Search

Mahubiri

Somo la 9: Warumi (Maoni juu ya Kitabu cha Warumi)

[SURA YA 9-3] Je, Ni Makosa Kwa Mungu Kumpenda Yakobo? (Warumi 9:30-33)

(Warumi 9:30-33)
“Tuseme nini, basi? Ya kwamba watu wa Mataifa, wasioifuata haki, walipata haki; lakini ile haki iliyo ya imani; bali Israeli wakiifuata sheria ya haki hawakuifikilia ile sheria. Kwa sababu gani? Kwa sababu hawakuifuata kwa njia ya imani, bali kana kwamba kwa njia ya matendo. Wakajikwaa juu ya jiwe lile likwazalo, kama ilivyoandikwa: 
‘Tazama, naweka katika Sayuni jiwe likwazalo, na mwamba uangushao; 
Na kila amwaminiye hatatahayarika.’”
 

Katika kutuita sisi sote Bwana wetu alisema, “Kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi” (Mathayo 9:13). Ni lazima tutambue kuwa karama ya wokovu hairuhusiwi kwa wale wanaoifuata haki yao wenyewe, ili kuepuka hali hii tunapaswa kuamini katika haki ya Mungu. 
Warumi 9:13 inasema kuwa Mungu alimpenda Yakobo kuliko Esau. Mungu amewapatia wale zawadi ya ondoleo la dhambi na baraka ya kuwafanya kuwa watu wake wale ambao wanaipokea haki ya Mungu kwa shukrani. Sisi sote ni lazima tumwamini Mungu hali tukiwa na ufahamu katika haki yake. 
Tunapaswa kujifunza na kulifahamu Neno la haki ya Mungu lilitolewa kwetu sote. Wakati mtu anataka kukombolewa toka katika dhambi zake, basi mtu huyo anapaswa ayafahamu mapungufu na udhaifu wake na pia ni lazima aifahamu haki ya Mungu. Ni lazima tuifahamu na kuiamini haki yake. Mungu alitueleza kuwa wale wanaofahamu kuwa wamefungwa kuzimu ndio walio na uhitaji wa haki ya Mungu. Ni muhimu sana kuzitambua dhambi zetu na kutambua kuwa kwa sababu ya dhambi hizi sisi sote tunakabiliana na ghadhabu ya Mungu ambayo itatufanya tuadhibiwe kuzimu. 
Lakini tunaweza kupokea katika mioyo yetu injili ya maji na Roho kwa kupitia ubatizo wa Bwana wetu, kifo chake Msalabani na ufufuo wake, hii ni kwa sababu ni wale tu wanaoifahamu haki ya Mungu ndio wanaoweza kuiamini haki hiyo. Hii ni kwa sababu neema ya Mungu na upendo wake si vitu vinavyoweza kupatikana kwa maombi ya toba au maisha ya huzuni ambayo watu wengi wa kidini wamekuwa wakiishi hivyo. Hata hivyo, ondoleo la dhambi lililotolewa na Mungu ni kwa wale wote wanaonyenyekea na kuiamini haki yake. 
Sisi sote ni lazima tuwe tayari kuiamini injili ya maji na Roho kwa hiari katika mioyo yetu. Je, unapenda kuipokea haki ya Mungu? Basi kama ni hivyo, kiri mapungufu yako mbele za Mungu na mbele ya sheria yake. Tambua kuwa upo chini ya ghadhabu ya Mungu kwa sababu ya dhambi zako na kwamba unahitaji haki ya Mungu! Unapoamini katika injili ya maji na Roho na kisha ukaikubali katika moyo wako, basi haki ya Mungu itakuwa yako. Ni lazima uufahamu ukweli huu. 
 

Akili za Wale Wasioiamini Haki ya Mungu Zimechanganyikiwa na Kufungwa Katika Utupu. 
 
Mungu alitueleza kuwa mawazo na akili zetu zilichanganyikiwa tangu hapo mwanzo (Mwanzo 1:2). Kwa nini mawazo ya mwanadamu yalichanganyikiwa tangu hapo mwanzo? Hii ni kwa sababu malaika walioanguka na kuwa kinyume na Mungu waliwazuia watu kuliamini Neno la haki ya Mungu kwa kuyafanya mawazo yao kuchanganyikiwa na kuwa na utupu. Hii ndiyo sababu dhambi ilikuja katika moyo wa mwanadamu (Mwanzo 3:1-8). 
Maandiko yanatueleza kuwa malaika aliyeumbwa na Mungu aligeuka na kuwa kinyume na Mungu. Malaika huyu alijaribu kukiteka kiti cha enzi cha Mungu kwa nguvu zake na mipango yake, na baada ya kuwa ameshindwa katika uasi huo, malaika huyo alifukuzwa na kuondolewa toka katika fursa aliyokuwa nayo. Malaika huyu aliyeanguka aliwarubuni na kuwadanganya wanadamu na akawabadilisha na kuwafanya kuwa kinyume na Mungu. Malaika huyu anaitwa Shetani. Malaika huyu mwenye majivuno bado anatenda kazi waamini na wasio waamini katika namna zote za uasi na majivuno. Shetani alilitea changamoto Neno la haki ya Mungu na mamlaka yake kwa kumdanganya mwanadamu. 
Mara nyingi Ibilisi anatumia uongo ili kwamba watu wasiweze kuiamini injili ya maji na Roho. Baada ya kuwa wamedanganywa na Ibilisi, basi watu wengi wasio na matunda hujitahidi kuanza kuishi kwa kuifuata haki yao wenyewe. Shetani aliwafanya wanadamu kuanguka katika dhambi na kama matokeo ya hilo aliwafanya wanadamu kuishi maisha yao wakiwa na akili zilizochanganyikiwa na zenye utupu. 
 

Ondoleo la Dhambi na Haki Iliyotolewa na Mungu
 
Ukombozi wa mwanadamu toka katika dhambi, mwanadamu aliyekuwa ameangukia katika dhambi kwa sababu ya majaribu ya Shetani, hakutegemei juu ya ridhaa ya haki binafsi. Hata hivyo, ni jambo la kuhuzunisha kuwa watu wengi wanajaribu kuzikwepa dhambi zao katika utupu hali wakigeuka kinyume na Mungu pasipo kuyatambua mapungufu yao. Mungu aliwakemea wale ambao walikuwa wakiitafuta haki yao wenyewe, yaani wale wanaojaribu kuipata haki ya Mungu kwa matendo yao mema. Kwa kweli ukombozi na haki ya Mungu haviwezi kuwafikia watu wa jinsi hiyo; ukombozi na haki ya Mungu vitawafikia wale wanaofahamu kuwa wao ni wenye dhambi, na wanaoamini katika injili ya kweli ya maji na Roho. 
Kwa asili, mapenzi ya Mungu ni tofauti kabisa na mawazo ya mwanadamu. Paulo alitueleza kuwa haijalishi mtu anavyoweza kujionyesha kuwa mwema katika hali yake ya nje ya usafi wa kidini, kuhudhuria kanisani, maombi ya usiku wa manane, maombi ya alfajiri na mapema, kufunga, kutoa zaka na matoleo mengine, n.k; ukweli utabaki kuwa mtu wa jinsi hiyo hataweza kamwe kuzisafisha dhambi zake. 
Mungu anatueleza kuwa matendo ya sheria hayawezi kutukomboa kamwe toka katika dhambi zetu na kuifanya haki ya Mungu kuwa mali yetu. Kama ambavyo aya za 32-33 za sura ya 9 zinavyosema, “Kwa sababu gani? Kwa sababu hawakuifuata kwa njia ya imani, bali kana kwamba kwa njia ya matendo. Wakajikwaa juu ya jiwe lile likwazalo, kama ilivyoandikwa, Tazama, naweka katika Sayuni jiwe likwazalo, na mwamba uangushao; na kila amwaminiye hatatahayarika.”
Kwa hiyo, ili kuipokea haki ya Mungu ni lazima tuamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani, ambavyo kwa hivyo, Yesu alifanyika kuwa sadaka ya kuteketezwa kati ya Mungu na wanadamu. Kwa hiyo ni jambo la muhimu sana kutambua kuwa ili uweze kuipata haki ya Mungu basi unapaswa kuiachilia mbali haki yako binafsi. Hatupaswi kuikataa haki ya Mungu ambayo inatolewa kwetu bure wakati tunapomkiri Yesu kuwa ni Mwokozi wetu. 
Hata sasa, watu wengi wanaomkiri Bwana Yesu kuwa ni Mwokozi wao wanabakia kuwa ni wenye dhambi kwa sababu hawaamini katika injili inayoidhihirisha haki ya Mungu. Watu hawawezi kujipatia haki ya Mungu kwa kuifuata Sheria. Wale wanaoamini katika Neno la haki ya Mungu ni lazima waachane kabisa na haki zao binafsi. Ni lazima ukumbuke kuwa Yesu alifanyika kuwa ni jiwe linalokwaza kwa wale waliokuwa wakiufuata ukombozi wao na haki ya Mungu kwa matendo yao ya sheria. 
Injili ya maji na Roho ilitolewa na Mungu ni ukweli ambao unawakomboa wale ambao wanaamini katika Yesu Kristo kuwa ni Mwokozi wao, na imani ya jinsi hiyo ni lazima iendane na wale wanaoitafuta haki ya Mungu. Jambo la muhimu kwa ukombozi na uzima wa milele ni imani katika Neno la haki ya Mungu lililodhihirishwa kwa kupitia ubatizo na damu ya Yesu Msalabani. Neno hili linatufunulia sisi tunaofikiri hatuwezi kupokea ondoleo la dhambi na kwa wakati huo huo linatufundisha kuwa wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho wataipokea haki ya Mungu. 
Kwa hiyo, imani sahihi inahitaji uelewa wa kwamba Mungu hakuamua kubeba kundi fulani la watu na kuwatupa kuzimu bila sababu yoyote. Ingekuwa ni kweli kuwa Mungu aliwapenda watu fulani na kisha akawachukia wengine bila sababu, basi kwa hakika watu wasingeiheshimu haki yake. 
Kwa kupitia injili ya maji na Roho, Mungu ameiweka sheria ya haki ya ukombozi ili kuwakomboa wenye dhambi wote toka katika dhambi zao, na pia ametupatia baraka kuu ya kuvikwa upendo wake. Kila mtu ni lazima aachilie mbali haki yake binafsi mbele ya injili ya maji na Roho iliyonenwa na haki ya Mungu. Mungu aliwapatia haki yake wale waliokuwa wakiiamini haki hiyo. 
Mungu hakuwaruhusu watu ili waweze kujiokoa wao wenyewe toka katika dhambi kwa haki yao binafsi. Pasipo kuiamini injili ya maji na Roho kuwa ni haki ya Mungu, basi hakuna hata mmoja anayeweza kuipokea haki hii hata kama mtu huyo anaikiri imani yake katika Yesu (Yohana 3:1-8).
Ubatizo ambao Yesu aliupokea na damu ambayo aliimwaga Msalabani vimefanyika kuwa haki ya Mungu. Hii ndiyo sababu Yesu amefanyika kuwa ni mwamba uangushao kwa wale wanaoifuata haki yao binafsi. Kwa hiyo, waamini katika Yesu ni lazima watambue kuwa wanapoifuata haki yao wenyewe basi wanakuwa wakiikanyaga haki ya Mungu. Hakuna mwenye dhambi anayeweza kuingia katika Malango ya Mbinguni pasipokuwa na imani katika haki ya Mungu. Sisi ambao tunamwamini Yesu ni lazima tupokee ondoleo la dhambi zetu kwa kuamini katika haki ya Mungu. 
Yesu Kristo, ambaye alikuja hapa duniani ni Mwokozi wa wenye dhambi na yeye ndiye haki ya Mungu. Ni lazima tuamini kwa kweli katika haki hii ya Mungu kwa kuwa Yesu amezisamehe dhambi zetu kwa Neno lake la maji na Roho. Wale wanaomwamini Yesu ni lazima waamini katika ubatizo ambao aliupokea toka kwa Yohana na damu yake Msalabani kuwa ndiyo haki ya Mungu. Ni wale tu wanaoamini katika Neno lililoandikwa la maji na Roho ndio wanaoweza kuingia Mbinguni. 
 

Tunaambiwa Kujigawa Kuwa Katika Vyombo vya Ghadhabu na Vyombo vya Rehema
 
Bwana alisema, “Kwani atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” (Mathayo 16:26). Ikiwa mtu ataupoteza uzima wa milele, basi mafanikio yake hapa duniani yatakuwa hayana maana hata kama yatakuwa ni makubwa kiasi gani. Pia haitakuwa na maana kwa mtu ambaye ameiteka dunia nzima au ulimwengu mzima halafu mtu huyo akawa hajaipokea haki ya Mungu kwa kuamini katika ubatizo wa Yesu na damu yake Msalabani. 
Haijalishi kuwa mafundisho ya kitheolojia yamefundishwa kwa kiwango gani; ukweli utabaki kuwa mtu anaweza kuipokea haki ya Mungu kwa kuiamini injili ya maji na Roho ambayo inaitimiza haki ya Mungu. Waamini wanaomwamini Yesu wanaweza kuwekwa huru toka katika dhambi zao pale wanapoipokea haki ya Mungu na kuiamini. 
Siku hizi, ni jambo la kawaida kuwaona waamini ambao wanadai kuamini katika haki ya Mungu wakiwa wananung’unikia dhambi zao kila asubuhi na mapema katika mikutano ya maombi. Kwa kweli watu wa jinsi hiyo hawaiamini kikamilifu haki ya Mungu. Ni lazima tutambue kuwa imani ya jinsi hiyo inayotajwa na wale ambao hawauamini ukombozi wa Mungu ndani ya haki yake, haimpendezi Mungu na badala yake inamkasirisha Mungu. Watu wa jinsi hiyo wanaweza kubakia katika ujinga wao kwa kuwa waligeuka na kuwa kinyume na Mungu. 
Yohana 3:5 inatueleza sisi kuwa, “Mtu asipozaliwa kwa maji na kwa Roho, hawezi kuuingia ufalme wa Mungu.” Hii ndiyo sababu unapaswa kuyatatua matatizo yako yote ya dhambi kwa kuamini katika injili ya maji na Roho na katika haki ya Mungu. Injili ya maji na Roho imefanyika kuwa haki ya Mungu ambayo inaweza kukupatia ondoleo la dhambi na kukupatia haki yake. 
Ikiwa unapenda kuwa na aina ya imani ambayo inaweza kukuhesabia haki mbele ya haki ya Mungu, basi ni lazima ufuate na kuamini katika Neno la maji na Roho ambalo lina hiyo haki ya Mungu. Pia ni lazima utambue kuwa ili moyo wako uweze kujazwa na imani katika haki ya Mungu unapaswa kuiachilia mbali haki yako binafsi. Kile ambacho Paulo anawaeleza Waisraeli na Wamataifa ni kwamba ikiwa wanataka kuipata haki ya Mungu basi ni lazima waache kuifuata haki yao binafsi. 
Mungu alimpatia Ibrahimu mtoto wake kama matokeo ya imani yake katika haki ya Mungu. Haki ya Mungu inaonekana katika Neno la maji na Roho. Yeyote anayeamini katika Neno la haki anafanyika kuwa mtu mwenye haki. Mke wa Isaka, aliyeitwa Rebeka, alipata mimba ya mapacha kwa msaada wa Mungu, na hata kabla mapacha hao hawajazaliwa na kabla hawajatenda jambo zuri au baya, Rebeka aliambiwa kuwa “mkubwa atamtumikia mdogo.” Kutokana na kifungu hiki baadhi ya watu walihitimisha kuwa Mungu si Mungu wa haki na kwamba hili ni hitimisho lenye makosa. 
Hii ni kwa sababu Mungu alikwisha zifahamu tangu kabla imani za baadaye za Yakobo na Esau walipokuwa wangali katika tumbo la mama yao. Siri ya haki ya Mungu imefichwa katika injili ya maji na Roho. Kwa kuwa Esau alikuwa ni mtu mwenye majivuno ya matendo yake mema, basi Mungu alimwona ya kuwa ni mtu asiye na lolote la kufanya kuhusiana na imani katika haki ya Mungu, na hii ndiyo sababu Mungu alimchukia. Kwa upande mwingine, Yakobo alikuwa ni mtu aliyeamini katika haki ya Mungu na alimpatia Mungu utukufu wote; hivyo Mungu hakuweza kufanya lolote zaidi ya kumpenda. 
Kwa hiyo kule kusema kuwa Mungu alimpenda Yakobo na akamchukia Esau kunatokana na msingi wa kweli. Mungu hawezi kuwakubali watu kama Esau ambao wanajidaia nguvu zao na pasipo kuamini katika haki ya Mungu, lakini Mungu anapendezwa na watu kama Yakobo ambao wanayafahamu mapungufu yao na wanaoamini katika haki ya Mungu. 
Mara nyingi watu wanaielewa vibaya haki ya Mungu kwa kujiuliza kuwa kwa nini Mungu amtendee hivyo Isaka. Wanafikiri kuwa ikiwa Mungu aliwapenda baadhi na kuwachukia baadhi, basi ni lazima Mungu ana tatizo, na kwa sababu wanaweza hata kukataa kumwamini Yesu Kristo kwa sababu watamfikiria Yesu kuwa ni Mungu asiye na haki. 
Lakini inawezekanaje kwa Mungu kutokuwa na haki? Ikiwa mtu anafikiri kuwa Mungu si wa haki basi huo ni uthibitisho wa wazi kuwa mtu wa jinsi hiyo haifahamu haki ya Mungu kiusahihi. Zaidi ya yote, wale wasioamini katika haki ya Mungu hupenda kuifunika haki ya Mungu kwa haki yao binafsi jambo ambalo ni kosa kubwa mbele za Mungu. Kila mtu ni lazima atupilie mbali haki yake binafsi mbele ya haki ya Mungu na aamini katika Neno la injili ya maji na Roho. 
Na hii ndiyo njia pekee, yaani kuamini katika Neno la ukombozi ambalo lina haki ya Mungu. Kufikiri kuwa Mungu si wa haki ni matokeo ya fikra zako binafsi, zinazotokana na ujinga wako wa kutolifahamu dhumuni pana la Mungu ambalo limewekwa katika mpango wake na kuchaguliwa tangu asili. Mpango wa haki wa Mungu ulilenga katika kuifunua haki yake kwetu. Kwa kuwa Mungu alifahamu habari za mbele za wale mapacha, basi Mungu alipanga kama alivyofahamu katika haki yake kumpenda yule ambaye aliamini. 
Ni lazima tuifahamu na kuiamini haki ya Mungu katika mpango mzima wa Mungu. Kati ya Yakobo na Esau ni nani ambaye Mungu atamwita? Bwana wetu alisema kuwa Yeye “hakuja kuwaita wenye haki bali wenye dhambi.” Kwa maneno mengine haki ya Mungu inawaita watu kama Yakobo. Kama ilivyokuwa kwa Esau, si kwamba tu alikataa kuuitikia wito wa Mungu bali pia alionyesha kujivunia haki yake. Hii ndiyo sababu Esau alichukiwa wakati Yakobo akafanyika kuwa yule aliyeuitikia wito wa haki ya Mungu. 
Kweli hizi zote za kibiblia ni lazima zifahamike ndani ya imani inayofahamu na kuamini katika upendo wa haki ya Mungu. Ikiwa mtu anataka kulitatua fumbo la kuchaguliwa tangu asili la Mungu pasipo kuwa na ufahamu sahihi upendo wa haki ya Mungu, basi mtu wa jinsi hiyo anaweza kuangukia katika mtego huo ambao yeye mwenyewe amejiwekea ambao utamwongoza kwenda katika maangamizi yake binafsi. 
Mungu alipanga kuchaguliwa tangu asili ili kuufunua upendo wa Mungu na haki yake. Yakobo alikuwa ni mtu aliyeyatambua mapungufu yake na aliliamini Neno la haki ya Mungu. Hivyo kule kusema kuwa Mungu alimpenda Yakobo na akamchukia Esau ni haki. Mbele ya haki ya Mungu, kila mtu anastahili ghadhabu yake, lakini Mungu ametupatia ukombozi wake kwetu sisi na kwa wote wanaoamini katika haki yake. Wale ambao wamefunikwa katika rehema za Mungu ni wale ambao hawajivunii haki yao binafsi, na ni wale ambao wanaamini katika haki ya Mungu kama msingi wa ukombozi wao. Hawa ni watu ambao wanakiri hivi, “Ninastahili kuhukumiwa adhabu huko kuzimu kwa sababu ya dhambi zangu. Bwana Mungu, nirehemu mimi, na unifundishe mimi haki yako.” 
Mungu anatoa ondoleo la dhambi kwa wale tu wanaoamini katika haki yake yenye upendo, na huu ndio mpango wa Mungu kwetu ambao amekwisha ufunua kwamba tufanyike kuwa watoto wa Mungu. Hupaswi kuuelewa vibaya mpango wa Mungu wa kumpenda Yakobo na kumchukia Esau. Ikiwa kwa namna yoyote ile hujaielewa vizuri haki ya Mungu, basi sasa ni wakati wako kuamini tena katika upendo wa haki ya Mungu katika haki ya Mungu. 
Ninaamini katika haki ya Mungu. Wale ambao wanaweza kuelewa kwa usahihi juu ya upendo wa haki ya Mungu ndio hao wanaoweza kuyaamini majaliwa ya haki ya Mungu ndani ya haki ya Mungu kwa usahihi kabisa. Lakini kuna watu wachache sana katika ulimwengu huu walio na uelewa sahihi wa mpango wa haki ya Mungu na wanaoiamini haki hiyo, na wengi wao wamepigwa mapigo kwa sababu ya kumwelewa Mungu vibaya. 
Watu hawa wanafikiri kuwa, kwa kuwa maandiko yanatueleza kuwa Mungu alimchukia Esau, basi inawezekana kuwa baadhi ya watu wamekwishatengwa na Mungu ili wachukiwe na Mungu, kana kwamba ni majaliwa yao kuchukiwa na Mungu. Lakini Mungu wetu si Mungu dikteta kiasi hicho. Mungu ni hakimu ambaye yuko sahihi na mwenye haki katika haki yake. Mungu anapenda kumpatia kila mmoja wetu haki yake, rehema na upendo. 
Mungu alipenda kutupatia haki yake kwa kupitia Yesu Kristo, na aliwafunika wote walioamini katika haki yake katika rehema zake na akawafanya kuwa watoto wake. 
Jambo hili linafunuliwa katika Agano Jipya katika Mathayo 9:12-13 ambapo Yesu anasema, “Naye aliposikia, aliwaambia, wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi. Lakini nendeni, mkajifunze maana yake maneno haya, Nataka rehema, wala si sadaka; kwa maana sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi.” Wale walio na afya hawahitaji tabibu na wanaweza kuwafikiria matatibu kama watu wanaoudhi. Kama ambavyo watu hawaufahamu umuhimu wa tabibu wanapokuwa na afya, ndivyo ambavyo watu hawaufahamu umuhimu wa kuipokea haki ya Mungu katika mioyo yao kwa kuiamini haki ya hiyo. Watu hao wanaendelea kuifuata haki yao binafsi pasipo kuifahamu haki ya Mungu. 
Lakini wenye dhambi ni lazima waiache haki yao wenyewe na waamini katika haki ya Mungu. Unaweza ama kuwa Yakobo au kuwa Esau mbele za Mungu. Je, unapenda kuwa nani? Taji ya Mungu na adhabu itategemea uamuzi wako wa kuamini au kutokuamini katika ukombozi wa haki ya Mungu. 
 

Mungu Hana Tatizo
 
Kwa asili kila kiumbe kina ile asili ya ushindani. Baadhi ya watu wanaweza kuwa na akili sana na kuwa na mafanikio na wengine wanaweza kuwa wamefanya matendo mema kwa wengine. Lakini pasipo uelewa na imani katika haki ya Mungu, watu wa jinsi hiyo hawataweza kupata kibali cha Mungu. Mbele za Mungu, kila mtu, mimi na wewe, hata Waisraeli walipaswa kuangamia kuzimu. Pamoja na hali hiyo, tumehesabiwa haki si kwa juhudi zetu au matendo yetu au nguvu zetu, bali tumehesabiwa haki kwa imani katika haki ya Mungu. 
Kwa kuwa Mungu bila ubaguzi na kwa haki amempatia kila mtu upendo wake wa haki, basi wale wote wanaoamini katika upendo wa haki ya Mungu wanaweza kuokolewa toka katika dhambi zao zote. Mungu si Mungu asiye na haki kama ambavyo unaweza kuwa umewahi kumfikiria. 
Kwa mtu kupokea baraka ya Mungu ya ukombozi kunategema ikiwa mtu huyo ameamua kuipokea haki ya Mungu au la. Hii ndio sababu baadhi ya watu wamefanyika kuwa ni vyombo vya ghadhabu na wengine wamefanyika kuwa ni vyombo vya rehema. Tunaweza kusema kuwa Yakobo alifanyika kuwa chombo cha rehema wakati Esau akifanyika kuwa ni chombo cha ghadhabu. 
Lakini mara nyingi baadhi ya watheolojia na wale wasio na Roho Mtakatifu humkashifu Mungu. Wao husema, “Tazama, je, Mungu hakumfanya Farao kuwa chombo cha ghadhabu? Hebu mwangalie Yakobo na Esau! Hebu mwangalie Rebecca! Hebu angalia yale ambayo mfinyanzi ameyafanya! Je, si kweli kuwa Mungu alimfanya mtu fulani kuwa chombo cha kuheshimiwa tangu zamani? Kwa kweli haya ni majaliwa tu!” Ufahamu wao unajengwa katika maelezo yafuatayo: baadhi ya watu walikwishachaguliwa kuwa watoto wa Mungu hata kabla ya kuzaliwa kwao; na watu wa jinsi hiyo ambao walikwishachaguliwa tangu asili ili kuvikwa upendo wa Mungu wanafanyika wote kuwa watoto wa Mungu wakati wengine wakifungwa kuzimu. Hivi ndivyo uchaguzi wa Mungu unavyopigwa vita. Lakini ukweli ni kuwa Mungu aliitoa haki yake kwa kila mtu na bila ubaguzi anawachagua wale ambao wanaiamini haki ya Mungu. 
Tulihesabiwa haki kwa kuamini katika haki ya Mungu wakati ambapo hatukuwa watu wake. Mungu anaweza kuikubali na kuithibitisha imani yetu kwa sababu tulihesabiwa haki kwa kuamini katika injili ya maji na Roho kwa kupitia Neno lake. Huu ndio ukweli wa injili unaoinyesha nguvu ya kushangaza ya Mungu. 
Kwa asili, sisi hatukuwa na Mungu ndani yetu, hatukumfahamu Mungu, na tulikuwa ni wenye dhambi, lakini sisi tumefanyika kuwa watu wake kwa kuamini katika haki ya Mungu. Injili ya maji na Roho, ambayo kwa hiyo tunaamini, si injili isiyo kamilifu, bali ni injili kamilifu kabisa. Tunapaswa kumsifu Mungu kwa kutupatia ukweli ambao kwa huo tunaweza kuipata haki yake. 
Maisha yetu yanaweza kuwa na matatizo mengi, lakini hatupaswi kuisahau haki ya Mungu kwa sababu Mungu ametufundisha sisi juu ya ukuu wa nguvu zake. Mtu mwenye furaha zaidi kuliko watu wote katika ulimwengu mzima ni yule anayeifahamu haki ya Mungu. Kwetu sisi tunaomwamini Mungu, basi Mungu utatu ni Baba wa rehema. Yeye ni Mungu wetu mtakatifu. Mungu anaiweka imani katika haki ya Mungu katika nafsi zetu sisi tunaoamini na kuamini katika haki ya Mungu. Sisi tulifanyika kuwa watoto wa Mungu na wapokeaji wa baraka zake kwa kufahamu na kuamini katika haki ya Mungu. 
Lakini kuna watu wengi ambao bado wametingwa na juhudi zao binafsi katika kutenda matendo mema. Wakitoa matoleo ya sadaka, wakijitolea katika kazi za kanisa, wakitoa michango mikubwa hali wakishindana na wengine, bila shaka unaweza kufikiria kuwa haya yote ni matendo mema, lakini matendo hayo pekee hayawezi kukuokoa. Kuwekea mkazo katika matendo haya pekee si ishara ya imani yako katika haki ya Mungu, bali ni ishara kuwa unaifuata haki yako binafsi. Wale waliotingwa na juhudi za miili yao binafsi wanakwenda kinyume na Mungu. Watu wanaotingwa na vitu kama hivyo vya mwili ni wale ambao hawaifahamu haki ya Mungu. 
Maandiko yanatueleza kuwa wokovu wa Mungu hautolewi kwa wale ambao wanaukimbilia, bali ni kwa wale ambao wanaiamini haki ya Mungu. Haki hii inaweza kupokelewa kwa kumwamini Mungu wetu mwenye rehema. Sisi hatupendwi na Mungu kwa sababu ya matendo yetu, bali tunaupokea upendo wake wa rehema kwa kuamini katika haki yake. Hii ndiyo sababu imani ya kweli inategemea ikiwa tunafahamu au hatufahamu na ikiwa tunaamini au hatuamini katika haki ya Mungu. 
Je, sisi hatukuwa viumbe tusio na faida toka zamani? Lakini je, hatujafanywa kuwa wa ukoo wa kifalme kwa sababu ya imani yetu katika haki ya Mungu? Tunaweza kuishika imani yetu hadi mwisho kwa kuamini katika haki ya Mungu na kuona fahari kutokana na ule ukweli kuwa sisi tumefanyika kuwa watoto wa Mungu. 
Kuna watu wengi hapa ulimwenguni wanaofanya maovu na kudai kuwa hakuna Mungu, lakini Mungu anatuonea huruma kwa kuwa tumeamini katika haki yake. Sisi ni waheshimiwa mbele za Mungu na fahari yetu katika Mungu inatunzwa vizuri. Tunapokuwa hapa duniani tunaweza kukutana na majaribu na mapigo, lakini ukweli ni kuwa sisi ni matajiri wa kiroho na wenye furaha. Sisi sote ni lazima tuifuate haki ya Mungu na tumwinue Yesu. 
Mungu aliwafanya wenye dhambi wote kuwa watoto wake, kuwa wenye haki, na kuwa wakamilifu mbele zake. Ni lazima tutambue kuwa haki ya Mungu inakuja kwa ajili ya akina nani. Haki hii ya Mungu imeyakamilisha mapungufu yetu yote na imesafishia mbali uchafu wetu wote wa dhambi. Kuamini katika ukweli huu au kutoamini kunategemea wewe mwenyewe. Wewe pia, umeokolewa kikamilifu toka katika dhambi zako kwa haki ya Mungu. Je, sasa utafanya nini? Je, utaahirisha maamuzi yako ya kuamini kesho? 
Haki ya Mungu na iwe pamoja nawe.