Search

Mahubiri

Somo la 9: Warumi (Maoni juu ya Kitabu cha Warumi)

[SURA YA 16] Salimianeni

Katika utangulizi wake, Mtume Paulo aliwaambia watakatifu waliokuwapo Roma na kwetu sisi kwamba tunapaswa kusalimiana. Je, ni nani tunayeweza kumsalimia kwa moyo wote katika Bwana katika kipindi hiki? Kwa kweli tunaweza kuwasalimia watumishi kwa furaha na waamini wanaolihubiri Neno la Mungu katika ulimwengu mzima. Tunaweza kuwa na ushirika na wale waliookoka kwa kuvisoma vitabu vya injili ya maji na Roho. Sisi pia tuna makanisa, waamini, na watumishi wa Mungu ambao tunaweza kusalimiana nao katika Kristo. 
Kwa kuwa si kila mtu anaamini katika injili ya maji na Roho, basi wenye haki hawawezi kumsalimia kila mtu. Hakuna watu wengi hapa duniani ambao tunaweza kuwasalimia kwa furaha. Ni jambo la kujutia kuona kuwa kuna watu wachache ambao wanaamini katika injili ya maji na Roho ambao tunaweza kuwasalimia na kuwa na ushirika nao katika imani moja. Hatuwezi kuwa na ushirikiano na wenye dhambi ambao wanajifanya kuwa ni watumishi wa Mungu katika makanisa ya kidunia. 
Kama ambavyo dhambi na Roho Mtakatifu haviwezi kukaa pamoja, basi vivyo hivyo wenye dhambi na wenye haki hawawezi kusalimiana. Wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho wanaweza kutoa ibada ya kiroho kwa Mungu na wanafanya kazi kwa mambo ya kiroho. Lakini wenye dhambi ambao bado hawajapokea ondoleo la dhambi zao wanajaribu kuokolewa kwa kuitunza na kuishika Sheria ya Mungu, na kwa sababu hiyo hawawezi kuwa na ushirika wa kiroho pamoja na wenye haki. Kama ambavyo hayawani pamoja na binadamu wasivyoweza kuongea pamoja, vivyo hivyo, wenye haki hawawezi kuwa na ushirika wa kiroho pamoja na wenye dhambi. 
Tunaweza kuona kuwa watu ambao Paulo alikuwa na ushirika nao wa kiroho walikuwa ni watu waliokuwa na imani kama yake. Tunafahamu kuwa ikiwa mtu alikuwa na ushirika wa kiroho pamoja na Paulo, basi inamaanisha kuwa Paulo aliikubali imani ya mtu kama huyo. Hivyo, nikafikiria, “Ikiwa leo hii nitaelekea katika mkoa fulani, basi ni nani ambaye nitapaswa kumtembelea na kumsalimia?” Nina hakika nitatembelea Kanisa la Sokcho ikiwa nitakuwa nimekwenda Sokcho au Kanisa la Gangneung ikiwa nitakuwa nimetembelea Gangneung. Ninaweza kuonana na watumishi wa Mungu na waamini, tukawa na ushirika na kuumega mkate pamoja. Pia ninaweza kutembelea nyumba ya kaka zangu na dada zangu waliopo pale na kuwasalimia. Lakini watu ambao ninaweza kuwasalimu ni wale tu ambao wanaamini katika injili ya maji na Roho, na wale ambao tunaweza kushirikiana imani moja katika Roho Mtakatifu. 
Tunaweza kuona jinsi walivyobarikiwa wale ambao imani yao imethibitishwa na Paulo. Kwa kweli ni jambo la kufurahisha kuona kuwa tuna injili ya maji na Roho inayotusaidia kuthibitisha imani ya kila mmoja wetu na inayotusaidia kusalimiana. Je, una imani katika injili ya maji na Roho inayokufanya usalimiane na waamini wengine? Je, unaweza kukiri kwa uaminifu bila mashaka kwa Mungu kuwa hauna dhambi yoyote ile? 
Nilipata nafasi ya kuwasalimia wapendwa waamini huko China wakati nilipotembelea huko. Nilimtembelea ndugu mmoja ambaye alikuwa anaishi katika kingo za Mto Heran. Basi mara tulipoamka asubuhi iliyofuata, ndugu huyo aliaanda kifungua kinywa cha kutosha. Tulikaa katika meza kubwa ya mviringo, kwa namna ile ambayo tulizoea kukaa katika familia pana, na tukawa na ushirika mzuri pamoja na waamini mahali pale. Pia kulikuwepo na mwinjilisti katika mji wa jirani ambaye alikuwa na shauku sana ya kutuona. Kwa hiyo tulimtembelea na kuwa na ushirika pamoja naye pia. Tunaweza kumsalimia yeyote anayeamini katika injili ya maji na Roho. 
Ikiwa ningekuwa nimeitembelea Marekani, ni mahali gani basi ambapo ningeweza kwenda? Ningelimtembelea Mchungaji Samuel Kim na mke wake huko Flushing, New York. Pia ningelitembelea Kanisa la Maisha Mapya ili kuonana na kaka na dada zetu. Pia huko Urusi kuna kanisa la waliozaliwa tena upya ambalo nililitembelea miaka michache iliyopita. Huko Japan, ningependa kuitembelea nyumba ya Mashemasi wa kike ya Soon-Ok Park iliyoko Tokyo. 
Sisi ni wenye haki ambao tumeokolewa kwa imani yetu katika injili ya maji na Roho. Sisi hatukuokolewa kama matokeo ya utimilifu wa miili yetu, bali kwa sababu ya haki ya Mungu ambayo tumeipokea kwa kupitia imani yetu katika injili ya maji na Roho. 
Kama unavyoweza kuona, kuna watu ambao wametengwa ili wenye haki waweze kuwasalimia kama ambavyo Paulo alivyokuwa na orodha ya watu wa kuwasalimia huko Roma katika sura ya 16. Kama Paulo alivyofanya, sisi pia hatuwezi kumsalimia kila Mkristo kwa sababu si wote walio na imani sahihi, isipokuwa ni kwa wale tu wanaoifahamu na kuiamini haki ya Mungu. Sisi hatuwezi kufanya lolote zaidi ya kumsifu Mungu kwa kutupatia imani ambayo kwa hiyo twaweza kusalimia na kusalimiwa. 
 

Paulo Alituonya Sisi Kukaa Mbali na Watu Hawa 
 
Ukianzia aya ya 17, onyo la pili ambalo Paulo analitoa kwetu ni kukaa mbali na wale ambao wanayatumikia matumbo yao tu. “Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao. Kwa sababu walio hivyo hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali matumbo yao wenyewe; na kwa maneno laini na ya kujipendekeza waidanganya mioyo ya watu wanyofu” (Warumi 16:17-18). Wapo wale ambao hawamtumikii Kristo bali wanayatumikia matumbo yao wenyewe. Hao ndio wale ambao wanaleta machafuko miongoni mwa waamini na wanawadanganya wanyofu kwa maneno laini na kauli za kujipendekeza. Hatupaswi kuwasalimu watu wa jinsi hiyo bali tunapaswa kukaa mbali nao. 
Paulo alituonya sisi kukaa mbali na watu wa jinsi hiyo, kwa kuwa wao hufurahia kusababisha vurugu ndani ya kanisa, na kuwachanganya wale ambao wanamwamini Mungu kwa kweli hali wakiwakusanya wanyofu ili waweze kujilisha kwa sababu ya tamaa yao. Viongozi potofu wa Kikristo kama hao wanajaribu kuwafungia watu chini ya dhambi kwa kuwafundisha wafuasi wao kuiheshimu na kuifuata Sheria kikamilifu. Kazi yao ni kuyajaza matumbo yao kwa jina la Yesu na kuwapotosha wakweli na wenye haki. Hakuna haja kwa sisi kuwasalimia watu kama hao kwa kuwa wao wapo katika huduma kwa ajili ya kuyalisha matumbo yao tu. 
 

Injili ya Maji na Roho Ni Lazima Ienezwe Kwa Mataifa Yote!
 
Tatu, Paulo alizungumzia juu ya hitaji la kuieneza injili kwa mataifa yote. Aya ya 26 inasema, “Ikadhihirishwa wakati huu kwa maandiko ya manabii, ikajulikana na mataifa yote kama alivyoamuru Mungu wa milele, ili waitii imani” Injili ya maji na Roho ambayo Paulo aliihubiri ni injili ya kweli ambayo mataifa yote wanapaswa kuiamini na kuitii. Kwa kweli ni bahati mbaya tu kuwa maeneno mengi ambayo Paulo alipanda makanisa pamoja na wale walioiamini injili ya maji na Roho yamekuwa ni maeneo ya kiislam. 
Kwa wakati huo, Paulo alikwenda katika maeneo haya na akawaweka viongozi wa kanisa kutoka miongoni mwa waamini waliokuwa wakiiamii injili ya maji na Roho ambayo ina haki ya Mungu. Ilikuwa ni sawa na jinsi tunavyowatuma watenda kazi katika kanisa letu baada ya kuwa wamefundishwa katika shule yetu ya utume. Pamoja na kuwa makanisa hayo kwa wakati huo yaliitunza na kuishika imani katika “Bwana mmoja, imani moja, ubatizo mmoja” (Waefeso 4:5), walishindwa kuiendeleza imani yao katika injili kwa kuwa hawakuiandika injili hiyo katika maandishi. 
Kwa sasa tupo katika mchakato wa kuvitafsiri vitabu vyetu katika lugha ya Kituruki. Mtu mmoja toka Uturuki aliguswa na matoleo yetu ya kiingereza na akajitolea kutafsiri matoleo hayo. Sasa tunaanza kuihubiri injili ya maji na Roho katika eneo ambapo Paulo mwenyewe aliwahi kuihubiri injili na akapanda makanisa ya Mungu. Sisi tunaihubiri injili moja ambayo Paulo aliihubiri katika eneo lilelile alilolipitia. Injili ambayo Paulo aliihubiri ni injili ya maji na Roho inayoweza kuyaokoa mataifa yote iwapo wataiamini na kuiheshimu. 
Katika sura ya mwisho ya Warumi, Paulo aliwaambia watakatifu huko Roma kusalimiana, kukaa mbali na wale ambao wanayajaza matumbo yao tu, na kuieneza injili ya maji na Roho kwa mataifa yote. 
 

Injili ya Maji na Roho Itatuimarisha 
 
Kitu cha nne ambacho Paulo alikitaja ni kwamba injili hii ya maji na Roho ni hekima ya Mungu ambayo itatuimarisha. “Sasa na atukuzwe yeye awezaye kuwafanya imara, sawasawa na injili yangu na kwa kuhubiriwa kwake Yesu Kristo, sawasawa na ufunuo wa ile siri iliyositirika tangu zamani za milele, ikadhihirishwa wakati huu kwa maandiko ya manabii, ikajulikana na mataifa yote kama alivyoamuru Mungu wa milele, ili waitii imani. Ndiye Mungu mwenye hekima peke yake. Utukufu una yeye kwa Yesu Kristo milele na milele. Amina.” (Warumi 16:25-27). Ni jambo gani ambalo lingaliwaimarisha watakatifu pale Roma? Ni injili ya Paulo ya maji na Roho ndiyo ambayo ingaliwaimarisha watakatifu pale Roma. Injili hii pia ni hekima ya Mungu. 
Katika injili ambayo Mungu ametupatia katika hekima yake. Injili hii ina nguvu ya kuzichukulia mbali dhambi zote hata za wale waliojawa na mapungufu. Hata kama watakuwa na mapungufu na udhaifu kiasi gani, wale wanaoamini katika injili ya maji na Roho sio tu kwamba wanafanywa wasio na dhambi bali pia wanafanywa kuwa wahubiri wa injili hii. Ni hekima ya Mungu tu na injili ya maji na Roho inayotoka ndani ya hekima hiyo ndivyo vinavyoweza kutufanya sisi kuwa viumbe wakamilifu. Kwa kweli hakuna ukweli zaidi ya injili hii ambao unaweza kuziimarisha nafsi zetu, mioyo yetu, fikra na miili yetu. 
Paulo hakuiita injili hii kwa wazi au kwa ufupi kama “injili,” bali aliita “injili yangu.” Injili ambayo Paulo aliihubiri ilikuwa ni injili ya maji na Roho iliyofunuliwa katika Agano la Kale na Agano Jipya. Injili hii ya maji na Roho inajengwa katika injili iliyofunuliwa kwa kupitia manabii katika Agano la Kale na kutimizwa na Yesu Kristo katika Agano Jipya. Hii ndiyo sababu Paulo alisema kuwa ‘injili yake’ ilidhihirishwa kwa mujibu wa ufunuo wa fumbo la imani ambalo lilikuwa limefichwa katika Maandiko ya unabii. 
Injili ambayo Paulo aliihubiri ilibeba maana yake toka katika utaratibu wa sadaka ya kuteketezwa katika vitabu vya Torati katika Agano la Kale, hasa katika kitabu cha Mambo ya Walawi, na ilitimizwa na Yesu Kristo katika Agano Jipya kama haki ya Mungu kwa kupitia ubatizo wake, kifo chake Msalabani na ufufuo wake. Hii ndiyo sababu Paulo aliutoa utukufu wote “kwake Yeye anayeweza kuwaimarisha kulingana na injili yake.” 
Injili ya maji na Roho inawaimarisha watakatifu na watumishi wa Mungu. Kwa kupitia injili hii, imani yetu, nafsi zetu, fikra na mawazo yetu, na miili yetu inaimarishwa. Imani yetu inaweza kuimarishwaje? Ni nini kinachotufanya tusimame imara wakati wote wakati sisi ni wadhaifu? 
Imani yetu inakuwa imara zaidi na zaidi kwa kuwa tumepokea wokovu wa Kristo, ambaye alizichukulia mbali dhambi zetu zote kwa kupitia ubatizo wake na damu yake iliyomwagika Msalabani. Tunaweza kusema kuwa hatuna dhambi mbele za Mungu kwa sababu mioyo yetu haina kitu cha kukionea aibu tena, na kwa sababu ya imani hii ya kiroho isiyo na aibu tunaweza kuieneza injili ya maji na Roho kwa wale ambao bado wamefungwa katika dhambi. 
 

Maonyo ya Mwisho
 
Paulo anaimalizia sura ya 16 kwa maombi ya kufunga akisema, “Ndiye Mungu mwenye hekima peke yake. Utukufu una yeye kwa Yesu Kristo, milele na milele. Amina.” Ni kitu gani ambacho kinamtukuza Mungu zaidi? Kuihubiri haki ya Mungu katika Yesu Kristo kunamtukuza Mungu zaidi. Sisi pia tunatukuzwa wakati tunapoitumikia injili kwa mioyo yetu yote. 
Mambo muhimu ya ujumbe wa Paulo katika Warumi sura ya 16 ni haya: salimianeni, kaeni mbali na wale wanaoyajaza matumbo yao, eneza injili kwa mataifa yote. Hili lilikuwa ni onyo la mwisho ambao Paulo alilipatia kanisa huko Roma. Injili ya maji na Roho ambayo Paulo aliihubiri ina nguvu ya kutuimarisha katika kila namna. Hivi ndivyo tunavyoamini. Imani katika injili ya maji na Roho ni sawa na imani ambayo mitume walikuwa nayo katika Biblia na ndiyo ile ambayo kanisa letu linaamini hata sasa. 
Je, unajisikia ule usawa au kule kufanana? Kwa kweli huwa ninashangazwa kila ninapoisoma Biblia na kutambua kuwa tuna imani moja kama ambayo watu wakuu katika Biblia walikuwa nayo miaka elfu mbili iliyopita. 
Je, umewahi kuwafikiria watu wangapi ambao tunashirikiana injili kila siku? Kwa kweli tunashirikiana injili na watu wasiopungua elfu mbili kila siku. Hii elfu mbili itazidi na kufikia elfu kumi muda si mrefu ikiwa watakatifu waliozaliwa upya katika kila taifa wataihubiri injili hii kwa majirani zao na watu hao elfu kumi nao wakiwashirikisha wengine injili basi itakuwa elfu ishirini. Kama unavyoweza kuona, kuihubiri injili katika ulimwengu mzima si jukumu ambalo haliwezekani kabisa. 
Kwa kweli, suala la msingi kuhusiana na vitabu vyetu vya injili ya maji na Roho ni kwamba vitabu hivyo visipotee bali vitunzwe na kwamba maana yake isibadilishwe bila kujalisha kuwa ni watu wangapi wanasoma vitabu hivyo. Mahali palipo na kitabu ambacho kina injili ya maji na Roho, basi ni hakika kuwa watu wengi watakiazima na kukisoma na injili ya Mungu itaenezwa. Kwa kweli siku ambapo injili hii itaufikia ulimwengu mzima haipo mbali sana. 
Haki ya Mungu ambayo umeipata kwa kupitia imani yako ni injili ya maji na Roho ambayo hata wale waliopo katika nchi zilizoendelea hawaifahamu. Injili ya kweli ambayo tunataka kushirikiana na ulimwengu mzima ni fumbo ambalo halijulikani katika ulimwengu huu, na kwa sababu hiyo tuna shauku ya kutaka kuifunua siri hii ya wokovu kwa wale wote ambao wamelowekwa katika dhambi zao. Haki hii ya Mungu inayoonyeshwa katika injili ya maji na Roho ni ya wazi kabisa kiasi kuwa yeyote anayeipokea injili hii atamtolea Mungu shurani na kumrudishia utukufu. 
Watu wengine wanaona kuwa ni kitu cha kuchosha tunaporudia rudia kuzungumza juu ya injili ya maji na Roho. Lakini haijalishi kuwa tunairudia mara ngapi, ukweli unabaki kuwa injili hiyo inaifurahisha mioyo na nafsi zetu. Kwa kuwa kuna Wakristo wengi sana ambao bado wamefungwa katika dhambi, basi sisi tunaendelea tena na tena kuihubiri injili ya maji na Roho kwa ulimwengu mzima. Kwa kuwa injili hii ndiyo injili halisi ambayo ilikabidhiwa kwetu na mitume, akiwemo Paulo, basi nafsi zote zinapaswa kuiamini injili hii. Tunahitaji kuisikiliza na kisha kuiandika injili hii ya maji na Roho katika mioyo yetu kwa sababu ni ya muhimu sana kwa kila Mkristo. 
Sisi tunashirikiana injili na zaidi ya watu elfu mbili kila siku kwa kupitia vitabu vyetu vilivyochapishwa na vitabu-pepe pamoja na tovuti. Tuna hakika kuwa ikiwa mbegu ya ukweli itaangukia katika udongo mzuri, basi kwa hakika itaweza kuzaa matunda—thelathini, sitini, au mara mia zaidi ya ile iliyopandwa. Mtu mmoja anaweza kuihubiri injili kwa dazani za watu, na kila mmoja kati ya watu hawa naye anaweza pia kuihubiri injili kwa dazani nyingine zaidi, na hivyo kuihubiri injili kwa watu wengi zaidi. 
Tunaposikia kuwa injili yetu inaenezwa kwa watu zaidi ya elfu mbili kwa siku, basi mioyo yetu inajazwa na ile haki ya Mungu. Ninamshukuru Mungu kwa kutufunulia njia kuieneza injili hii katika ulimwengu mzima. Ninaomba kuwa Mungu azidi kuziimarisha imani za watumishi wake zaidi na zaidi. 
Injili ya maji na Roho ambayo sasa inaenea katika ulimwengu mzima ni wimbi jipya la ukweli kwa wokovu. Injili hii ni njia pekee ya kupokea Roho Mtakatifu na kuingia katika Ufalme wa Mungu. Huwezi kuipata injili ya maji na Roho katika dini nyingine za kidunia hata kama utatafuta kwa nguvu kiasi gani. 
Watu ulimwenguni mwote watamshukuru Mungu kwa sababu sasa wanaweza kuamini katika haki yake kwa kupitia injili ya maji na Roho. Kila mmoja anayevisoma vitabu vyetu anaweza kushangaa, “Aah! Hivi ndivyo Yesu alivyoniokoa toka katika dhambi zangu!”, kwa kuwa hawajawahi kuisikia injili hii hapo kabla. 
Wale wanaotaka kuwekwa huru toka katika kifungo cha dhambi na wale ambao wanatamani daima kupokea Roho Mtakatifu watapokea msamaha kamili wa dhambi zao na amani ya akili zao mara watakapokuwa wameifahamu na kuikubali injili ya maji na Roho. Tangu sasa na kuendelea, injili ya maji na Roho itaenea kwa kila taifa ulimwenguni. 
Moyo wangu umejazwa furaha kwamba injili ya maji na Roho inaenea ulimwenguni kote. Pamoja na kuwa ninaitumikia injili, ninafahamu kuwa bado nina madhaifu mengi na mapungufu. Lakini kwa sababu ninaamini kikamilifu katika injili ya maji na Roho na kwa kuwa ninaifahamu haki ya Mungu, basi mara nyingi ninapokea nguvu mpya toka kwa Bwana ili kwamba niweze kuendelea kuitumikia injili yake. Kwa sasa injili imeingia katika mataifa mengi zaidi; watu wengi wamevisoma vitabu vyetu na wameshangazwa kwa mafundisho sahihi yaliyomo katika vitabu hivyo. 
Wale wanaoamini katika haki ya Mungu ulimwenguni kote ndio wale ambao wameokolewa kwa kuamini katika injili ya maji na Roho. Sababu inayotufanya tusimame wakamilifu pamoja na kuwa tuna madhaifu mengi ni kwa sababu tunamwamini Bwana wetu, ambaye ni haki ya Mungu. Sisi ni watenda kazi wa Mungu. Sisi hatuangalii kule kuyaridhisha matumbo yetu ya kimwili, bali tunalenga katika kuieneza imani ya kweli ulimwenguni mwote. Ninatumaini kuwa waamini wengi wenye haki watainuka na kwenda kuieneza injili ulimwenguni mwote. 
Kama Paulo, sisi tunaweza kuihubiri injili ya maji na Roho bila kujali kuwa ni lini Bwana wetu atakuja. Hebu tufanye kazi kwa juhudi pamoja kwa ajili ya Agizo lake la Utume. Tunapoieneza injili hadi miisho ya dunia, basi Bwana atakuja kulingana na ahadi zake na kutuchukua kwenda nyumbani. Ni lazima tusikilize kwa makini kwa yale ambayo Paulo alituonya, kwamba tusalimiane na kutiana moyo. Ingawa tunapungukiwa katika matendo yetu, ukweli ni kuwa tunaimarishwa kiroho vizuri sana kwa kupitia imani yetu katika haki ya Mungu. Hapo ndipo tunapofikia hatua ya kuona jinsi imani yetu katika injili ya maji na Roho ilivyo ya uhakika. Kwa hakika sisi ni waamini katika Bwana wetu ambao tuna haki ya Mungu kamilifu. 
Tunapouangalia ulimwengu huu kwa imani yetu katika haki ya Mungu tunaona kuwa kuna mambo mengi sana ya kufanya. Sisi sote tunaweza kuishi maisha yetu hali tukiieneza injili katika ulimwengu mzima, tukimsifu Mungu kwa imani yetu katika Kristo ambaye ndiye haki ya Mungu. 
Halleluya! Ninamsifu Bwana milele ambaye ni haki ya Mungu!