataletwa hapa ulimwenguni. Hili ni pigo la kwanza kati ya haya mapigo saba. 
 

Pigo la Tarumbeta la Pili Likiletwa na Mungu
 
Tarumbeta la Pili—Aya ya 8-9: “Malaika wa pili akapiga baragumu, na kitu, mfano wa mlima mkubwa uwakao moto, kikatupwa katika bahari; theluthi ya bahari ikawa damu. Wakafa theluthi ya viumbe vilivyomo baharini, vyenye uhai; theluthi ya merikebu zikaharibiwa.”
Tunapaswa kuzingatia ukweli kwamba watakatifu wataishi na kupitia hili pigo la pili. 
Hapa andiko linaeleza kwamba kitu kama mlima mkubwa kilitupwa baharini, na kubadili theluthi ya bahari kuwa damu na kuua theluthi ya viumbe hai baharini. Wakati nyakati za mwisho zitakapowadia, utaratibu wa ulimwengu utavunjika, hali ukizidhoofisha kundi la nyota na kuzifanya kugongana na kuvunjika, na kwa sababu ya hili vimondo vingi vitaangukia duniani na kusababisha mgongano mkubwa. Baadhi ya vimondo hivi vitaangukia baharini kwa nguvu kubwa, huku vikibadili theluthi ya bahari kuwa damu, na kisha kuua theluthi ya viumbe hai wa baharini, na kuharibu theluthi ya meli. Hili ni pigo la tarumbeta la pili kati ya mapigo ya matarumbeta saba. 
Je, wakati hili litakapotokea tutaweza kula samaki toka baharini, au kuogelea ndani yake? Haitawezekana kamwe. Wakati kimondo kikubwa kama mlima mkubwa kitakapoangukia baharini, theluthi ya bahari itageuka na kuwa damu, theluthi ya viumbe wake hai watauawa, wataifanya bahari ioze kwa sababu ya mizoga yao iliyokufa, na mawimbi ya bahari na matetemeko yatawaangamiza watu wengi pamoja na meli. 
Nakumbuka niliwahi kuiona sinema moja ambapo kimondo kinaangukia baharini na kusababisha mawimbi makubwa sana yanayoifunika dunia. Ninaamini kwamba watengenezaji wa sinema hii walikuwa na picha halisi kuhusu nyakati za mwisho katika fikra zao. Ni kweli kwamba machafuko makuu yataipiga dunia, na huu ni ukweli ambao hawa watu wasioamini wanautambua. Watu wengi sana watauawa kwa pigo la kuanguka kwa vimondo. Lakini kwa kuwa ni theluthi tuya ulimwengu ndio itakayoharibiwa, wewe na mimi tutaendelea kuishi hapa duniani hadi mapigo ya mabakuli saba yatakapomiminwa. 
Watu walizoea kuamini kwamba unyakuo utatokea baada ya kuisha kwa Dhiki Kuu, lakini baada ya kutokea nadharia ya kunyakuliwa kabla ya dhiki, wanatheolojia wengi walianza kuiamini nadharia hii ya kunyakuliwa kabla ya dhiki. Mbaya zaidi, hivi sasa kuna nadharia ya Amilenia ambayo kimsingi inakana kuhusu Ufalme wa Milenia. Watheolojia, kutokana na kushindwa kwao kuliangalia vizuri Neno la Ufunuo, hivi sasa wanajaribu kulikimbia Neno la kitabu hiki. Wale ambao watalipoteza tumaini lao hapa duniani kuhusiana na mapigo yatakayokuja watakuwa ni wa kulinganishwa kivingine na watakatifu waliozaliwa tena upya na ambao watavumilia hali ilivyo, hali wakiwa wameliweka tumaini lao katika Ufalme wa Milenia katika Mbingu na Nchi Mpya vilivyoahidiwa na Bwana. 
Tunapaswa kuiandaa imani yetu kadri nyakati za mwisho zinavyozidi kutukaribia, lakini badala ya kufanya hivyo, watu wengi wanapendelea kuongelea kuhusu kunyakuliwa kabla ya dhiki au kuhusu Amilenia, wakijaribu kukwepa kukabiliana na imani halisi. Kwa kuwa wanaamini kwamba Yesu atarudi katika mawingu hali wakiendelea katika shughuli zao za kila siku, wakiwa katika maisha yasiyo na bugudha, na kwa kuwa wanaamini kwamba watainuliwa moja kwa moja kwenda katika Ufalme wa Mungu pasipo kupitia mapigo yoyote, basi ukweli ni kwamba hawaiandai imani yao kukabiliana na Dhiki Kuu. 
Kwa mtazamo wa haraka, wale waliotulia na wasiojiandaa kwa ajili ya Dhiki Kuu wanaweza kuonekana kuwa ni majasiri. Sababu inayowafanya wenye dhambi ambao hawajazaliwa tena upya kuonekana kuwa ni majasiri mbele ya Dhiki Kuu ni kwa sababu nafsi zao, baada ya kuwa zimelewa kutokana na uongo wa manabii wa uongo, zimekwisha kufa, na hazina matamanio yoyote ndani yao. Kwa sababu iyo hiyo, yaani kwamba nafsi zao zimekwisha kufa, ndio maana basi watu hao hawaisikii na wanaikataa injili ya maji na Roho inayowawezesha kuzaliwa tena upya kwa maji na Roho na kisha kuingia katika Ufalme wa Mungu (Yohana 3:5).
Lakini waliozaliwa tena upya ni lazima waziandae imani zao kwa ajili ya dhiki katika nyakati za mwisho, hii haijalishi kwamba maisha yao ya sasa yana raha kiasi gani. Wanapaswa kujiandaa mapema kwa ajili ya baadaye kwa kuweka katika akili zao nia ya kuihubiri injili kwa wale ambao watakuwa waaminifu kwa Mungu, ili kwamba waweze kuziokoa nafsi nyingi kadri itakavyowezekana utakapowadia wakati wa Dhiki. 
Kudharau ujio wa karibu wa Dhiki Kuu ni jambo la kijinga kabisa. Wale watakaodharau watajikuta hawana la kufanya mbele ya hayo mapigo, kama kile kilichotokea katika Vita vya Wakorea. Kabla ya kuzuka kwa Vita vya Wakorea, Marekani ilikuwa imegundua uandaaji wa makundi makubwa ya jeshi la Korea ya Kaskazini na waliionya Korea Kusini kuhusu uvamizi unaoweza kujitokeza, lakini serikali ya Korea Kusini na jeshi lake walidharau onyo hilo, kiasi kuwa wakaruhusu hata majeshi kwenda likizo na kuwaruhusu maafisa wa mstari wa mbele kufurahia mapumziko ya mwisho wa wiki katika siku ambayo walivamiwa. 
Kwa kuwa walikuwa hawajajiandaa kwa ajili ya vita basi hata baada ya uvamizi wa Korea Kaskazini kuthibitishwa, ukweli ni kwamba walishindwa kuzuia uvamizi wa Korea Kaskazini na wakasukumwa hadi kusini mwa nchi. Baada ya Korea Kusini kuviita vikosi vyake toka likizo ya mapumzika na kuviandaa kwa vita, askari wake wa mstari wa mbele walikuwa wameshadhoofishwa, na kilichofuatia ilikuwa ni kurudi nyuma huku majeruhi wakiwa wengi sana.
Hii ndiyo aina ya ole ambayo itatukuta ikiwa hatutaliamini Neno ambalo Mungu ameliongea kwetu kuhusu nyakati za mwisho. Lakini kama tutaliamini Neno hilo kwa uaminifu, basi ni hakika kwamba tunaweza kuikwepa hiyo ole. Ufunuo inazungumzia juu ya kimbilio wakati wa Dhiki, lakini haituelezi juu ya eneo halisi ya kukimbilia. Hivyo, inatueleza kwamba watakatifu watalindwa na kutunzwa katika kimbilio. Hili kimbilio si jingine bali ni kanisa. Ni wapi mtu anapoweza kupata kimbilio hapa ulimwenguni? Baadhi ya watu wanasema kwamba wanaweza kuwa hai ikiwa watakimbilia kwenda Israeli. Lakini huko Israeli watakabiliana na dhiku kuu zaidi. Unapaswa kutambua kwamba Mpinga Kristo mwenyewe ataweka makao makuu yake Israeli, basi mapigo yatakuwa ni mazito zaidi pale Israeli. 
Ingawa hili Neno kuhusu dhiki linaweza lisionekana kuwa ni halisia hivi sasa, lakini unapaswa kulifahamu katika moyo wako na kisha ujiandae kwa ajili ya yatakayojiri hapo baadaye. Unapaswa kuliamini hili Neno kwa moyo wako wote, na ni lazima uihubiri injili hii kwa imani hii kwa watu wengine kana kwamba unaishi katika kipindi cha Dhiki Kuu. Unapaswa kuiandaa mioyo ya watu na kuiongoza kwenda katika kimbilio kwa kuwahubiria injili ya maji na Roho. Mungu ametuweka katika makanisa yake ili kwamba tuweze kuwahubiria watu mambo kama haya yatakayokuja na kisha kuwasaidia kuiandaa imani yao kwa ajili ya nyakati za mwisho. 
Hii ndio sababu tunafanya hiki tunachokifanya—yaani, kuihubiri injili ya maji na Roho kwa nguvu zetu zote. Tunalihubiri Neno la Ufunuo nyakati hizi si kwa sababu ya kujisifu, bali kwa kuwa ni Neno ambalo ni la muhimu sana katika kipindi cha sasa kwa waamini na wasio waamini. Ni kwa kuiandaa imani yetu sasa ndipo mioyo yetu inapoweza kutoyumbishwa wakati dhiki na mapigo yatakapotushukia.
Ni kweli, kwamba Mungu atatupatia ulinzi wake maalumu, lakini kwa kuwa tunaishi katika ulimwengu wa kutisha, na mgumu, basi ikiwa tutafahamu kile ambacho kitakuja katika nyakati za mwisho na kisha kuiandaa imani yetu ili kuishinda dhiki, basi tunaweza kuieneza injili zaidi na zaidi. Pia, kwa kuwa tutaweka tumaini letu lenye ujasiri katika Ufalme wa Mungu, basi ni kweli kwamba hatutafagiliwa mbali na ulimwengu wa sasa, wala hatutaiuza imani yetu, bali tutatenda zaidi matendo ya imani. Hii ndio sababu tunalihubiri Neno la Ufunuo na kuzifanya kazi nyingi za imani.
 

Pigo la Tarumbeta la Tatu
 
Tarumbeta la Tatu—Aya ya 10-11: “Malaika wa tatu akapiga baragumu, nyota kubwa ikaanguka kutoka mbinguni, iliyokuwa ikiwaka kama taa, ikaanguka juu ya theluthi ya mito, na juu ya chemchemi za maji. Na jina lake ile nyota yaitwa Pakanga; theluthi ya maji ikawa pakanga, na wanadamu wengi wakafa kwa maji hayo, kwa kuwa yalitiwa uchungu.”
Watakatifu wataishi hadi kulipitia hili pigo la tatu. Pigo katika tarumbeta la pili lililetwa juu ya bahari, lakini wakati huu tarumbeta la tatu litaleta pigo juu ya mito na chemichemi. Nyota kubwa ikianguka kutoka mbinguni ina maanisha ni kimondo. Mito na chemichemi ambazo zitapigwa na hicho kimondo itageuka na kuwa michungu, maana itageuka na kuwa pakanga. Hapo zamani, watu walizoea kusaga pakanga na ule unga wake kwa madhumuni ya dawa, dawa ambayo ilikuwa ni chungu sana kupita maelezo. Biblia inatueleza kwamba kadri hii pakanga itakavyoenea katika maji ya ulimwenguni, basi watu wengi sana watakufa baada ya kunywa maji hayo yenye pakanga. 
Theluthi ya maji safi ulimwenguni yatageuka na kuwa pakanga, watu wengi watakufa kutokana na maji hayo, lakini Bwana atawalinda watu wake katika hili pigo. Huenda kitu ambacho kitasababisha vifo zaidi ni magonjwa yatokanayo na maji, pengine itakuwa ni kutokana na mabadiliko ya kemikali katika maji kutokana na kuangukiwa na kimondo. Kwa maneno mengine, watu hawatakufa ati kwa sababu tu maji yamekuwa ni machungu, bali ni kwa sababu ya kitu kingine zaidi. Tunafahamu na kuamini kwamba haya mambo yote ni halisi, na kwamba ni hakika kuwa yatakuja kutokea hapo baadaye.
 

Pigo la Tarumbeta la Nne
 
Tarumbeta la Nne—Aya ya 12: “Malaika wa nne akapiga baragumu, theluthi ya jua ikapigwa, na theluthi ya mwezi, na theluthi ya nyota, ili kwamba ile theluthi itiwe giza, mchana usiangaze theluthi yake, wala usiku vivyo hivyo.”
Usisahau kwamba watakatifu watakuwa bado wakiishi hapa duniani hadi katika hili pigo la nne.
Ikiwa theluthi ya mwanga wa mchana hauangazi, basi hii ina maanisha kwamba mchana utapungua kwa takribani masaa manne kati ya masaa saba hadi nane. Kwa kuwa mwezi pamoja na nyota zitapoteza theluthi ya nuru yake, basi ulimwengu wote utakuwa giza. Kwa maneno mengine, wakati ingalipaswa kuwa mchana angavu, badala yake kutakuwa na giza. Sinema inayoitwa Unyakuo inafuata nadharia ya kunyakuliwa kabla ya dhiki, lakini katika sinema hiyo unaweza kuuona ulimwengu mzima ukigeuka na kuwa giza wakati wa mchana, huku watu wote wakipatwa na wasiwasi. Hebu fikiria wewe mwenyewe: inadhaniwa kuwa ni saa 5 kamili asubuhi, halafu fumba na kufumbua jua linatoweka na kunakuwa hakuna mwanga. Hata wewe pia utakumbwa na hofu kana kwamba umetembelewa na malaika wa mauti.
Tunafahamu kwamba tutapaswa kuishi na kukipitia kipindi chenye machafuko kama hicho, lakini usiogope. Mungu atatulinda na kutubariki zaidi na zaidi. Wakati huo, imani yako itakuwa na nguvu sana kiasi kwamba Mungu atajibu sara zako na kukusaidia mara utakapoomba kwake. Kwa kuwa Mungu ametuahidi wakati wote kuwa pamoja nasi hadi mwisho wa ulimwengu, basi ni hakika kwamba Mungu hatatuacha peke yetu katika nyakati za Dhiki Kuu. Pasipo shaka yoyote ile, Mungu atakuwa pamoja nasi wakati wote. Kwa hiyo, kwa kuwa Mungu atakuwa pamoja nasi wakati wote, basi tunapaswa kuamini kwamba atatulinda na kuturuhusu kuishi, na kwamba tunapaswa kuieneza imani hii kwa wengine na pia kuziandaa imani zao vilevile.
 

Mapigo Mengine Matatu Yatakayokuja
 
Aya ya 13 inasema, “Kisha nikaona, nikasikia tai mmoja akiruka katikati ya mbingu, akisema kwa sauti kuu, Ole, ole, ole wao wakaao juu ya nchi! Kwa sababu ya sauti zisaliazo za baragumu za malaika watatu, walio tayari kupiga!”
Kama vile malaika alivyosema ole kwa sauti kuu mara tatu, basi ni hakika kwamba kutakuwa na mapigo mengine matatu yatakayofuata hapa duniani. Kwa maneno mengine, kati ya mapigo ya matarumbeta saba, bado kuna mapigo mengine matatu yatakayofuata. Tunapaswa kutambua kwamba itakapofikia tarumbeta la saba basi unyakuo wetu utatokea. Baada ya kuisha kwa mapigo sita, na wakati malaika wa saba atakapolipiga tarumbeta la saba, basi hapo watakatifu watafufuliwa na kunyakuliwa mara moja. Baada ya watakatifu wote kuinuliwa angani, basi hapo ndipo mapigo ya mabakuli saba yatakapomiminwa hapa duniani.
Tunapaswa kutambua kwamba dunia hii hivi punde itaingia katika mwanzo wa mapigo ya matarumbeta saba na yale ya mabakuli saba, ambao haya mapigo ya mabakuli saba yatamiminwa mara baada ya tarumbeta la saba kupigwa kwa mujibu wa mapenzi ya Mungu. Tunapawa kuyaamini hayo yote kwa mioyo yetu yote, na kisha kuilea imani yetu sasa ili kwamba imani yetu iweze kukua na kuweza kuyavumilia mapigo yote. Ikiwa watu wanaamini pasipo kuwa na ufahamu wa nyakati za mwisho, basi ni hakika kwamba wataogopa mara Dhiki itakapokuja, kiasi kwamba wataishia kuikana imani.
Kwa hiyo, ili tuweze kushinda katika nyakati za mwisho, basi imani yetu katika mambo haya ni lazima iambatane na ufahamu sahihi wa nyakati za mwisho. Leo hii, wakati mwisho unatukaribia, basi tunapaswa kutolidharau kanisa au kuangukia mbali na kanisa. Mioyo yetu yote ni lazima iungane katika kanisa, na bila kujalisha chochote kile tunapaswa kuendelea kuliamini Neno la Mungu linalohubiriwa kwetu kupitia kanisa, huku tukishikana na kuishi kwa imani
Wakati mapigo haya yatakapokuja, baadhi ya watu ambao hawajaokoka toka katka familia yako, ukoo, au hata marafiki wanaweza kukugeukia. Hata katika nyakati za kawaida, tunapoulizwa kwamba ndugu zetu, kaka zetu, au wazazi wentu ni akina nani, tukumbuke kwamba Bwana wetu alitueleza kwamba wale wote wanaoyafuata mapenzi ya Baba hao ndio familia zetu, wazazi, na ndugu. Wakati ulimwengu wa dhiki utakapowadia, wale waliozaliwa tena upya watatambua kwa hakika kuwa ndugu, wanafamilia, na akina dada wa kweli ni wepi. Kwa kuwa tunafahamu na kusaidiana kwa imani hii, na kwa kuwa Mungu amekwisha kukukomboa wewe na mimi toka katika mapigo haya, basi Mungu atatuchunga, na kutulinda toka katika mapigo, na atatutunza katika kanisa lake huku tukiwa kama watoto wake. Imani hii inapaswa kupandwa kikamlifu ndani yetu.
Wale ambao katika nyakati za mwisho watatuuza kwa Mpinga Kristo wanaweza kwa hakika kuwa wale wanaotoka katika familia zetu za kimwili. Kwa hiyo, hata kama ni ndugu wa familia zetu, ukweli ni kuwa kama hawajazaliwa tena upya kwa maji na kwa Roho, basi tunapaswa kuwa na imani ya kuwaona ndugu hao kama ni wageni tu. Kwa maneno mengine, wanaweza kufanya mambo mabaya kwetu kuliko hata wageni. Haijalishi ikiwa watu hao ni ndugu wa familia zetu kimwili—ukweli ni kuwa kama hawajaokolewa, basi tunapaswa kuwatambua kwamba hao ni adui zetu. Ni lazima tuifungue mioyo yetu ili kusikia mara mara toka katika Neno la Mungu kuhusiana na jambo hili na kisha tuamini yale yanayoelezwa kuwa ni ukweli.
Kama vile Mungu alivyoigeuza Sodoma na Gomora kuwa ziwa la moto kwa kuwamiminia kibiriti na moto, ni hakikwa kwamba Mungu atayaleta mapigo kama hao katika nyakati za mwisho kwa wenye dhambi. Maangamizi ya Mungu ya Sodoma na Gomora ni ukweli uliothibitishwa na uchimbaji wa maeneo ya kale.
Katika siku hizi, sinema nyingi ambazo maelezo yake ni kuhusu kuangamizwa kwa mwanadamu kutokana na mgongano kati ya ya vimondo na dunia zimekwishatokea. Sinema kama hizo zimetengenezwa kwa kuzingatia Neno la Biblia linalozungumzia juu ya mapigo ya siku za mwisho ambayo yataishukia dunia hii. Uwezekano wa vimondo kuanguka duniani upo juu sana, kiasi kwamba mapigo haya yanaweza kutokea katika ulimwengu huu wa sasa.
Mfano mzuri ni ushahidi wa elimu ya visukuku vya kale toka katika mabaki ya dinosauria, ambayo yanaonyesha kwamba ulimwengu ulipitia mabadiliko makubwa sana katika nyakati za kale. Mfumo wa maisha ulio tofauti unatuonyesha juu ya uwepo wao tofauti kupitia mabaki hayo ya visukuku. Baadhi ya wanasayansi wanapendekeza kwamba utofauti huu wa maisha ya kale, wakiwemo dinosauria, unaelezewa kutokana na mgongano mkubwa kati ya dunia na kimondo. Hivyo, pigo la vimondo linaloandikwa katika Ufunuo 8 linawezakana sana kutokea katika ulimwengu huu.
 

Muda si Mrefu Sana…
 
Tunapaswa kutambua kwamba mapigo ya jinsi hiyo yatakuja hapa duniani muda si mrefu sana. Baadhi ya wanasayansi wamekwisha jaribisha kufanya uzalishaji wa mwanadamu kwa kutumia seli za mwanadamu pasipo kujamiiana, hili ni jambo ambalo linaweza kuleta changamoto kubwa kwa Mungu. Kwa hiyo, mapigo haya yote yapo tayari kuletwa na Mungu katika kipindi hiki. Wanadamu wanapaswa kutomsahau Mungu ati kwa sababu tu ya kuzitegemea nguvu za kisayansi.
Hivi sasa, mwanadamu anajaribu kuyajibu mapigo yote juu ya ulimwengu kwa kutumia nguvu na ufahamu wa kisayansi. Lakini hakuna uvumbuzi wa kisayansi unaoweza kuzuia mapigo ya Mungu, kwa kuwa mapigo hayo ni ya kutisha kuliko machafuko yoyote yale yaliyowahi kutokea hapo kabla. Tunapoyaangalia mavumbuzi ya leo ya kisayansi yaliyofanywa na mwanadamu, tunaweza kuona kwamba mwanadamu anajaribu kuleta changamoto kwa mamlaka ya Mungu, huku akitaka kuwa kama Mungu. Lakini haijalishi kwamba maendeleo ya kisayansi yatakuwa yamefikia kiwango gani, hakuna hata mmoja anayeweza kuyazuia mapigo yatakayoletwa na Mungu. Mapigo haya yote yameletwa si kwa sababu nyingine yeyote bali ni kwa sababu ya mwanadamu mwenyewe.
Njia pekee ya kuyakwepa mapigo yatakayoletwa na Mungu ni kuugundua ukweli wa wokovu kwa kupitia injili ya maji na Roho, na kisha kupata kimbilio katika mikono ya Bwana kwa kuiamini injili hiyo. Hebu uyakwepe mapigo haya kwa kutambua na kuamini kwamba njia pekee ya wewe kuyakwepa mapigo hayo ya kutisha ni imani yako katika injili ya maji na Roho.
Baraka zote na laana zimeshikiliwa katika mikono ya Mungu. Ikiwa Mungu anaamua kuihifadhi dunia hii, basi ni hakika kwamba dunia itaishi; lakini asipoamua, ni hakika kwamba dunia hii itaangamizwa. Kwa hiyo utakapokuwa ukiishi katika kipindi hicho, basi ikiwa unaamini na kulifuata Neno la Mungu huki ukimhofia Mungu, basi ni hakika kwamba Mungu atakuongoza kwenda katika injili ya maji na Roho ambayo itakulinda dhidi ya mapigo ya kutisha yatakayokuja.
Hata sasa, kuna watu wengi sana ulimwenguni kote wanaendelea kufa na kutetemeka kwa hofu kutokana na matetemeko ya ardhi, vimbunga, na magonjwa. Zaidi ya yote, vita haiishi kila mahali, huku mataifa yakisimama dhidi ya mataifa mengine, na huku tawala zikisimama dhidi ya tawala nyingine. Kwa hiyo, wakati Mpinga Kristo atakapotokea hivi karibuni na kisha kuyatatua matatizo ya machafuko kama hayo, basi watu wengi sana watamfuata. Hii itafuatiwa na kushuka kwa mapigo ya kutisha zaidi hapa duniani, na hatimaye ulimwengu huu utaangamizwa kikamilifu kwa mapigo haya yatakayoletwa na Mungu.
Mungu ataumba Mbingu na Nchi Mpya na kisha kuwapatia wale waliokombolewa toka katika dhambi. Dhumuni la uumbaji wa Mungu wa Mbingu na Nchi Mpya ni ili kuwapatia wale waliozaliwa tena upya kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. Muda si mrefu, Mungu atauangamiza ulimwengu wa kwanza na kisha kuufungua ulimwengu wa pili. Kama vile ulimwengu wa kale wa dinosauria ulivyotoweka, basi vivyo hivyo ulimwengu huu wa sasa wenye ustaarabu wa kisayansi ndivyo utakavyotoweka, nasi tutashuhudia kwa macho yetu kuhusu mwanzo wa ulimwengu mpya ambao Mungu atauleta.
Hivyo ni lazima tufikirie jinsi tutakavyoishi sasa. Ni lazima tuamini juu ya mapigo yote yatakayokuja kama yalivyoandikwa katika kifungu cha leo cha maandiko, na kisha tuishi maisha yetu yaliyosalia kwa ajili ya haki ya Mungu, hali tukijiandaa kwa ajili ya ulimwengu ujao kwa imani. Ni lazima tuwe na ufahamu kuhusu Neno la unabii la Ufunuo. Ninasema hivi kwa sasa kwa kuwa siku itakapowadia, ufahamu wote ambao umeupata utakuwa ni wa faida kubwa kwa imani yako.
Vitu vyote katika anga ambavyo vinaweza kugongana na dunia, yaani kuanzia vimondo-sayari ambavyo vimetawanyika kati ya sayari ya Zuhura na ile ya Jupita hadi vimondo vingi ambavyo hata mzunguko wake haufahamiki vinaitwa kwa umoja wao “Vitu Vilivyo Karibu na Dunia (VIVIKADU).” Wakati fulani taasisi ya uchunguzi wa anga za mbali inayoitwa NASA iliwahi kuorodhesha VIVIKADU 893 vikiwemo katika mfumo wa anga peke yake. Ikiwa kimojawapo kati ya hivyo VIVIKADU kingeliigonga dunia, basi madhara ambayo yangeletwa kwa tukio hilo ni makubwa sana kuliko mtu anavyoweza kufikiri. Madhara yake yanaweza kuwa makubwa sana kuliko yale ya mabomu elfu moja ya nyuklia kwa pamoja.
Hebu fikiria ni kitu gani kingelitokea basi wakati huo. Ni hakika kwamba misitu, maji, na meli zingeliharibiwa. Hivyo, wanadamu wote ni lazima waiamini injili ya maji na Roho na kisha waishi maisha yao huku wakijiandaa kwa ajili ya maisha ya milele.
Bwana ametueleza kwamba wakati mapigo ya kiasili yatakapo kuja hapa duniani, theluthi ya jua, mwezi, na nyote zote zitapoteza nuru yake. Lakini ni watu wachache sana wanaolifahamu hili, na watu wachache pia wanaoliamini hili. Kwa hiyo, ni idadi ndogo tu ya watu inayoamini katika injili ya maji na Roho na ndio hao wanaouhubiri ukweli wa injili hii.
Akili zetu ni lazima ziamke. Ni hakika kwamba mapigo yatakuja. Ni lazima tufahamu kwamba tunapaswa kuishi kwa imani gani katika maisha yetu yote yaliyosalia. Wewe na mimi ni lazima tutambue kwamba kipindi cha leo ni hatua chache sana hadi kuifikia Dhiki Kuu, hivyo ni lazima tuishi maisha yetu yaliyosalia katika imani, na pasipo kuwa na shaka katika mioyo yetu.
Ikiwa hatutaishi kwa kuliamini Neno la unabii kuhusu hii Dhiki, basi ni hakika kwamba mioyo yetu itakuwa mitupu, na madhumini yetu yatapotea, na hivyo tutagubikwa na mashaka ya maisha. Tujitahidi hali hii isitokee. Wakati huo huo, hatupaswi kuishi maisha yetu hali tukiliweka tumaini letu katika ulimwengu huu, kana kwamba hatutauacha ulimwengu huu. Wale walio na ufahamu wa kisayansi kwa kiwango kidogo wanafahamu wazi kwamba hakuna tumaini kwa ulimwengu huu. Ni hakika kwamba Mungu ataufanya ulimwengu huu kuwa kama uchafu.
Mungu ataufanya Ufalme mpya wa Yesu na kisha kuwaruhusu wenye haki kuishi ndani yake. Naye atawaruhusu wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho kuishi pamoja naye milele.
Tunapaswa kuachilia mbali nia na mawazo yetu binafsi mbele za Mungu, na kisha kwa unyenyekevu tulipokee na kuliamini Neno lake la unabii. Tunapaswa kuihubiri injili ya maji na Roho, ili tuweze tena kuonana na Bwana mara atakapokuja. Hebu tuishi kwa ajili ya kazi hii ya Mungu. Wakati Bwana atakaporudi hapa duniani, basi sisi tutapokea maisha mapya, miili yetu itabadilishwa na kuwa kama mwili wa Bwana, kisha tutaishi tena katika ulimwengu wake mpya, mambo haya yote yatatokea kama alivyotuambia.
Hatufahami siku halisi ambayo Bwana atarudi. Lakini kwa kuziangalia ishara za ulimwengu, basi tunafahamu wazi kwamba yale mapigo yote yaliyoandikwa katika Neno la Mungu yanatukaribia kwa karibu kabisa. Hivyo, sisi tunamwamini Mungu ambaye ametabiri mambo haya yote, na ambaye ametuonyesha njia ya wokovu.