Search

Mahubiri

Somo la 10: Ufunuo (Ufafanuzi juu ya Ufunuo)

[13-1] Kutokea Kwa Mpinga Kristo (Ufunuo 13:1-18)

(Ufunuo 13:1-18) 
“Kisha nikaona mnyama akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba, na juu ya pembe zake ana vilemba kumi, na juu ya vichwa vyake majina ya makufuru. Na yule mnyama niliyemwona alikuwa mfano wa chui, na miguu yake ilikuwa kama miguu ya dubu, na kinywa chake kama kinywa cha simba, yule joka akampa nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi. Nikaona kimoja cha vichwa vyake kana kwamba kimetiwa jeraha la mauti, na pigo lake la mauti likapona. Dunia yote ikamstaajabia mnyama yule. Wakamsujudu yule joka kwa sababu alimpa huyo mnyama uwezo wake; nao wakamsujudu yule mnyama, wakisema, Ni nani afananaye na mnyama huyu? Tena ni nani awezaye kufanya vita naye? Naye akapewa kinywa cha kunena maneno makuu, ya makufuru. Akapewa uwezo wa kufanya kazi yake miezi arobaini na miwili. Akafunua kinywa chake amtukane Mungu, na kulitukana jina lake, na maskani yake, nao wakaao mbinguni. Tena akapewa kufanya vita na watakatifu na kuwashinda, akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa. Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu, kila ambaye jina lake halikuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo, aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia. Mtu akiwa na sikio na asikie. Mtu akichukua mateka, atachukuliwa mateka. Mtu akiua kwa upanga, atauawa kwa upanga. Hapa ndipo penye subira na imani ya watakatifu. Kisha nikaona mnyama mwingine, akipanda juu kutoka katika nchi; naye alikuwa na pembe mbili mfano wa Mwana-Kondoo, akanena kama joka. Naye atumia uwezo wote wa mnyama yule wa kwanza mbele yake. Naye aifanya dunia na wote wakaao ndani yake wamsujudie mnyama wa kwanza, ambaye jeraha lake la mauti lilipona. Naye afanya ishara kubwa, hata kufanya moto kushuka kutoka mbinguni uje juu ya nchi mbele ya wanadamu. Naye awakosesha wale wakaao juu ya nchi, kwa ishara zile alizopewa kuzifanya mbele ya huyo mnyama, akiwaambia wakaao juu ya nchi kumfanyia sanamu yule mnyama, aliyekuwa na jeraha la upanga naye akaishi. Akapewa kutia pumzi katika ile sanamu ya mnyama, hata ile sanamu ya mnyama inene, na kuwafanya hao wote wasioisujudu sanamu ya mnyama wauawe. Naye awafanya wote, wadogo kwa wakubwa, na matajiri kwa maskini, na walio huru kwa watumwa, watiwe chapa katika mkono wao wa kuume, au katika vipaji vya nyuso zao; tena kwamba mtu awaye yote asiweze kununua wala kuuza, isipokuwa ana chapa ile, yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake. Hapa ndipo penye hekima. Yeye aliye na akili, na aihesabu hesabu ya mnyama huyo; maana ni hesabu ya kibinadamu. Na hesabu yake ni mia sita, sitini na sita.”
 

Ufafanuzi
 
Aya ya 1: Kisha nikaona mnyama akitoka katika bahari, mwenye pembe kumi, na vichwa saba, na juu ya pembe zake ana vilemba kumi, na juu ya vichwa vyake majina ya makufuru.
Mtume Yohana alimwona mnyama akitoka katika bahari. Mungu anatuonyesha sisi kile ambacho Mpinga Kristo atakifanya mara atakapotokea hapa duniani kwa kupitia Mnyama huyu ambaye Yohana alimwona. Mungu alimwonyesha Yohana huyu Mnyama mwenye vichwa saba na pembe kumi si kwa kumaanisha kwamba atatokea mnyama wa jinsi hii na kisha kuonekana duniani, bali alifanya hivyo ili kutuonyesha kwamba mtu fulani mwenye mamlaka na nguvu za huyu Mnyama atakuja kutokea, atawatesa watakatifu, na kisha atawaua kama wafia-dini.
Je, hii ina maanisha kwamba kila kitu kinachoonekana katika Ufunuo ni lugha ya picha? Si kweli kabisa! Mungu alitumia maono ya jinsi hiyo ili kufunua kutokea kwa Mpinga Kristo na kazi zake katika nyakati za mwisho. Hii ni hekima na nguvu ambazo ni Mungu peke yake ndiye anayeweza kuongea. Kwa kupitia Neno la Ufunuo 13, tunapaswa kuiona picha ya wazi kabisa ya nyakati za mwisho.
Kile ambacho Yohana alikiona kwanza ni umbile la mnyama aliyetoka baharini. Hivi vichwa saba vya mnyama pamoja na pembe zake kumi zina maanisha ni nguvu za Mpinga Kristo zinazotoka hapa ulimwenguni. Hii sentensi inayosema, “na juu ya pembe zake ana vilemba kumi, na juu ya vichwa vyake majina ya makufuru,” maana yake ni kwamba Mpinga Kristo atawakusanya mataifa ya ulimwengu ili kusimama kinyume na Mungu. Pia sentensi hii inatueleza kwamba huyu Mpinga Kristo atawatawala wafalme wote wa ulimwengu. Vile vilemba kumi vina maanisha ni ushindi wao, na yale majina ya makufuru katika kichwa cha Mnyama yana maanisha ni kiburi na majivuno yao.
Hapo baadaye, ulimwengu utatawaliwa na kamati ya umoja wa mataifa, utawala huu utazingatia mfumo unaotelekeza matakwa ya jumla ya nchi zilizoungana. Hizi nguvu kuu zilizoungana, ambazo muungano wa mataifa makubwa, wataupanua utawala wao na kisha kuyatawala mataifa yote ya ulimwengu, na hatimaye watazitenda kazi zote za Mpinga Kristo mara atakapokuwa ametoka hapa duniani. Mpinga Kristo ni adui wa Mungu, yeye anayefanya kazi hali akiwa amevikwa nguvu za Shetani, pia yeye ni mtumishi wa Ibilisi.
 
Aya ya 2: Na yule mnyama niliyemwona alikuwa mfano wa chui, na miguu yake ilikuwa kama miguu ya dubu, na kinywa chake kama kinywa cha simba, yule joka akampa nguvu zake na kiti chake cha enzi na uwezo mwingi.
Neno hili linatueleza kile ambacho Mpinga Kristo atakifanya kwa watakatifu na kwa watu wa ulimwengu mara baada ya kuonekana kwake. Mpinga Kristo anayekuja atafanya vitu vya kikatili kwa watakatifu kwa kuwa atakuwa amepokea mamlaka na nguvu toka kwa Shetani ili kufanya mambo hayo. Hii inatuonyesha jinsi Mpinga Kristo atakavyowafanyia watakatifu kwa sumu mara baada ya kuonekana kwake, na hii inaonyesha ni aina gani ya mateso ambayo watakatifu watakabiliana nayo toka kwa Mpinga Kristo na hatimaye kushinda kwa kuuawa kama wafia-dini.
Neno hili linatuonyesha jinsi Mpinga Kristo alivyo katili. Sentesi inayosema, “na miguu yake ilikuwa kama miguu ya dubu,” inaonyesha jinsi nguvu zake zilivyo na uharibifu. Na huyu “Joka” kwa asili yeye alikuwa ni malaika aliyeumbwa na Mungu, na ambaye alishindana na Mungu kwa ajili ya kiti cha enzi cha Mungu. Mnyama anayeonekana katika sura hii ana maanisha ni yule aliyepokea mamlaka toka kwa Joka na anayefanya kazi ya kusimama kinyume na Mungu na watakatifu wake.
Shetani, ambaye alikuwa ni malaika aliyefukuzwa Mbinguni, atatoa nguvu na mamlaka yake kwa yule ambaye atasimama kinyume na Mungu, na kisha kumwongoza kwenye mauti yake kwa kumfanya apigane na Mungu na watakatifu wake. Mpinga Kristo, hali akiwa amevikwa nguvu za Shetani, atawanyanyasa watu wa Mungu na wanadamu wote kwa ukatili hapo baadaye.
 
Aya ya 3: Nikaona kimoja cha vichwa vyake kana kwamba kimetiwa jeraha la mauti, na pigo lake la mauti likapona. Dunia yote ikamstaajabia mnyama yule.
Aya hii inatueleza kwamba Mpinga Kristo atatokea kama mmoja wa wafalme saba. Mpinga Kristo anatajwa pia kama Mnyama kwa kuwa atatenda vitu vya kinyama kwa watakatifu.
Hapa, adui wa Mungu na wa watakatifu atatokea kama anayeweza kutatua hata tatizo la kifo katika nyakati za mwisho. Kwa hiyo, watu wengi wa nyakati za mwisho watamwamini kwamba anaweza kutatua matatizo yote yanayoipiga dunia. Lakini yeye ni adui wa Mungu. Pamoja na kuwa atawafanya watu wa kidunia kusalimu amri mbele zake, ukweli ni kwamba hatimaye ataangamizwa kwa kitendo chake cha kusimama dhidi ya Mungu na watakatifu wake.
 
Aya ya 4: Wakamsujudu yule joka kwa sababu alimpa huyo mnyama uwezo wake; nao wakamsujudu yule mnyama, wakisema, Ni nani afananaye na mnyama huyu? Tena ni nani awezaye kufanya vita naye?”
Hii aya inatueleza kwamba yule Joka atazitoa nguvu zake zote kwa yule anayefanya mambo ya kinyama, ambaye atakuwa amemgeuza kuwa mtumishi wake. Kwa sababu ya jambo hili, watu wote wa ulimwenguni watamfikia yule Joka kana kwamba ni mungu, huku wakitetemeka kwa hofu, na kisha kumwabudu. Kwa kuwa wakati huo hakuna mfale yeyote katika dunia hii atakayekuwa na nguvu alizonazo Joka, basi hakuna hata mmoja atakayeweza kumzuia asijitangaze kuwa yeye ni mungu.
Kwa kuwa Joka anampatia huyo Mnyama nguvu kuu, basi kila mtu atamheshimu Joka na Mnyama na kisha kumwabudu huyu Mnyama kama mungu wao. Wakati Mpinga Kristo akiwa amepokea nguvu za jinsi hiyo atakapoonekana, wale wanaopenda giza kuliko nuru watamfuata, kisha watamwabudu kama mungu wao, na watamwinua juu sana.
 
Aya ya 5: Naye akapewa kinywa cha kunena maneno makuu, ya makufuru. Akapewa uwezo wa kufanya kazi yake miezi arobaini na miwili.
Mnyama atapokea toka kwa Joka moyo wenye kiburi na majivuno na atapokea pia mamlaka ya kuongea maneno ya kujisifu kwa miaka mitatu na miezi sita (miezi 42). Hivyo, mnyama atapokea mamlaka ya kuwadhuru watakatifu na watu wa hapa ulimwenguni kwa miaka hii mitatu na nusu.
Mnyama, ambaye ni Mpinga Kristo, atapokea mamlaka ya kunena maneno yanasimama kinyume na Mungu na kulikufuru Kanisa lake kwa miaka mitatu na nusu. Hivyo, wenye dhambi wote wataishia kusalimu amri kwa huyu Mnyama, na hivyo mwishowe wataingia katika maangamizi yao pamoja na huyo Mnyama.
 
Aya ya 6: Akafunua kinywa chake amtukane Mungu, na kulitukana jina lake, na maskani yake, nao wakaao mbinguni.
Huyu Mnyama, baada ya kuwa amepokea mamlaka toka kwa Joka, atamkufuru Mungu, pamoja na malaika wake wote na watakatifu kwa miaka mitatu na miezi sita, huku akimlaani Mungu na kuwapinga. Mambo haya yote yatatokea kwa jinsi anavyoelekezwa na Joka. Hapa, tunapaswa kutambua na kuamini kwamba tendo hili la Shetani—yaani la kumpatia Mnyama mamlaka yake ili kumkufuru Mungu kwa miaka mitatu na nusu—litawezekana kwa ruhusa ya Mungu tu.
Kimsingi, Mpinga Kristo yupo ili kumkufuru Mungu na wake wake. Baada ya kupokea mamlaka toka kwa Joka, Mpinga Kristo atalikufuru jina la Mungu na watu wake kwa miaka miatatu ya nusu ya kwanza katika ile miaka ya Dhiki Kuu.
 
Aya ya 7: Tena akapewa kufanya vita na watakatifu na kuwashinda, akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa.
Mnyama atapokea mamlaka toka kwa Joka ya kuwaua watakatifu wote na hivyo kufanya wafia-dini kati ya watakatifu. Baada ya kuwa amepewa mamlaka ya kumtiisha kila mtu katika ulimwengu huu chini ya utawala wake, basi atautawala pia ulimwengu wote.
Mpinga Kristo atawaua watakatifu, hii ni kwa sababu njia pekee ya yeye kuweza kuutawala ulimwengu ni kwa yeye kupambana na kisha kuwashinda watakatifu. Huyu anayevuta kamba ya waya ya Mpinga Kristo ni Ibilisi, malaika aliyeanguka na ambaye anataka kuabudiwa kama Mungu anavyoabudiwa. Hivyo, kwa tendo lake la kuwaua watakatifu, basi wale ambao hawajazaliwa tena upya watamhusudu. Katika wakati huu wa Dhiki, watakatifu wote watateswa na kisha kuuawa na Mpinga Kristo na kuwa wafia-dini.

Aya ya 8: Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu, kila ambaye jina lake halikuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo, aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia.
Wakati Mpinga Kristo atakapokuwa ameishinda dunia hii na kuifanya mateka, basi kila mtu isipokuwa wale waliozaliwa tena upya kwa kuamini katika injili ya maji na Roho—au wale wote ambao watakuwa hawajazaliwa tena upya—watamwabudu Mpinga Kristo kama mungu wao. Lakini huyu Mpinga Kristo ataabudiwa na wenye dhambi tu ambao majina yao hayajaandikwa katika Kitabu cha Uzima.
 
Aya ya 9: Mtu akiwa na sikio na asikie.
Hii inatueleza kwamba yeyeote ambaye yupo katika kundi la watu wa Mungu ni lazima aiandae imani yake tayari kwa kuuawa na kuwa mfia-dini, kwa kuwa mambo haya yote yatatimizwa kama yalivyoandikwa katika Maandikko.
 
Aya ya 10: Mtu akichukua mateka, atachukuliwa mateka. Mtu akiua kwa upanga, atauawa kwa upanga. Hapa ndipo penye subira na imani ya watakatifu.
Hapa Mungu anasema kwamba ataleta kifo kile kile na dhiki kwa wale wote waliowaua watakatifu waliozaliwa tena upya katika nyakati za mwisho. Baada ya kupita kwa miaka mitatu na nusu katika miaka ya ile Dhiki, basi watakatifu watauawa na Mpinga Kristo na wafuasi wake. Lakini kwa wale ambao watakuwa wamewaua watakatifu, basi Mungu atawalipiza kwa dhiki kuu zaidi na mateso. Kwa hiyo, watakatifu wote ni lazima waiunganishe mioyo yao, waishinde hii Dhiki ngumu kwa imani yao katika Neno la bwana, na kisha wampatie Mungu utukufu kwa kuyapokea mauaji na kuwa wafia-dini.
 
Aya ya 11: Kisha nikaona mnyama mwingine, akipanda juu kutoka katika nchi; naye alikuwa na pembe mbili mfano wa Mwana-Kondoo, akanena kama joka.
Hapa tunachoona si yule Mnyama wa kwanza, bali ni mnyama wa pili. Huyu mnyama wa pili anafikiri na kuongea pia kama Joka. Sio kwamba anafikiri kana kwamba yeye ni kama Joka, lakini matendo yake yote yatawekwa katika imani yake, naye atawatesa watakatifu kwa ukatili zaidi. Huyu mnyama ni nabii wa Mpinga Kristo. 
Aya ya 12: Naye atumia uwezo wote wa mnyama yule wa kwanza mbele yake. Naye aifanya dunia na wote wakaao ndani yake wamsujudie mnyama wa kwanza, ambaye jeraha lake la mauti lilipona. 
Mnyama wa pili, hali akiwa amepewa nguvu ya Mnyama wa kwanza, atamsujudu Mnyama wa kwanza na kisha kumfanya yeyote atakayekuwa yupo hapa duniani kumwabudu huyo Mnyama pia. Kazi yake itakuwa ni kuzifanya sanamu za Mnyama wa kwanza na kisha kumfanya kila mtu kuiabudu sanamu hiyo kama vile Mungu. Kwa sababu ya kazi hii, Mnyama wa kwanza ataabudiwa kana kwamba yeye ni Mungu. Hii ndiyo hali yake ni udhihirisho wa kweli wa Shetani. 
 
Aya ya 13: Naye afanya ishara kubwa, hata kufanya moto kushuka kutoka mbinguni uje juu ya nchi mbele ya wanadamu. 
Kwa kuwa Shetani atafanya miujiza mingi hapa duniani mbele ya macho ya wanadamu, basi ataweza kuwadanganya watu wengi. Atakuwa na nguvu ya kuweza hata kuufanya moto utoke mbinguni kuja duniani. 
 
Aya ya 14: Naye awakosesha wale wakaao juu ya nchi, kwa ishara zile alizopewa kuzifanya mbele ya huyo mnyama, akiwaambia wakaao juu ya nchi kumfanyia sanamu yule mnyama, aliyekuwa na jeraha la upanga naye akaishi.
Lakini muda si mrefu, Shetani atazifunua rangi zake halisi. Anachotaka kukifanya ni kuiiba imani ya Mungu toka katika mioyo ya watu na kisha kuwafanya wamwabudu yeye. Ili kufanikisha jambo hili, atafanya miujiza mingi mbele za wanadamu na kisha atawaua watu wa Mungu. Ili kulitimiza dhumuni lake la mwisho—yaani kuwa kama Mungu—basi Shetani atajaribu kujiinua ili kuwa sawa na Mungu. Hivyo atafanya sanamu ya Mnyama wa kwanza na kuwafanya watu wamwabudu kama vile ni Mungu.
 
Aya ya 15: Akapewa kutia pumzi katika ile sanamu ya mnyama, hata ile sanamu ya mnyama inene, na kuwafanya hao wote wasioisujudu sanamu ya mnyama wauawe.
Kwa kuwa kikwazo kikuu cha yeye kujifanya kuwa Mungu ni watu wa Mungu, basi Shetani atafanya kila awezalo kuwaondolea mbali. Hivyo atawaua wale wote ambao hawaiabudu sanamu ya Mnyama, atafanya hivyo bila kujalisha wingi wa watu hao. Lakini watakatifu hawatasalimu amri kwa Mnyama huyu. Kwa hiyo, watakatifu wengi wakati huo watakuwa tayari kupokea vifo vya kuifia-dini kwa imani yao, huku wakiangalia zaidi maisha yao ya baadaye baada ya kufa. Kwa kuwa Mpinga Kristo atakuwa ameleta mateso makuu kwa watakatifu, basi Mungu atamwandalia mapigo ya mabakuli saba na adhabu ya kuungua milele huko kuzimu.
 
Ayay ya 16-17: Naye awafanya wote, wadogo kwa wakubwa, na matajiri kwa maskini, na walio huru kwa watumwa, watiwe chapa katika mkono wao wa kuume, au katika vipaji vya nyuso zao; tena kwamba mtu awaye yote asiweze kununua wala kuuza, isipokuwa ana chapa ile, yaani, jina la mnyama yule, au hesabu ya jina lake.
Wakati Dhiki itakapofikia kiwango chake cha juu, Mpinga Kristo atawataka watu wote kuipokea alama au chapa katika mikono yao ya kulia au katika vipaji vyao vya nyuso, atafanya hivyo ili kuhakikisha kwamba kila mtu anakuwa chini ya himaya yake. Alama au chapa hii ni alama ya Mnyama. Mpinga Kristo atawalazimisha watu kuipokea alama yake ili kuwafanya watu wote kuwa watumishi wake.
Hali akishikilia maisha ya watu kama vile dhamana yake, basi Mpinga Kristo ataendelea na mipango yake ya kisiasa. Hivyo atamfanya yule asiye na alama ya Mnyama, ambayo ni uthibitisho wa utii kwake, kutoweza kununua wala kuuza kitu chochote. Alama hii jina la Mnyama au namba yake. Wakati Mnyama atakapokuja hapa ulimwenguni hapo baadaye, basi kila mtu atatakiwa kuipokea alama yake, alama iliyotengenezwa kwa jina lake au namba yake. Hivyo, ni lazima tujikumbushe juu ya onyo la Mungu kwamba wale wote watakaoipokea alama yake watatupwa katika ziwa la moto na kibiriti.
 
Aya ya 18: Hapa ndipo penye hekima. Yeye aliye na akili, na aihesabu hesabu ya mnyama huyo; maana ni hesabu ya kibinadamu. Na hesabu yake ni mia sita, sitini na sita.
Namba ya huyu Mnyama ni 666. Kwa kifupi, hii ina maanisha kwamba huyu Mnyama anakazia kwamba yeye yupo sawa na Mungu. Je, kuna namba yoyote inayoonyesha kwamba, “Mwanadamu ni Mungu?” Namba inayobeba maana hiyo ni namba ya Mpinga Kristo. Kwa hiyo, watakatifu hawawezi kuipokea alama hii, kwa kuwa Mungu Utatu ndiye Mungu wetu wa kweli. Watakatifu ni lazima wamshinde Shetani kwa imani yao katika Bwana na kisha kumpatia Mungu utukufu. Hii ni imani nzuri na ibada ambayo kwa hiyo watakatifu wanaweza kumpatia Bwana utukufu. Hebu tushinde kwa imani yetu.
 

Maelezo ya Maneno Makuu
 
Mada ya sura ya 13 inaongelea juu ya kuonekana kwa Mpinga Kristo na Shetani. Baada ya kuonekana kwao, watakatifu wapambana nao katika vita ya kiroho, ambayo hatimaye hawatakuwa na la kufanya zaidi ya kuuawa na kuifia-dini kwa mkono wa Mpinga Kristo. Mpinga Kristo ni mtumishi wa Shetani, na ndiye atakayewatesa watakatifu na kuwafanya wafe kwa kuifia-dini.
Wakristo wote na wasio Wakristo wanaoishi katika kipindi cha sasa wanapaswa kulifahamu Neno la Ufunuo. Sura ya 13 ya Ufunuo inatabiri kwamba utafika wakati ambapo Shetani atamfanya Mpinga Kristo kuwa kama Mungu. Shetani atatoa mamlaka yake kw ammoja wa viongozi wenye nguvu wa kisiasa wa hapa ulimwenguni na atamfanya kiongozi huyo kusimama kinyume na Mungu na watakatifu wake. Kimsingi, Mpinga Kristo atajifanya kama Mungu na kisha kumshambulia Mungu.
Kila mtu wakiwemo watu wa Mungu watateseka sana kutokana na dhiki na mateso yatakayoletwa na Mpinga Kriso mnyama. Kifungu kikuu kinaonyesha kwamba sanamu ya Mpinga Kristo, baada ya kuwa imepokea pumzi ya uhai ya Shetani, itaweza kuongea kama vile ipo hai, pia itakuwa na mamlaka ya kuwadhuru watu. Hivyo wale ambao hawajazaliwa tena upya watasalimu amri kwa Mpinga Kristo na kisha kuwa watumishi wake. Kwa upande mwinegine, wale wote wasioiabudu sanamu ya Shetani, watauawa bila kujalisha idadi yao. Pia Shetani atawafanya wote kuipokea alama yake au namba yake katika mikono yao ya kulia au katika vipaji vya nyuso zao.
Sisi sote tunapaswa kuiandaa imani yetu mapema, na kisha tupambane na kumshinda Shetani kwa imani yetu hapo baadaye kwa kufahamu na kuamini juu ya maana ya Neno hili lililofunuliwa katika Ufunuo 13. Watu wa Mungu wa leo wanapaswa kumpatia Bwana utukufu kwa kujifunza na kuliamini Neno hili la Ufunuo, na hivyo kusimama imara dhidi ya Mpinga Kristo na kisha kumshinda kwa ushindi.
 
 
Asili ya Kuzimu 
 
Kwanza tunapaswa kufahamu ni kwa nini kuwe na kuzimu na kwamba ilianzia wapi hadi ikawepo. Kuzimu ni mahali palipoandaliwa kwa ajili ya Shetani. Biblia inatueleza kwamba yeye hakuwa Shetani tangu mwanzo, bali alikuwa ni mmoja wa malaika wengi walioumbwa na Mungu. Lakini kwa sababu ya kumbishania Mungu kwa ajili ya kiburi na majivuno yake, basi malaika huyu aligeuka na kuwa Shetani kama mshahara wa dhambi yake, na kuzimu ni mahali ambapo Mungu alipaumba ili aweze kumfungia huko. Mungu aliifanya kuzimu ili aweze kumpatia Shetani pamoja na wafuasi wake adhabu iliyohifadhiwa kwa ajili ya wale wote wanaosimama kinyume na Mungu.
Isaya 14:12-15 inaleza jinsi malaila huyu alivyoishia kugeuka kuwa Shetani: “Jinsi ulivyoanguka kutoka mbinguni, Ewe nyota ya alfajiri, mwana wa asubuhi! Jinsi ulivyokatwa kabisa, Ewe uliyewaangusha mataifa! Nawe ulisema moyoni mwako, Nitapanda mpaka mbinguni, Nitakiinua kiti changu juu kuliko nyota za Mungu; Nami nitaketi juu ya mlima wa mkutano, Katika pande za mwisho za kaskazini. Nitapaa kupita vimo vya mawingu, Nitafanana na yeye Aliye juu. Lakini utashushwa mpaka kuzimu; Mpaka pande za mwisho za shimo.”
Malaika huyu aliyesimama kinyume na Mungu huko Mbinguni alikifanyia hila kiti cha enzi cha Mungu. Baada ya kuona kwamba ni Mungu tu ndiye aliyekuwa juu ya kiti cha enzi, basi huyu malaika aliwaza kumwondoa ili yeye aweze kukikalia kiti cha enzi cha Mungu, lakini kama matokeo ya uasi huu ulioshindwa, malaika huyo alifukuzwa na Mungu toka Mbinguni na hatimaye akaishia kuwa Shetani. Pia Biblia inawataja malaika wengine waliomfuata Shetani kuwa ni mapepo.
Mungu aliitengeneza sehemu hii inayoitwa “kuzimu” ili kuitoa adhabu yake ya haki kwa viumbe ambao waligeuka na kuwa kinyume na Mungu. Ingawa Shetani anaweza kuonekana kama anamletea Mungu changamoto bila ukomo huku akizikufuru kazi zake, basi ukweli ni kwamba injili ya maji na Roho itakapohubiriwa kwa wote, basi Shetani huyu atafungwa katika shimo la kuzimu lisilo na mwisho kwa miaka elfu moja.
Kwa kuwa kimsingi Shetani hataitubia dhambi yake ya kugeuka na kuwa kinyume na Mungu, basi ataendelea kujiinua ili awe juu kama Mungu, na hatimaye ataishia kupokea adhabu ya kutisha huko kuzimu milele. Shetani ataendelea kusimama kinyume na Mungu na kinyume na wenye haki kwa kuwafanya watu wamfanye yeye kuwa Mungu hadi mwisho. Biblia inamtaja huyu malaika aliyeanguka na anayemkufuru Mungu na watakatifu wake, kuwa ni Shetani au Ibilisi, na Joka wa kale (Ufunuo 12:9).
 

666, Namba ya Mnyama 
 
Hatimaye Mungu atamfunga Shetani katika gereza lake. Lakini kabla ya kufungiwa kuzimu, Shetani atawafanya watu waipokee alama ya 666, ambayo ni jina na namba yake, katika mikono yao ya kulia au katika vipaji vya nyuso zao. Atakamkataza mtu yeyote asiyekuwa na alama hii kununua au kuuza chochote.
Namba 7 ni namba ya ukamilifu, ambayo ina maanisha kuwa ni Mungu. Kwa upande mwingine, namba sita ina maanisha ni mwanadamu, hii ni kwa sababu Mungu alimwumba mwanadamu katika siku ya sita kwa sura na mfano wake. Hii namba ya Mnyama, yaani 666, ina onyesha kiburi cha mwanadamu kwa kujaribu kuwa kama Mungu Utatu. Muda si mrefu, utafika wakati hapa uliwenguni ambapo wanadamu wataipokea alama hii ya 666.
Ufunuo 13:1 inatueleza kwamba wafalme saba watatokea kati ya mataifa kumi. Kati yao, yeye aliye na nguvu kuu, na aliyepewa mamlaka toka kwa Shetani, atauweka ulimwengu huu chini ya utawala wake. Atafanya miujiza mikuu kama vile kuliponya jeraha lake la kufa na kuleta moto toka mbinguni kuja duniani, atawafanya watu wote wa ulimwengu kumfuata.
Kwa maneno mengine, kadri Shetani anavyowafanya watu kumfuata kuliko kumfuata Mungu, basi watu wengi wataishia kumwabudu yeye kama Mungu. Kama vile mashujaa wanavyoinuka wakati wa shida, Mpinga Kristo, baada ya kuwa amepokea mamlaka makuu toka kwa Shetani, atataka kufuatwa na kila mtu kama Mungu, atafanya hivyo kwa kuyatatua matatizo ya kisiasa na ya kiuchumi ambayo ulimwengu itakuwa ikikabiliana nayo. Hatimaye, Shetani atazidhirisha rangi zake kwa kujaribu kumpa Mungu changamoto katika nyakati za mwisho.
Kama tunavyoweza kuona atoka katika Kitabu cha Danieli, Dhiki Kuu itageuka na kuwa kali sana itapofikia nusu yake ya kwanza, ambayo itadumu kwa miaka mitatu na nusu, na kipindi hiki ni cha mapigo ya kutisha na kipindi cha utawala wa Shetani wenye nguvu. Lakini mara baada ya kuisha kwa miaka hii mitatu na nusu, basi kitakachofuata ni dhiki kuu sana kama bomu. Wakati huu, Shetani atapewa mamlaka kuzifanya kazi zake kati ya watu ulimwenguni, huku akimuua yeyote asiyemsikiliza, huku akiwadanganya wanadamu kwa miujiza yake inayoweza kuleta moto toka angani, atajifanyia kuwa Mungu, na kisha atawafanya wanadamu kuzifanya kazi za machukizo dhidi ya Mungu.
Wakati huo huo, Mpinga Kristo, baada ya kuwa amepokea mamlaka toka kwa Shetani, awakufuru watakatifu kuwaua watakatifu wote wasiomtii yeye. Kama aya ya 7-8 inavyotueleza, “Tena akapewa kufanya vita na watakatifu na kuwashinda, akapewa uwezo juu ya kila kabila na jamaa na lugha na taifa. Na watu wote wakaao juu ya nchi watamsujudu, kila ambaye jina lake halikuandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo, aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia.” Hata hivyo, wapo wale ambao watakataa kumwabudu Mnyama wakati huo, na hao si wengine bali ni wale watu wa Mungu waliozaliwa atena upya na ambao majina yao yameandikwa katika Kitabu cha Uzima cha Mwana-kondoo.
 

Tukio la Mauji ya Wafia-dini
 
Mauji ya wafia-dini ni tukio ambalo litatokea wakati watakatifu waliozaliwa tena upya kwa kuamini katika injili ya maji na Roho watakapoilinda imai katika Bwana kwa kuikataa alama ya Shetani. Kwa lugha nyingine, Dhiki Kuu itafikia kiwango chake cha juu itakapokaribia mwisho wa miaka mitatu na nusu katika ile miaka ya Dhiki. Wakati huu, wenye haki ni lazima wajiandae kwa mauaji ya kuifia-dini.
Hata hivyo, wale ambao hata kama wanamwamini Yesu kama Mwokozi wao, watakuwa hawajaiamini injili ya maji na Roho, na kwa sababu hiyo kutopokea ondoleo la dhambi zao na hivyo kubaki na dhambi katika mioyo yao, wataishia kuwa upande wa Shetani na hatimaye kusalimu amri. Hii ni kwa sababu Wakristo wanaomwamini Yesu lakini ambao hawajazaliwa tena upya hawana Roho Mtakatifu katika mioyo yao, basi wakibilishwa na msukosuko kidogo, wote hao wataishia kusalimu amri kwa Shetani, na kisha kuipokea alama yake katika mikono yao ya kulia au katika vipaji vya nyuso zao, na hatimaye watamwabudu yeye kana kwamba ni Mungu.
Ni lazima tufahamu kwa wazi kwamba wale wasiomwabudu Shetani wakati huo watakuwa ni wale tu waliopokea ondoleo la dhambi zao. Pia tunapaswa kutambua kwamba Mungu ametueleza bayana kwamba atawatupa wale wote watakaosalimu amri kwa Mnyama pamoja na Shetani katika ziwa la moto na kibiriti.
Aya ya 9-10 inatueleza kwamba, “Mtu akiwa na sikio na asikie. Mtu akichukua mateka, atachukuliwa mateka. Mtu akiua kwa upanga, atauawa kwa upanga. Hapa ndipo penye subira na imani ya watakatifu.” Wakati huu, Mpinga Kristo na wafuasi wake wataleta mateso makuu kwa wenye haki, watawatoa na kisha kuwaua kwa mapanga yao. Hata hivyo, tunachopaswa kukitambua hapa ni kwamba ni hakika kuwa Mungu atatulipia kisasi kwa adui zetu wanaowaua na kuwatesa wenye haki.
Kwa hiyo, watakatifu ni lazima wayapitie mateso na vifo kwa kuziamini ahadi za Mungu. Ikiwa Mungu hangelipanga kutulipia kisasi tungeliwezaje kuifumbia macho haki yetu? Lakini kwa vile Mungu alimeahidi kutulipia kisasi kwa adui zetu wanaotudhuru, basi ni hakika kwamba vifo vyetu hazitaishia kwenye utupu. Ni hakika kwamba Mungu atalipa kisasi kwa wale wote wanaowatesa na kuwanyanyasa wenye haki, kisha atawaongoza wenye haki kuelekea katika ufufuo wao, kunyakuliwa, na katika karamu ya harusi ya Mwana-Kondoo, na atawafanya kutawala pamoja na Bwana kwa miaka elfu moja nao wataishi na Bwana milele. Sisi sote tunaamini juu ya hili na tuna tumaini hivyo. Hivyo, Bwana wetu ndiye Mungu bora ambaye atayatimiza matumaini yetu yote.