Search

Mahubiri

Somo la 10: Ufunuo (Ufafanuzi juu ya Ufunuo)

[21-2] Ni Lazima Tuwe na Imani Iliyothibitishwa na Mungu (Ufunuo 21:1-27)

(Ufunuo 21:1-27)
 
Mungu ametupatia Mbingu na Nchi Mpya. Mungu anatueleza kwamba kile unachokiona hivi sasa, yaani mbingu hii na nchi ya kwanza, pamoja na vitu vyake vyote vitatoweka, na kwamba atatupatia badala yake mbingu mpya, nchi mpya, na bahari mpya, na kisha atavifanya vitu vyote kuwa vipya katika ulimwengu mpya ulioumbwa. Hii ina maanisha kwamba Bwana Mungu atatupatia Mbingu na Nchi Mpya kama zawadi yake kwa watakatifu ambao wameshiriki katika ufufuo wa kwanza. Baraka hii ni thawabu toka kwa Mungu ambayo atawapatia wale watakatifu wake, ambao wamepokea ondoleo la dhambi. 
Hivyo, Mungu atawapatia baraka hii watakatifu walioshiriki katika ufufuo wa kwanza. Baraka hii imeruhusiwa kwa watakatifu tu, ambao kwa kuamini katika injili takatifu ya maji na Roho iliyotolewa na Yesu Kristo, wamepokea ondoleo la dhambi zao. Hivyo Bwana wetu atafanyika kuwa Bwana harusi wa watakatifu. Kuanzia sasa na kuendelea, kile kilichobakia kwa mabibi harusi ni kuvikwa ulinzi wa Bwana harusi na kuzipata baraka na nguvu zake kama wake za Mwana-kondoo, na kisha kuishi kwa utukufu katika Ufalme wake wenye utukufu. 
Kifungu hiki pia kinatueleza kwamba Mji Mtakatifu, Yerusalemu Mpya ulishuka kutoka Mbinguni. Huu haukuwa mji wa kawaida, kwa kuwa kifungu kinaeleza kwamba Mji huu ulikuwa ni mzuri sana kama vile bibi harusi alivyojimba kwa ajili ya mumewe, ukitoka toka Mbinguni. 
Mungu ameuandaa mji mtakatifu kwa ajili ya watakatifu. Mji huu ni mji wa Yerusalemu ambao ni Hekalu la Mungu. Hekalu hili limeandaliwa kwa ajili ya watakatifu wa Mungu. Pia hili lilikuwa limepangwa kwa ajili ya watakatifu pamoja na Yesu Kristo, hata kabla ya Bwana Mungu hajauumba ulimwengu huu. Hivyo, watakatifu hawawezi kufanya lolote zaidi ya kumshukuru Bwana Mungu kwa imani yao na kisha kumpatia Mungu utukufu kwa zawadi hii ya neema. 
Mambo haya yote—kwamba watakatifu wamefanywa kuwa watu wa Mungu na kwamba Yeye amefanyika kuwa Mungu wao—ni neema ambayo imetolewa na Mungu na ni zawadi ambayo watakatifu wameipokea toka kwake kwa kuliamini Neno la wokovu la maji na Roho. 
Hivyo, wale wote waliobarikiwa kuingia katika Hekalu la Bwana na kuishi pamoja naye watampatia Mungu shukrani na utukufu milele, hii ni kwa sababu Maandiko yanatueleza kwamba atayafuta machozi yao, na kwamba hakutakuwa na kifo tena, wala kilio, wala kuteseka na kwamba mambo yote ya kale yatakuwa yamepita. Pamoja na kuwa huzuni, vilio, maumivu, vifo, na majonzi vimejaa katika ulimwengu huu kwa sasa, ukweli ni kuwa katika Mbingu na Nchi Mpya mambo hayo yote yatakuwa yamepita. Wale wanaoishi katika Mbingu na Nchi Mpya iliyotolewa na Bwana hawatamwaga machozi yao tena kwa sababu ya majonzi au kulia kwa huzuni kwa sababu ya kuwapoteza wanaowapenda. 
Wakati muda wa watakatiu kuingia katika Mbingu na Nchi Mpya utakapowadia, basi mbingu ya kwanza, na nchi ya kwanza, pamoja na huzuni zake zote zitatoweka, na kwamba kitakachokuwa kikiwangojea watakatifu ni kuishi maisha yao yenye utukufu na baraka zote pamoja na Mungu katika Mbingu na Nchi Mpya milele. Wakati huo Mungu atakuwa amekwishayaondolea mbali mapungufu yote ya ulimwengu wa kwanza na atakuwa ameufanya ulimwengu huu mpya ukiwa mkamilifu zaidi. 
Kifungu kikuu cha sura ya 21 kinatueleza juu ya Mbingu na Nchi Mpya, ambavyo vitafuatia baada ya kuondolewa kabisa kwa ulimwengu huu, na hii ni baada ya kupita kwa Ufalme wa Milenia unaotajwa katika sura ya 20. Mambo yote katika ulimwengu huu hata yale yaliyo mbali sana yanahusiana na dunia hii yatakuwa yamekwisha. Wakati huo nyakati za Mpinga Kristo (Mnyama), manabii wa uongo, watumishi wake, na wale wote ambao hawakumwamini Mungu badala yake wakasimama kinyume na Mungu hapa ulimwenguni, watakuwa wamepita. Hii ni kwa sababu watakuwa wametupwa katika moto bara baada ya kufungwa kwa Ufalme wa Milenia, hivyo wakati huo wataweza kuonekana wakiwa kuzimu tu. 
Hivyo, katika sura ya 21, Mungu anatueleza juu ya Mbingu na Nchi Mpya ambayo ataitoa kwa watakatifu, mahali ambapo ni pakamilifu ambapo hakuna mwenye dhambi anayeweza kuonekana humo. Ni kama vile unapotaka kuangalia wanyama wa porini itakubidi uende katika bustani ya kufugia wanyama, basi wakati huu utakapowadia, basi yeyote anayetaka kumwona Shetani na wafuasi wake atapaswa kwenda kuzimu. 
Mahali ambapo Mungu atatupatia Mbingu na Nchi Mpya, ni mahali ambapo Bwana wetu ataishi pamoja nasi. Pia Mungu ametufanyia Mji Mtakatifu ukiwa na asili ya kupendekeza sana na bustani za kupendekeza za kijani. Wakati Mbingu na Nchi Mpya vitakapowadia, basi vitu vyote vya ulimwengu wa kwanza na mapungufu yake yote vitakuwa vimeshatoweka, na ukweli tu ndio utakaokuwepo, kisha watakatifu wakamilifu watautawala Ufalme wote wa Mbinguni milele na milele.
 

Usivunjwe Moyo na Hali Yako ya Sasa
 
Kipindi hiki cha sasa ni kipindi cha giza na hali ya kutokuwa na tumaini. Katika nyakati hizi tumaini haliweza kupatikana popote pale, siku za mbele za nyakati hizi zimejawa na hali ya kutokuwa na hali ya mashaka. Na hii ndio sababu kwa baadhi ya nyakati tunajisikia kama tumechanganyikiwa na wadhaifu pamoja na kuwa tunaihubiri injili. Mimi mwenyewe, kwa baadhi ya nyakati moyo wangu umekuwa na huzini kwa sababu ya hali hii, lakini ninapolisoma Neno la Ufunuo na kuelezea vifungu vyake, nimetambua kwamba watakatifu na watumishi wa Mungu wanaokabiliana na nyakati za mwisho hawana cha kuwatia huzuni. Mungu ameuimarisha moyo wangu na kuufanya usipate shinda tena kwa kunifanya kutambua kwamba dhiki za sasa na mateso ni vya muda tu, na kwamba ulimwengu mzuri na angavu zaidi upo mbele yangu. 
Ikiwa tutaiangalia hali yetu ya sasa, ukweli ni kuwa maisha yetu yanatia huzuni sana, na hayafurahishi, kiasi kuwa tunashawishika kufa moyo kutokana na matatizo yasiyoisha yanayotupitia wakati tunapoitumikia injili. Lakini kwa sababu ya baraka zote za Bwana zinazotukaribia, ingawa baraka hizo zinaweza zisionekane kwa macho ya kimwili, basi mioyo yetu inawekwa huru kutokana na huzuni na badala yake inajazwa na tumaini kuu na furaha. Sababu inayofanya kwamba kusiwe na sababu ya sisi kuishi katika huzuni ni kwa kuwa Mungu wetu amekwisha tupatia Mbingu na Nchi Mpya. 
Je, unaamini katika Mbingu na Nchi Mpya? Pamoja na kuwa hujaweza kupata uzoefu wa vitu hivyo, je umewahi kuvitafakari? 
Dunia hii pia ina sehemu ambazo ni nzuri sana. Tunapozungumzia juu ya mazingira mazuri ya kuishi katika ulimwengu huu, mara nyingi huwa tunazungumzia kuhusu miti, malisho mazuri ya kijani kando ya mito, maua mashambani, na watu wema. Pia ni lazima kuwe mtiririko mzuri wa maji, na kwamba kusiwe na watu wabaya, wala kusiwe na mapungufu yoyote yale. Wakati mazingira hayo yote yanapokuwa yametimia, basi mara zote huwa tunasema hayo ni mazingira bora kabisa. Lakini huko Mbinguni, kila kitu ni kikamilifu, ni kwema na kuzuri zaidi kupitia mahali popote hapa duniani panapoweza kujisifu. 
Swali ni hili, Mungu ameuandaa Mji Mtakatifu uliojengwa kikamilifu toka Mbinguni ambao atauleta hapa duniani kwa ajili ya akina nani? Ukweli ni kuwa Mungu amufanya huu Mji si kwa watu wengine bali ni kwa ajili ya watakatifu. Na hii ndio sababu tunaweza kusahau kila kitu kuhusu dunia ya kwanza. Pamoja na kuwa tutaishi kwa utukufu katika Ufalme wa Milenia, ukweli ni kuwa katika ulimwengu ujao, yaani katika Mbingu na Nchi Mpya vinavyoelezwa katika sura ya 21, ambavyo Mungu anataka kutupatia, huko tutaishi pamoja na Bwana kwa utukufu mkuu zaidi. Ili kufanya hivyo, Mungu ametuokoa kwa kumtuma Yesu Kristo, kisha atatufufua na kutunyakua. Kuishi pamoja na Bwana katika miili iliyofanywa kuwa mikamilifu kama Mwili wa Yesu Mfufuka kunatoa picha kamilifu ya utukufu na maisha yaliyobarikiwa yanayotungojea. 
Ili kutupatia Ufalme wa Mbingu na Nchi Mpya, basi Mungu ametufanya wewe na mimi kuzaliwa katika dunia hii, na ametuokoa. Ikiwa watakatifu wanaishi katika ulimwengu huu hali wakiyatambua majaliwa ya Mungu, basi wataishi vizuri sana, tena pasipo kukutana na magumu, mateso, huzuni, na pasipo majonzi. Kwa kuangalia yale ambayo Bwana ameyafanya, na yale ambayo atayafanya kwetu sisi hapo baadaye, basi sisi sote tunaweza kuishi kwa ujasiri na kwa mtazamo chanya. 
Lakini ikiwa tutajiangalia sisi wenyewe na kisha kuiangalia hali isiyo na tumaini ya kisiasa, kiuchumi, na kijamii hapa duniani, tutaona wazi kwamba hakuna chaguo zaidi ya kuangukia katika hali ya huzuni. Wewe na mimi ni hatupaswi kusahau kwamba Mungu ametupatia Mbingu na Nchip Mpya kuwa vyetu. Huu ndio uhalisia. Huu ndio ukweli. Hata kama ulimwengu huu unajaribu kukufanya uwe na huzuni, kwa kweli usihuzunishwe na ulimwengu huu, wala usikasirishwe, bali umwangalie Bwana tu. Kisha uishi maisha yako kwa tumaini, hali ukiamini kwa hakika kwamba Bwana amewapatia Mbingu na Nchi Mpya watakatifu wake. 
Mungu alisema kwamba atavifanya vitu vyote kuwa vipya. Alimwambia Yohana kuyaandika Maneno haya, kwamba atafanya vitu vyote kuwa vipya, “ya kwamba maneno hayo ni amini na kweli.” Wale watakaoshiriki katika ufufuo wa kwanza pia watashiriki katika baraka hizi zote za kuishi mahali ambapo Mungu amefanya vitu vyote kuwa vipya. Hiki ni kitu ambacho hatuwezi hata kukiota kwa kutumia mawazo ya kibinadamu, bali ni kitu ambacho Mungu ameandaa kwa ajili ya watakatifu wake. Hivyo, watakatifu na vitu vyote vitampatia Mungu utukufu wote, shukrani, heshima, na kisha kumsifu Mungu milele kwa kulitimiza hili tendo kuu. 
Biblia inasema kwamba “imani ni kuwa na hakika na mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana (Waebrania 11:1).” Kwa maneno mengine, pamoja na kuwa hatuwezi kuyaona mambo haya kwa macho yetu, ukweli ni kuwa mambo hayo yote ni amini na kweli. Tulitumaini kuokolewa toka katiak dhambi zetu zote, na kwa kuamini katika wokovu wetu basi ni hakika kuwa tumeokolewa. Na kwa kuwa, baada ya kuokolewa, tumetamani na tumetumaini kuishi milele katika ulimwengu mkamilifu usiopungukiwa kitu, basi ni hakika kwamba Mungu ametimiza kila kitu kwa ajili yetu. Kila kitu ambacho tulikitamani na kukitumainia kitakuja kuwa halisi, hii ni kwa sababu matumaini yetu yote ni ya kweli.
Katika sura ya 10 ya Kitabu cha Ufunuo, wakati Bwana alipozungumza na Yohana kwa kupitia malaika wake aliyekuwa amesimama katika nchi na katika bahari, na wakati Yohana alipojaribu kuyaandika mambo hayo, Mungu alimwambia asiyaandike. Kati ya vitu ambavyo Bwana alivizungumza, kuna vitu ambavyo ni vya uhakika ambavyo Mungu hakuviruhusu kuandikwa, kwa kuwa mambo hayo ni siri ambayo ataifunua kwetu sisi watakatifu. 
Siri hii si nyingine bali ni unyakuo. Ili kufahamu kuwa ni lini hasa unyakuo utatokea, basi tunapaswa kwanza kutambua kuwa tarumbeta la saba la Mungu ndio kigezo kinachoamua na kuifumbua siri hii. Sasa, ni lini basi ambapo tarumbeta la saba litapigwa? Tarumbeta la saba litapigwa wakati miaka mitatu na nusu kati ya ile miaka saba ya Dhiki Kuu kuwa imepita kidogo. Hapo ndipo ufufuo na unyakuo wa watakatifu utakapotokea. Baada ya unyakuo huo kuisha, basi hapo yatafuatia mapigo ya mabakuli saba. 
Miaka kadhaa iliyopita, niliusikia mkutano mmoja wa uamsho uliokuwa na mada isemayo “Makanisa Saba ya Asia Ndogo.” Pia niliandika kitabu juu ya haya makanisa saba ya Asia Ndogo, na maelezo yake yanaendana vizuri na maelezo niliyoyaeleza katika kifungu hiki. Ninapoyaangalia yale mahubiri katika kile kitabu, ninaona wazi kwamba nyakati zimebadilika sana, lakini Neno la Mungu halijabadilika hata kidogo pamoja na kuwa muda mrefu umepita. 
Je, unataka kuishi katika Mbingu na Nchi Mpya, mahali ambapo Mungu amepaandaa kwa ajili yako wewe na mimi? Mapungufu ya ulimwengu huu hayapo katika ulimwengu huo mpya. Wakati Mungu aliposema kwamba atafanya vitu vyote kuwa vipya, baadhi ya watu wanaweza kutafsiri kwamba Mungu alisema kwamba atavibadilisha vile ambavyo tayari vipo katika ulimwengu huu, yana kwamba atavigeuza upya. Lakini kuanzia sura ya 21 na kuendelea, tunachoweza kukona hapo ni ulimwengu mpya kabisa, ulimwengu ambao ni tofauti kabisa na ulimwengu wa zamani. Wale waliozaliwa tena upya watashiriki katika Mbingu na Nchi Mpya vilivyofanywa upya na Mungu, hii ni kwa sababu wao ndio washiriki wa tabia-sifa za kimungu. Kwa maneno mengine, ni kwa sababu wamefanyika kuwa washiriki wa uwepo wa kimungu. 
Badala ya kuyaweka mawazo yetu yote katika dhana ya mali na vitu, sasa tunapaswa kufikiri katika vipimo vya kiroho. Ninaomba kwamba ninyi nyote muwe ni watakatifu na watumishi mnaoamini katika kile ambacho Mungu amezipatia roho zetu, na mnaoamini katika imani kwamba, ingawa mambo haya bado hayajatimizwa, basi ipo siku mambo haya yatakuwa halisi. Mungu ametupata baraka kuu. 
Mungu alisema kwamba atatoa chemichemi ya maji ya uzima bure kwa wale walio na kiu. Neno hili halimaanishi juu ya injili ya maji na Roho. Wakati watu wanapoamini kwamba Mungu amewakomboa toka katika kiu yao kwa kuwapatia injili yake hapa duniani na kwa kuwaokoa toka katika dhambi zao, na kwamba hii ni sawa na kuyanywa maji ya uzima. Lakini kifungu hiki hakimaanishi hilo tu, bali ina maanisha ni maji halisi ya uzima ambayo watu watayanywa katika Mbingu na Nchi Mpya, ambapo yeyote atakayeyanywa maji haya ya uzima hatakufa kamwe, mwili wake utabadilishwa na kuwa kama wa Bwana, naye ataishi na Bwana milele. 
Bwana Mungu wetu amepanga na kuyatimiza haya mambo yote, kuanzia mwanzo hadi mwisho. Mambo yote ambayo Bwana ameyafanya, ameyafanya kwa ajili yake na kwa ajili ya watakatifu wake. Kwa hiyo, watakatifu wanaitwa na Mungu kuwa ni watu wa Kristo na wamefanyika kuwa watoto wa kweli wa Mungu kwa mujibu wa mpango wake. Wale waliofanyika kuwa watakatifu kwa kuiamini injili ya maji na Roho sasa wanaweza kutambua, toka katika imani yao katika upendo mkuu wa Mungu na matendo yake ya ajabu, kwamba hakuna wanachopungukiwa katiak kumshukuru na kumsifu Bwana milele. 
Kama Bwana alivyosema, “Mimi nitampa yeye mwenye kiu, ya chemchemi ya maji ya uzima, bure.” Ni hakika kwamba Mungu ametupatia chemichemi ya maji ya uzima kwa watakatifu wake na amewaruhusu kufurahia uzima wa milele. Hii ni zawadi kuu ambayo Mungu amewapatia watakatifu wake. Sasa watakatifu wataishi milele katika Mbingu na Nchi Mpya na kisha kunywa katika chemichemi ya maji ya uzima, ambapo hawataona kiu tena milele. Kwa maneno mengine, watakatifu wamefanyika kuwa watoto wa Mungu ambao watakuwa na uzima wa milele, yaani kama vile Bwana Mungu, kisha wataishi katika utukufu. Ninampatia Bwana Mungu shukrani na utukufu tena kwa kutupatia baraka hii kuu. 
 

Imani Katika Injili ya Kweli Inatuwezesha Kuushinda Ulimwengu
 
Mtume Yohana sasa anarudi katika wakati wake. Aya ya 7 inasema, “Yeye ashindaye atayarithi haya, nami nitakuwa Mungu wake, naye atakuwa mwanangu.” “Yeye ashindaye” ina maanisha ni wale wanaoilinda imani iliyotolewa na Bwana. Imani hii inawaruhusu watakatifu wote kuyashinda matatizo yote na majaribu. Imani yetu katika Bwana Mungu na katika upendo wa kweli wa injili ya maji na Roho iliyotolewa na Mungu ndivyo vinavyotupatia ushindi dhidi ya dhambi zote za ulimwengu, na dhidi ya hukumu ya Mungu, na dhidi ya maadui zetu, na dhidi ya udhaifu wetu binafsi, na dhidi ya mateso ya Mpinga Kristo. 
Ninatoa shukrani na kumpatia Bwana Mungu wetu utukufu kwa kutupatia ushindi dhidi ya hayo yote. Wakatifu wanaomwamini Bwana Mungu wanaweza kumshinda Mpinga Kristo kwa imani yao, hii ni kwa sababu, Bwana Mungu wetu amempatia kila mmoja wao imani hii ambayo kwa hiyo anaweza kushinda katika mapambano yao dhidi ya maadui zao wote. Sasa, Mungu amewaruhusu watakatifu, ambao wameushinda ulimwengu na Mpinga Kristo kwa imani yao kuirithi Mbingu na Nchi Mpya. Ninatoa shukrani na kumsifu Mungu wetu kwa kutupatia imani hii imara. 
Mungu alisema kwamba kwamba kwa wale watakaoshinda, basi atawapatia Mbingu na Nchi Mpya kuwa urithi wao, mahali ambapo hakuna machozi, wala huzuni, wala mashaka. Ni wale tu watakaoshinda ndio watakaostahili kuipokea hiyo Mbingu na Nchi Mpya. Imani ya ushindi huu ni imani katika injili ya maji na Roho ambayo Bwana ametupatia. Hii ndio imani ambayo kwa hiyo tunaweza kuushinda ulimwengu, dhambi zetu, madhaifu yetu binafsi, na pia kumshinda Mpinga Kristo. 
Kama thawabu ya imani yetu inayomshinda Mpinga Kristo, basi hivi punde tutapokea Mbingu na Nchi Mpya toka kwa Mungu. Kwa kuwa tutapokea baraka hizi zote kwa ajili ya imani yetu, basi wakati Mpinga Kristo atakaposimama kinyume nasi na kujaribu kuichukua imani yetu, basi ni hakika kwamba tutaishinda mipango yote ya maadui zetu kwa imani. Wale wanaoshinda wanaliamini Neno la Mungu bila kujalisha kile ambacho wengine wanasema juu yao, na wanailinda imani yao katika ukweli kwamba Bwana amezichukulia mbali dhambi zao zote. Sisi, ambao tumepokea ondoleo la dhambi zetu na ambao tumezaliwa tena upya, na ambao tunaishi katika nyakati hizi za mwisho, ni lazima tuishinde mipango ya Mpinga Kristo kwa imani. 
Tunaweza kuishinda dhiki itakayodumu kwa muda mfupi kwa imani yetu katika ukweli kwamba Bwana ametupatia Mbingu na Nchi Mpya, pamoja na utajiri, heshima na utukufu. Wakati ulimwengu bora ukiwa unatuongojea, je, ni kweli kuwa tunaweza kuikana injili ya imani hii? Wakati mambo mema yatatujia kesho, na wakati ambapo vitu vingi vya kushangaza na kupendeza vinatungojea hiyo kesho, basi si hakika kwamba tutavumilia leo, yaani kuvumilia magumu ya siku ya leo? Ukweli ni kwamba sisi sote tunaweza kuvumilia. 
Biblia inatueleza mara kwa mara kuhusu ‘imani, tumaini na upendo’ kama vitu vya muhimu sana ambavyo watakatifu wanapaswa kuvitunza na kuvishikilia katika akili zao. Wale walio na tumaini wana uwezo zaidi wa kuishinda dhiki yao ya sasa kwa kuamini kwamba baraka hizi zote ambazo Mungu ametupatia ni vitu halisi. Na kwa kuwa mapigo ya nyakati za mwisho yatadumu kwa muda mfupi, na kwa kuwa Mungu atawapatia watakatifu wake njia ya kuyakwepa mapigo hayo, basi ni hakika kwamba sisi sote tunaweza kuvumilia. Ninatumaini kwamba kuanzia wakati huu na kuendelea, wewe nawe utaweza kuvumilia, na kwamba utakuwa tayari kuingia katika Mbingu na Nchi Mpya na kisha kuishi ndani yake kwa imani. 
Katika himaya ya imani, Neno hili lote ni lazima liuguse moyo wako kwa kupitia imani, na sio kugusa ngozi ya mwili wako. Linapofanya hivyo, basi moyo wako utakuwa imara kwa kuwa utapata nguvu mpya, na pia utakuwa na tumaini. 
Watakatifu wote watauawa na kuifia-dini katika nyakati za mwisho. Hali tukiliangalia tumaini ambalo tumeliweka katika Mbingu na Nchi Mpya, basi ndio maana tunaweza tena zaidi kuyapokea mauaji ya kuwa wafia-dini hali tukiwa na nguvu mpya. 
Katika uwepo wake, Bwana Mungu Wetu ni Mungu wa ukweli na Mungu wa upendo. Sasa, ni akina nani ambao basi kimsingi ni waoga mbele za Mungu? Ni wale ambao wamezaliwa wakiwa na dhambi ya asili na ambao hawajaziosha dhambi zao zote kwa Neno la injili ya maji na Roho iliyotolewa na Bwana. Kwa kuwa katika hali yao ya kimsingi wanamwamini yule mwovu kuliko kumwamini Mungu, na kwa sababu hiyo wamefanyika kwa wazi kuwa watumishi wa Shetani. Kwa kuwa wanamwabudu mwovu mbele za Mungu, na kwa kuwa wanaipenda giza na kuifuata kuliko kuipenda nuru, basi ndio sababu watu hao ni waoga mbele za Bwana Mungu. Wale wote ambao ni waoga mbele za Mungu watashiriki katika kuunguzwa katika ziwa la moto na kibiriti. 
Ni ukweli usio na shaka kwamba watu hawa, ambao wao wenyewe ni giza kwa sababu ya dhambi katika mioyo yao, basi ndio maana hawana uchaguzi mwingine zaidi ya kumwogopa Mungu. Wakati roho za wale walio mali ya Shetani wanapoipenda giza, basi ndio maana wanakuwa waoga mbele za Yesu ambaye amefanyika kuwa nuru. Na hii ndio sababu tunapaswa kuyachukua maovu na udhaifu wao kwenda kwa Mungu ili wapokee ondoleo la dhambi zao toka kwa Mungu. Wale wasioiamini injili ya maji na Roho iliyotolewa na Bwana ni wenye dhambi wakuu mbele za Mungu na ni maadui zake. 
Kwa kuwa nafsi zao ni machukizo, na kwa kuwa wanasimama kinyume na Mungu, huku wakipenda na kuzitenda dhambi nyingi, na kwa kuwa wanazifuata ishara za uongo, huku wakiabudu kila aina ya sanamu, na kusema maneno yote ya uongo, basi kwa kupitia hukumu ya Mungu ya haki watu hao wote watatupwa katika ziwa liwakalo kwa moto na kibiriti. Hii ndio adhabu yao ya mauti ya pili. 
Mauti ya pili itakuwa maalumu kwa wale ambao watakuwa wamepelekwa kuzimu, na hawa ndio wale waoga, wasioamini, wenye machukizo, wauaji, wazinzi, wachawi, na waabudu sanamu ambao pamoja na Mpinga Kristo na wafuasi wake, ambao kwa sasa hawaupokei upendo wa Mungu. Wale wasiomwamini Mungu ndio waovu zaidi. Biblia inatueleza kwamba hawa waovu wote watatupwa katika ziwa liwakalo kwa moto na kibiriti. Hii ndio sababu Biblia inayataja mauti hayo kuwa ni mauti ya pili. 
Wale watakaoshiriki katika ufufuo wa pili hawatakufa hata baada ya kuwa wametupwa katika moto, hii ndio sababu watafufuliwa katika miili ambayo itaishi milele ili waweze kutupwa katika moto. 
Wasiomwamini Mungu watainuliwa tena ili waweze kutupwa katika ziwa la moto na kibiriti. Ufufuo wa pili, ambao utaleta mateso ya milele katika moto wa kuzimu pasipo kufa, umehifadhiwa kwa ajili ya hawa watu wote wasioamini. 
Muda mfupi baada ya kumiminwa kwa mabakuli yenye mapigo saba, basi Ufalme wa Milenia utakamilishwa, na baada ya kupita miaka elfu moja, watakatifu watahamia katika Mbingu na Nchi Mpya. Na katika sentensi inayosema, “Nami nitakuonyesha yule Bibi-arusi, mke wa Mwana-Kondoo,” hili neno mke wa Mwana-kondoo lina maanisha ni wale waliookolewa kwa injili ya maji na Roho iliyotolewa na Yesu Kristo na kwa kuiamini injili hiyo. 
 

Utukufu na Uzuri wa Mji Mtakatifu Ni Zaidi ya Maelezo
 
Mji wa Yerusalemu una maanisha ni Mji Mtakatifu ambako watakatifu wataishi pamoja na Bwana-harusi wao. Huu Mji ambao Yohana aliuona kwa kweli ulikuwa ni mzuri sana na wa ajabu. Ulikuwa ni mji mkubwa, uliokuwa umepambwa kwa vito vya thamani ndani na nje, hali ukiwa safi na angavu. Malaika alimwonyesha Yohana mahali ambapo mabibi-harusi wa Yesu Kristo wataishi pamoja na Bwana-harusi wao. 
Hebu fikiria suala la kuishi mahali ambapo pamejengwa kwa vito vya dhamani. Katika Mji huu ambao umejengwa kwa aina kumi na mbili tofauti za vito vya thamani, ni mahali ambapo mabibi-harusi wa Mwana-kondoo wataishi milele. Mji huu ni zawadi ya Mungu ambayo ataitoa kwa mke wa Mwana-kondoo. Kifungu hiki kinatueleza kwamba mji wa Yerusalem unang’ara sana, na kwamba mwanga wake ni kama ule wa vito vya thamani, kama vile kito cha yaspi, kilicho angavu kama kioo. 
Hivyo, utukufu wa Mungu upo katika huo Mji na wale wote wanaoishi ndani yake. Mamlaka ya Mungu ni ile ya nuru, hivyo ni wale tu ambao wamesafishwa giza lote, udhaifu na dhambi zote ndio wanaoweza kuingia na kuishi katika Mji huu. Kwa hiyo, ili kuweza kuingia katika Mji huu Mtakatifu, basi inatupasa sisi sote kuliamini Neno la kweli la injili ya maji na Roho ambalo Bwana wetu ametupatia. 
Hiki kifungu kinaeleza kwamba Mji huu umezungukwa kwa ukuta mkubwa na mrefu wenye malango kumi na mbili. Pia kifungu hiki kinaeleza kwamba majina yameandikwa katika malango hayo, na majina hayo ni yale majina kumi na mbili ya kabila za wana wa Israeli. Mungu anatueleza kwa hakika kwamba ameuandaa mji huu kwa ajili ya watakatifu wake, na ameuzungushia ukuta mkubwa na mrefu. 
Hii ni alama ya kiroho kwamba njia ya kuingia katika huu Mji Mtakatifu ni ngumu sana. Kwa maneno mengine, kifungu hiki kinatueleza kwamba kuokolewa mbele za Mungu kwa kutegemea jitihada za kibinadamu au kutegemea mali na vitu vya ulimwengu huu ambavyo Mungu aliviumba ni jambo lisilowezekana. Ili kuweza kukombolewa toka katika dhambi zetu zote na kisha kuingia katika Mji Mtakatifu wa Mungu, basi ni muhimu sana kuwa na imani ambayo wanafunzi kumi na mbili wa Yesu walikuwa nayo, yaani imani inayoamini katika ukweli wa injili ya maji na Roho. Kwa hiyo, hakuna hata mmoja asiye na imani hii katika injili ya maji na Roho anayeweza kuingia katika huu Mji Mtakatifu. 
Mji huu unalindwa na malaika kumi na mbili waliosimama kama walinzi wa malango huku wakiwa wametumwa na bwana Mungu. Kwa upande mwingine, hii sentensi inayosema, “majina yameandikwa [milango],” inatueleza kwamba wamiliki wa Mji huu wamekwisha amuliwa, maana yake ni kwamba wamiliki wa Mji huu ni Mungu Mwenyewe pamoja na watu wake, na Mji huu ni mali ya watu wa Mungu ambao sasa wamefanyika kuwa watoto wake. 
Huu Mji Mtakatifu una malango matatu katika kila uelekeo wake wa kaskazini, kusini, mashariki, na magharibi. Nina hakika kwamba Bwana aliyataja haya malango matatu ili kutueleza kwamba yanahusiana hasa na injili ambayo tunaiamini. 1 Yohana 5:7-8 inaeleza kwamba kuna watatu wanaoishuhudia injili ya kweli huko Mbinguni na duniani. Ni wale tu wanaowaamini hawa mashahidi watatu Mbinguni na duniani ndio wanaoweza kuingia Mbinguni. Sisi, tuliozaliwa tena upya, tunamwamini Mungu Utatu na matendo yake ya haki ya kutuokoa kupitia maji, damu, na Roho. 
Ule ukweli kwamba majina ya mitume kumi na mbili yameandikwa katika misingi kumi na mbili ya huu Mji unatueleza kwamba Bwana amefanya kwa usahihi kabisa kama vile alivyoahidi, kwamba hatayatoweshea mbali majina yao kamwe katika Kitabu cha Uzima. 
Yadi, au ‘Stadion’ kwa Kiyunani, ni kipimo cha kupimia umbali, ni sawa na futi 600 (Mita 185) kwa vipimo vya sasa. Biblia inapotueleza kwamba kila upande wa ule Mji wa Mbinguni una yadi 12,000, basi hii inatueleza kwamba kila upande wa ule mji una urefu wa kilomita 2,220 sawa na (maili 1,390). Tunaambiwa kwamba urefu wake, upana, na kimo na sawa. Ukubwa wa Mji huu unatueleza jinsi Ufalme wa Mungu ulivyo mkuu na wa kushangaza. 
Maana ya kibiblia ya namba nne ni mateso. Imani ambayo Bwana anaihitaji kutoka kwetu si kitu ambachoa kila mtu anaweza kuwa nacho, bali ni imani ambayo wanaweza kuwa nayo wale tu wanaolipokea Neno la Mungu kama lilivyo, hata kama hawawezi kulielewa vizuri kwa ufahamu wao wa kibinadamu. 
Ukiwa kama Mkristo, haiwezekani kuingia katika Mji Mtakatifu wa Mungu kwa kuuamini Msalaba wa Yesu tu, huku ukisema Yesu ni Mungu na Mwokozi. Kama Bwana wetu alivyosema, hakuna anayeweza kuingia katika Ufalme wa Mungu hadi awe amezaliwa tena upya kwa maji na kwa Roho. Watu wanaweza kuzaliwa tena upya pale tu wanapoamini kwamba dhambi zote za ulimwengu zilizipitishwa kwenda kwa Yesu wakati alipobatizwa na Yohana Mbatizaji, na kwamba Yesu alizipatanisha dhambi zao zote kwa kuimwaga damu yake na kufa Msalabani kwa niaba yao. 
Sentensi inayosema, “na mji ule ulikuwa wa dhahabu safi, mfano wa kioo safi,” inatueleza kwamba ni wale tu ambao imani yao ni kama dhahabu—yaani, wale wanaomwamini Mungu kwa kweli—ndio wanaoweza kuingia katika ule Mji. Sentesi hii inatueleza pia kwamba imani inayomruhusu mtu kuingia katika Mji Mtakatifu wa Bwana ni ile imani inayoliamini Neno la Mungu kama lilivyo andikwa, imani ambayo ni safi na iliyo mbali na mambo ya kidunia. Kwa maneno mengine, sentensi hii inatueleza kwamba imempasa mtu kulipokea Neno la Mungu la kuzaliwa tena upya kwa maji na Roho katika usafi wake wote, kisha kuliamini Neno hili kwa kweli, na hatimaye kuwa na imani iliyofanywa upya. 
Misingi ya ule ukutwa wa Mji imepambwa kwa aina zote za vito vya thamani, na hii inatueleza kwamba tunaweza kutiwa faraja na kuimarishwa kwa namna mbalimbali za kiimani toka katika hili Neno la Bwana wetu. Ni lazima tuwe na imani yenye nidhamu, na si bora imani katika injili ya maji na Roho au tumaini katika Mbingu na katika Ufalme wa Milenia. Imani hii ya kufundishwa pia inatujia kupitia Neno la Mungu wakati ambapo tukiyavumilia mateso ya sasa. 
Sio kwamba Bwana amewapatia watakatifu wake baraka ya ondoleo la dhambi zao tu, bali amewapatia pia baraka ya kuyatimiza matumaini yao, kwamba wale wote waliosamehewa dhambi zao wataingia katika Ufalme wa Milenia na Mbinguni. Sisi, watakatifu, tunaweza kumshukuru Mungu kwa kuturuhusu kuingia katika Mbingu na Nchi Mpya, mahali ambako hakuna huzuni wala majonzi. 
Watakatifu ambao watauingia Mji Mtakatifu wanapaswa kuwa na uvumilivu wa kutosha wanapokuwa hapa duniani, hali wakiwa wamesimama imara katika kiini cha imani yao. Kwa maneno mengine, wale wanaoliamini Neno la kweli lililozungumzwa na Bwana Mungu, wanahitaji kuwa na uvumlifu mkuu katika kuilinda imani yao. Nyakati za mwisho zitakapowadia, basi kipindi cha Mpinga Kristo, ambaye ni mpinzani wa imani, kitawasili. 
Huyu Mpinga Kristo, akiwa kama mtumishi wa Shetani, ataleta mateso kwa watu wengi wa kiimani, huku akiwataka waikane imani yao. Ikiwa watu watasimama upande wa Mpinga Kristo na kisha kuiacha imani yao, basi ni dhahiri kwamba watashindwa kuufikia Ufalme wa Milenia na Mbinguni, na watatupwa kuzimu pamoja na Shetani. 
Hivyo, tutakapokuwa katikati ya majaribu, mateso, na mapigo ya nyakati za mwisho, basi ni dhahidi kwamba tutahitaji uvumilivu utakaoturuhusu kuilinda imani yetu kikamilifu, kwa kuwa uvumilivu huu wa kutoshtushwa na usioyumba ndio utakaotupatia Mbingu na Nchi Mpya. 
Kuishi katika Mbingu na Nchi Mpya ni sawa na kuishi ukiwa umekumbatiwa katika mikono ya Bwana. Kwa kuwa Yesu Kristo, ambaye amefanyika kuwa nuru ya ulimwengu mpya, anang’aa katika nchi hii takatifu akiwa ndio nuru yake, na kwa sababu hiyo hakuna haja ya kuwa na mwanga wa jua wala mwezi. Yesu Kristo ni Mwokozi wetu, Muumbaji, na Hakimu, na katika Mbingu na Nchi Mpya, Yesu ni Mungu ambaye anaishi pamoja nasi. Tunaingia Mbinguni kupitia Yeye, na kwa yeye huyo baraka zote zinatiririka. Watakatifu hawatakuwa na la kufanya zaidi ya kumsifu Bwana wakati wote. 
Katika toleo la Biblia la Mfalme Yakobo, aya ya 24 imeandikwa kama ifuatavyo: “Na mataifa watatembea katika nuru yake. Na wafalme wa nchi huleta utukufu wao ndani yake.” Andiko hili linaposema utukufu wa duniani unaletwa Mbinguni, hii haimaanishi kwamba wale waliokuwa wametawala katika dunia ya kwanza, ati kwa kuwa walikuwa matajiri, wataleta utajiri wao katika Mbingu na Nchi Mpya. Dunia inayotajwa hapa ni dunia ya Ufalme wa Milenia. 
Pamoja na kuwa watakatifu wameokolewa na kwamba wataingia katika Ufalme wa Milenia kwa namna moja, ukweli ni kwamba watapewa mamlaka mbalimbali, wengine watatawala juu ya miji kumi, na wengine juu ya miji mitano, hii itategemea na jitihada zao katika kuihubiri injili wakati walipokuwa wakiishi katika ulimwenguni wa kwanza. 
Kile ambacho aya ya 24 inatueleza ni kwamba hawa wafalme ambao walikuwa na mamlaka mbalimbali watahamia katika Mbingu na Nchi Mpya. Kwa maneno mengine, wale waliotawala katika Ufalme wa Milenia wataingia katika Mbingu na Nchi Mpya wakiwa kama wafalme huku wakiileta imani yao katika Bwana pamoja na heshima na utukufu. Hivyo, aya hii haijishughulishi na dunia hii ya kwanza ambapo sisi sote tunaishi hivi sasa. 
Kwa kuwa Mbingu na Nchi Mpya, mahali ambapo Mji Mtakatifu upo, imekwishajazwa na na mwanga mtakatifu, basi huko hakuwezi kuwa na giza au usiku kamwe, wala hakuan mwovu hata mmoja. Wale wote wasioufahamu ukweli wa injili ya maji na Roho miongoni mwa Wakristo na wasio Wakristo, kwa ujumla wao hao wote ni watenda maovu, ni wenye machukizo, na waongo. Hivyo hawawezi kuingia katika Mji Mtakatifu. Kwa kuwa yeyote anayeiamini injili ya maji na Roho anaweza kuingia Mbinguni, basi hii injili ya maji na Roho ni ufunguo wa kuingia Mbinguni na ufunguo wa ondoleo la dhambi. Unapaswa kuelewa kuwa unapotambua na kuamini kwamba Mungu amekupatia funguo hii, basi ni hakika kwamba jina lako litaandikwa katika Kitabu cha Uzima. Na unapoupokea ukweli wa injili hii, basi ni wazi kuwa utavikwa baraka ya kuingia katika huu Mji Mtakatifu. 
Amini kwamba tumeshapewa Mji Mtakatifu. Na kisha uishi maisha yako kwa imani kama ipasavyo hali ukiwa na tumaini. 
Kwa kuwa kila kitu tunachokabiliana nacho katika wakati huu kinapimwa kwa mfumo wa thamani wa ulimwengu huu wa kimwili, basi ndio maana hatuwezi kuipima kikamilifu furaha ya kweli. Lakini tunapopima kwa kutumia kipimo cha Mungu, basi hapo tunaweza kutambua kwamba wale walio na milki ya Mbinguni ndio wenye furaha ya kweli. Kwa nini? Kwa kuwa hivi punde au baadaye, mambo ya ulimwengu huu yatatoweka yote. Mambo hayo ya kidunia yatatoweka na kutuacha bila mahali pa kuliweka tumaini letu, mambo hayo yatatoweka mara baada ya kuletwa kwa dhiki na mapigo kwa mujibu wa mpango wa Mungu. Hakuna kitu kitakachokuwa cha kijinga kama kuweka tumaini katika vitu hivyo vya kimwili ambavyo vitaoza na kisha kuungua na kuwa majivu. 
Lakini kwa upande mwingine, wale wanaoliweka tumaini lao katika Ufalme wa Mbinguni wa milele ambao hauwezi kuoza wala kuungua ndio waliobarikiwa. Ni wale tu wasio na dhambi ndio wanaoweza kuingia Mji Mtakatifu wa Yerusalemu ulioandaliwa na Mungu. Watu walio na furaha zaidi katika ulimwengu huu ni wale ambao Mbingu ni urithi wao, watu ambao dhambi zao zote zimesamehewa na kusafishiliwa mbali. 
Tunapaswa kuishi maisha yetu hali tukiwa tumebarikiwa na Mungu, tukiwa wale tunaompatia Mungu utukufu kwa kutupatia Mbingu na Nchi Mpya, na ambao tumejitoa katika kuihubiri injili ya kweli inayoiwezesha kila nafsi kuingia Mbinguni. 
Hebu sisi sote tuishi kwa baraka hizo, hebu tupendwe na Mungu, ili kwamba siku moja tutakaposimama mbele za Bwana, tuishi milele tukiwa tumekumbatiwa katika mikono ya Mungu.