Search

Mahubiri

Somo la 10: Ufunuo (Ufafanuzi juu ya Ufunuo)

[8-1] Matarumbeta Yanayoyatangaza Mapigo Saba (Ufunuo 8:1-13)

(Ufunuo 8:1-13)
“Hata alipoifungua muhuri ya saba, kukawa kimya mbinguni kama muda wa nusu saa. Nami nikawaona wale malaika saba wasimamao mbele za Mungu, nao wakapewa baragumu saba. Na malaika mwingine akaja akasimama mbele ya madhabahu, mwenye chetezo cha dhahabu, akapewa uvumba mwingi, ili autie pamoja na maombi ya watakatifu wote juu ya madhabahu ya dhahabu, iliyo mbele ya kiti cha enzi. Na moshi wa ule uvumba ukapanda mbele za Mungu pamoja na maombi ya watakatifu, kutoka mkononi mwa malaika. Na huyo malaika akakitwaa kile chetezo, akaijaza moto wa madhabahu, akautupa juu ya nchi, kukawa radi na sauti na umeme na tetemeko la chi. Na wale malaika saba wenye baragumu saba wakajifanya tayari ili wazipige. Malaika wa kwanza akapiga baragumu, kukawa mvua ya mawe na moto vilivyotangamana na damu, vikatupwa juu ya nchi; theluthi ya nchi ikateketea, na theluthi ya miti ikateketea, na majani mabichi yote yakateketea. Malaika wa pili akapiga baragumu, na kitu, mfano wa mlima mkubwa uwakao moto, kikatupwa katika bahari; theluthi ya bahari ikawa damu. Wakafa theluthi ya viumbe vilivyomo baharini, vyenye uhai; theluthi ya merikebu zikaharibiwa. Malaika wa tatu akapiga baragumu, nyota kubwa ikaanguka kutoka mbinguni, iliyokuwa ikiwaka kama taa, ikaanguka juu ya theluthi ya mito, na juu ya chemchemi za maji. Na jina lake ile nyota yaitwa Pakanga; theluthi ya maji ikawa pakanga, na wanadamu wengi wakafa kwa maji hayo, kwa kuwa yalitiwa uchungu. Malaika wa nne akapiga baragumu, theluthi ya jua ikapigwa, na theluthi ya mwezi, na theluthi ya nyota, ili kwamba ile theluthi itiwe giza, mchana usiangaze theluthi yake, wala usiku vivyo hivyo. Kisha nikaona, nikasikia tai mmoja akiruka katikati ya mbingu, akisema kwa sauti kuu, Ole, ole, ole wao wakaao juu ya nchi! Kwa sababu ya sauti zisaliazo za baragumu za malaika watatu, walio tayari kupiga.”
 

Mafafanuzi
 
Ufunuo 8 inaeleza juu ya mapigo ambayo Mungu atayaleta juu ya dunia hii. Moja kati ya maswali ya msingi hapa ni kwamba watakatifu watahusishwa ama kutohusishwa katika kuteseka chini ya mapigo hayo. Biblia inatueleza kuwa watakatifu pia, watayapitia mateso ya matarumbeta saba. Kati ya mapigo saba, watakatifu watayapitia mapigo yote isipokuwa ni lile pigo la mwisho. Mapigo haya saba ya matarumbeta yanayoonekana katika sura hii ni mapigo halisi ambayo Mungu atayaleta duniani. Mungu anatueleza kuwa atauadhibu ulimwengu kwa mapigo ambayo yataanza kwa sauti za matarumbeta saba ya malaika.
 
Aya ya 1: Hata alipoifungua muhuri ya saba, kukawa kimya mbinguni kama muda wa nusu saa.
Aya hii inaeleza juu ya ukimya kabla hasira ya Mungu haijamiminwa kwa wanadamu. Mungu atakaa kimya kwa muda kabla ya kuyaleta mapigo yake makali na ya kutisha hapa duniani. Hii inatuonyesha jinsi ambavyo mapigo ya Mungu ya matarumbeta saba yatakavyokuwa. Wakati wanadamu watakaposimama mbele za Mungu baada ya mapigo haya, basi wale waliookoka watapokea uzima wa milele, lakini wale ambao hawajaokoka watapokea adhabu ya milele. Hivyo, tukikitambua aina ya kipindi tunachoishi, basi tunapaswa kuwa macho na kuifanya kazi ya uinjilisti.
 
Aya ya 2: Nami nikawaona wale malaika saba wasimamao mbele za Mungu, nao wakapewa baragumu saba.
Mungu aliwatumia malaika saba kuifanya kazi yake. Lakini tusisahau kwamba katika kipindi cha sasa, Mungu anafanya kazi kupitia wenye haki wanaoamini katika Neno la injili ya maji na Roho.
 
Aya ya 3: Na malaika mwingine akaja akasimama mbele ya madhabahu, mwenye chetezo cha dhahabu, akapewa uvumba mwingi, ili autie pamoja na maombi ya watakatifu wote juu ya madhabahu ya dhahabu, iliyo mbele ya kiti cha enzi.
Hii inatuonyesha kuwa Mungu atayaleta mapigo yake yote duniani, baada ya kuwa ameyasikia maombi ya watakatifu yaliyotolewa katikati ya mateso na mapigo toka kwa Shetani na wafuasi wake. “Chetezo cha dhahabu” kina maanisha ni maombi ya watakatifu, na hii ina maanisha kuwa kadri maombi yao yanavyotolewa kwa Mungu, basi kazi zote za Mungu zitatimizwa. Mungu anafanya kazi kwa kuyasikia maombi ya watakatifu.
 
Aya ya 4: Na moshi wa ule uvumba ukapanda mbele za Mungu pamoja na maombi ya watakatifu, kutoka mkononi mwa malaika.
Hii inaonyesha ni kwa kiasi gani Mpinga Kristo amewatesa watakatifu katika dunia hii. Kutokana na mapigo ya nyakati za mwisho, watakatifu watamwomba Mungu ili kumwondoa Mpinga Kristo, kuyafanya mapigo yawapite kwa haraka, na kisha kuwaonyesha wanaowaua jinsi hasira ya Mungu ilivyo kali juu yao. Aya hii inaonyesha kuwa Mungu atayapokea maombi ya watakatifu wote. Baada ya kuyapokea maombi haya ya watakatifu, basi hapo ndipo Mungu atakapoanza kumhukumu Mpinga Kristo na wafuasi wake kwa mapigo saba ya matarumbeta na yale ya mabakuli saba. Hukumu ya Mungu kwa Mpinga Kristo na wafuasi wake ni jibu la mwisho kwa maombi ya watakatifu.
 
Aya ya 5-6: Na huyo malaika akakitwaa kile chetezo, akaijaza moto wa madhabahu, akautupa juu ya nchi, kukawa radi na sauti na umeme na tetemeko la chi. Na wale malaika saba wenye baragumu saba wakajifanya tayari ili wazipige.
Mungu anayaandaa mapigo ya matarumbeta saba hapa duniani. Hivyo, ulimwengu huu hauwezi kukwepa kelele, ngurumo, radi, na matetemeko ya ardhi.
 
Aya ya 7: Malaika wa kwanza akapiga baragumu, kukawa mvua ya mawe na moto vilivyotangamana na damu, vikatupwa juu ya nchi; theluthi ya nchi ikateketea, na theluthi ya miti ikateketea, na majani mabichi yote yakateketea. 
Pigo la kwanza ni la kuunguza theluthi ya dunia, ambapo theluthi ya miti na nyasi vitaungua. Pigo hili litaangukia juu ya misitu ya ulimwengu huu.
Ni kwa nini Mungu atalileta pigo la aina hii? Kwa sababu, pamoja na kuwa watu wameuona uzuri wa uumbaji wa Mungu kwa macho yao wenyewe, bado hawakumtambua Muumba kuwa ni Mungu na kumwabudu yeye, na badala yake “waliabudu na kuutumikia uumbaji badala ya Muumbaji” (Warumi 1:25). Hivyo, Mungu anayaleta mapigo ya matarumbeta saba kwa wale wote wasiompatia Mungu utukufu na badala yake wanasimama kinyume na Mungu.
 
Aya ya 8-9: Malaika wa pili akapiga baragumu, na kitu, mfano wa mlima mkubwa uwakao moto, kikatupwa katika bahari; theluthi ya bahari ikawa damu. Wakafa theluthi ya viumbe vilivyomo baharini, vyenye uhai; theluthi ya merikebu zikaharibiwa.
Pigo la tarumbeta la pili linahusisha nyota inayoanguka na kuiangukia dunia. Nyota hii itaangukia baharini na kisha kuibadili theluthi ya bahari kuwa damu, itaua theluthi ya viumbe hai waishio baharini na kisha itaharibu theluthi ya merikebu. Wanadamu wamepokea baraka nyingi sana kupitia hali ya asili iliyoumbwa na Mungu, halafu wakawa waasi na kuwa kinyume na Mungu. Pigo hili la pili linawaadhibu wanadamu kwa sababu ya dhambi hii.
 
Aya ya 10: Malaika wa tatu akapiga baragumu, nyota kubwa ikaanguka kutoka mbinguni, iliyokuwa ikiwaka kama taa, ikaanguka juu ya theluthi ya mito, na juu ya chemchemi za maji.
Kwa nini Mungu aliiruhusu hii nyota kuanguka “juu ya theluthi ya mito na katika chemchemi za maji?” Ni kwa sababu, mwanadamu, pamoja na kuwa anaishi kwa msaada wa Bwana ambaye ndiye chanzo cha uhai, ukweli ni kuwa hakumwabudu na kumshukuru Mungu, na badala yake alimdharau huyu Bwana wa uzima.
 
Aya ya 11: Na jina lake ile nyota yaitwa Pakanga; theluthi ya maji ikawa pakanga, na wanadamu wengi wakafa kwa maji hayo, kwa kuwa yalitiwa uchungu.
Kutokana na pigo hili theluthi ya mito na chemchem za maji zitageuka na kuwa pakanga, na watu wengi watakufa baada ya kuyanywa maji yake. Hili ni pigo la adhabu kwa kwenye dhambi ambao walikuwa wamesimama kinyume na Mungu na wakainyanyasa mioyo ya watakatifu. Hivyo, Mungu hataacha kuwalipiza wenye dhambi kwa matendo yao yote waliyoyafanya dhidi ya wenye haki. Wakati wenye dhambi wanapoleta mateso kwa wenye haki, basi ni hakika kuwa Mungu atawahukumu. Pia pigo hili la tatu ni pigo jingine juu ya hali ya asili; ni pigo lililoletwa kwa sababu ya dhambi za watu za kutotii kwa kutoiamini injili ya maji na Roho iliyotolewa na Mungu. “Pakanga” katika Biblia imekuwa ikimaanisha hukumu kwa wale wote wasiomtii na wanaompinga Mungu.
 
Aya ya 12: Malaika wa nne akapiga baragumu, theluthi ya jua ikapigwa, na theluthi ya mwezi, na theluthi ya nyota, ili kwamba ile theluthi itiwe giza, mchana usiangaze theluthi yake, wala usiku vivyo hivyo.
Pigo la nne ni la jua, mwezi, na nyota kutiwa giza. Katika kipindi hiki chote mwanadamu amekuwa akimfuata Shetani ana amelipenda giza. Wamekuwa wakiukataa mwanga wa wokovu unaoangazwa na injili ya maji na Roho iliyotolewa na Yesu Kristo. Kwa hiyo, ili kuwafundisha wanadamu jinsi ulimwengu wa gizo ulivyo wa kutisha, basi Mungu atawaletea pigo hili la kuleta giza. Pia pigo hili linaonyesha jinsi hasira ya Mungu ilivyo kali kwa ajili ya dhambi yao ya kumchukia Yesu Kristo na kuipenda giza. Hivyo, theluthi ya jua, mwezi, na nyota za ulimwengu huu zitapoteza nuru yake na kutiwa giza.
 
Aya ya 13: Kisha nikaona, nikasikia tai mmoja akiruka katikati ya mbingu, akisema kwa sauti kuu, Ole, ole, ole wao wakaao juu ya nchi! Kwa sababu ya sauti zisaliazo za baragumu za malaika watatu, walio tayari kupiga!”
Aya hii inatueleza kuwa bado kuna ole nyingine tatu zitakazokuja kwa wale wote wanaoishi katika ulimwengu huu. Hivyo, wenye dhambi wote, na wale wote wanaosimama kinyume na Mungu wanapaswa kukombolewa toka katika dhambi zao zote kwa kuamini katika injili ya maji na Roho mara moja.